LIVE STREAM ADS

Header Ads

Maombi kwa wafanyakazi kuelekea Sikukuu ya Mei Mosi 2023

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Mchungaji wa Kanisa la Moravian Kusini Kati Tanzania Parishi ya Singida Mjini, Yona Mbogo (kushoto) akiongoza maombi ya kuwaombea wafanyakazi kuelekea sherehe za Mei Mosi 2023 zitakazofanyika kesho duniani kote katika maombi yaliyofanyika leo Aprili 30, 2023 wakati wa siku ya uimbaji iliyofanyika kanisani hapo.


Na Dotto Mwaibale, Singida
Kanisa la Moravian Kusini Kati Tanzania Parishi ya Singida Mjini kuelekea Sikukuu ya Wafanyakazi Mei Mosi 2023 limewaombea wafanyakazi wote nchini ili wawe na afya bora na kuweza kufanyakazi zao mbalimbali kwa ajili ya kuinuka kiuchumi na taifa kwa ujumla.

Ombi hilo limetolewa na Mchungaji wa kanisa hilo, Yona Mbogo wakati akiongoza maombi maalum ya kuwaombea wafanyakazi katika siku ya uimbaji iliyofanyika leo Aprili 30 katika kanisa hilo lililopo Mwenge Manispaa ya Singida.

"Siku ya leo tupo katika ibada hii kwa ajili ya kuwaombea wafanyakazi wote walio ajiriwa, kujiajiri, wakulima, wafanyabiashara, sekta binafsi na wengine wote wanaofanya kazi kwa mikono yao ili wapate baraka za mafanikio kutoka kwa Mungu kuelekea kilele cha Sikukuu ya wafanyakazi itakayofanyika duniani kote kesho Mei Mosi, 2023," alisema Mchungaji Mbogo.

Alisema pamoja na kuwaombea wafanyakazi hao pia wanawaombea wale wote ambao wanachangamoto ya kutokuwa na kazi ambao wanazungka na vyeti vyao ili wapate kazi na wale wenye kazi warudi kwenye madhabahu ya Mungu kumtolea sadaka baada ya kupata mafanikio yaliyotokana na kazi zao" alisema Mbogo.

Mchungaji Mbogo aliwataka wafanyakazi kufanya kazi kwa bidii kwa uweza wa Mungu na si kutumia nguvu za giza, kufanya matambiko, uchawi, chuma ulete na mambo mengine yanayofanana na hayo kwa lengo la kuzuia mafanikio ya watu wengine.

Aidha, Mchungaji Mbogo alisema watu wote wanaoharibu kazi, uchumi na maisha ya watanzania kwa namna mbalimbali wapingwe kwa nguvu zote kwani huo sio mpango wa Mungu.



Mchungaji Mbogo aliwataka wafanyakazi wote na kila mmoja kwa shughuli anayoifanya wakiwemo wanafunzi baada ya sikukuu hiyo kuendelea kufanya kazi na kusoma kwa bidii ili kuliinua taifa kiuchumi kwani hata biblia imeeleza asiyefanya kazi na asile.

Katika siku hiyo ya uimbaji kwaya mbalimbali na waimbaji mmoja mmoja walipata fursa ya kuimba nyimbo za kumtukuza Mungu na kusifu.
Mchungaji Mbogo akiongoza maombi hayo.
Kwaya ikitoa burudani
Mwanadada Eva akiongoza kwaya huku akiimba kwa umahiri wa hali ya juu.
Kwaya ya wanaume ikifanya yake katika siku hiyo ya uimbaji.
Kwaya ya watoto wa kanisa hilo ikinogesha uimbaji katika siku hiyo ya uimbaji.
Maombi ya kuwaombea wafanyakazi yakiendelea.
Muumini wa kanisa hilo, Fotunatus Mkoma akiwa katika maombi makali ya kuwaombea wafanyakazi.
Maombi ya kuwaombea wafanyakazi yakiendelea.

No comments:

Powered by Blogger.