LIVE STREAM ADS

Header Ads

CHAMA CHA WAGANGA NA TIBA ASILIA TANZANIA (CHAWATIATA) CHALAANI VIKALI MAUAJI YA ALBINO.

Kutoka Kushoto ni Hamis Hassan ambae ni Mwenyekiti wa Chama cha Waganga na Tiba Asilia Tanzania CHAWATIATA akifuatiwa na Kawawa Athumani ambae ni Katibu, anaefuata ni Jumanne John ambae ni Mjumbe akifuatiwa na Steven Sebastian ambae ni Katibu Mwenezi Mkoa wa Mwanza.
Na: George Binagi-GB Pazzo
Chama cha Waganga na Tiba Asilia Tanzania CHAWATIATA Mkoa wa Mwanza Kimelaani na Kukemea vikali Mauaji ya Watu wenye Ulemavu wa ngozi ambayo yameshamiri hapa nchini huku pia kikitoa onyo kali kwa waganga wa jadi wanaochafua taaluma hiyo kwa kujihusisha na ramli chonganishi kujisalimisha wenyewe polisi kabla hawajatiwa nguvuni.

Kauli hiyo ilitolewa jana Mkoani Mwanza yalipo Makao Makuu ya Chama hicho na Kawawa Athuman ambae ni Katibu wa Chama hicho wakati akizungumza na Wanahabari juu ya Kushamiri kwa vitendo vya Ukatili, Utekwaji na Mauaji kwa watu wenye Ulemavu wa ngozi hapa nchini sanjari na Oparesheni ya Jeshi la Polisi inayoendelea katika maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwa na lengo la kuwasaka waganga wa kienyeji wanaojihusisha na ramli chonganishi.

“Awali ya yote natoa tamko kwa niaba ya kamati ya CHAWATIATA Mkoa wa Mwanza kulaani mauaji yote ya Albino yanayotendeka katika Mkoa wa Mwanza na Tanzania nzima kwa ujumla na vilevile ninalaani wale wote wanaotumia kimvuli cha Waganga wa Tiba Asilia kama wao ndio waganga”. Alisema Athuman huku akiongeza kuwa,

“Hakika tiba asilia ni ni tiba ambayo ipo kihalali na kisheria lakini kwa sababu tiba hii imevamiwa na wavamizi ambao si watu wanaitwa waganga, tunaweza tukasema ni wavamizi wa waganga, hao ni majambazi wa waganga, hao ni maharamia katika uganga huu, wanajihusisha na Mauaji ya Albino ambao wanakuja kuchafua taasisi au taaluma ya watu ambao wamerithi miaka nenda rudi”. Alisema Athuman huku akiwatahadharisha waganga wote wanaojihusisha na upigaji wa ramli chonganishi kujisalimisha polisi kabla hawajatia nguvuni na jeshi hilo.

Nae Steve Sebastian ambae ni Katibu Mwenezi CHAWATIATA Mkoa wa Mwanza aliitahadharisha jamii kuwa makini na baadhi ya watu wanaotumia mazingaombwe huku wakijiita ni waganga kwa kuwa watu hao ni matapeli kwani wakiweka matangazo mbalimbali kuonyesha kuwa wanatengeneza pesa jambo linachochochea mauaji ya Watu wenye ulemavu wa ngozi ambapo aliodokeza kuwa CHAWATIATA imeanza kuwabaini watu hao na inashirikiana na Serikali kiupitia jeshi la polisi kwa ajili ya kuwakamata watu hao ambao wamekuwa wakijitangaza kuwa ni waganga.

Kwa upande wake Jumanne John ambae ni Mjumbe wa CHAWATIATA Wilaya ya Nyamagana aliwaomba waganga wote kushirikiana kwa pamoja na Serikali kwa lengo la kulaani mauaji ya Albino na Vikongwe huku akiongeza kuwa yeye hajui Albino anatibu nini wala hajui ngozi ya mtu inatibu nini hivyo Ushirikiano wa pamoja unahitajika kwa lengo la kukomesha mauaji ya Watu wenye ulemavu wa ngozi pamoja na vikongwe hapa nchini.


Kauli ya CHAWATIATA Mkoa wa Mwanza imekuja siku moja baada ya Jeshi la Polisi Mkoani Mwanza kupitia kwa Kamanda Valentino Mlowola kueleza kuwatia nguvuni waganga 55 wakiwa na vitu mbalimbali ambavyo vinaaminika kutumika katika Shughuli za Upigaji Ramli ambayo imepigwa marufuku na Serikali kutokana na kuleta uchonganishi katika jamii ikiwa ni pamoja na kuongeza vitendo vya Ukatili, Utekwaji na Mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi hapa nchini hususani katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa.
Hamis Hassan ambae ni Mwenyekiti wa Chama cha Waganga na Tiba Asilia Tanzania CHAWATIATA akionyesha namna wanavyohifadi dawa za mitishamba kwa ajili ya tiba mbalimbali.

No comments:

Powered by Blogger.