LIVE STREAM ADS

Header Ads

WANAHABARI WAIPINGA SHERIA MPYA YA HUDUMA ZA VYOMBO VYA HABARI MAHAKAMA KUU.


Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na kampuni ya Hali Halisi Publishers Limited leo tarehe 18 Januari 2017 wamefungua kesi katika Mahakama Kuu ya Tanzania Mwanza wakidai kuwa sheria ya Huduma ya Vyombo vya Habari, 2016 inakiuka katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Sheria hiyo ilipitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Novemba 5, 2016 na kuridhiwa na Rais Novemba 16, 2016.

Katika kufungua kesi hiyo, timu ya wanasheria Fulgence Massawe, Edwin Hans, Jenerali Ulimwengu, Jebra Kambole, Francis Stolla na Mpale Mpoki, wanaziwakilisha taasisi hizo katika Mahakama Kuu.

Walalamikaji wanadai kuwa baadhi ya vifungu vya sheria hiyo vinakandamiza uhuru wa habari na uhuru wa kujieleza, vinakiuka Ibara ya 18 ya katiba ya nchi. 

Ibara ya 18 inatoa haki kwa kila mtu kuwa na uhuru wa maoni na kueleza fikra zake, kutafuta, kupokea habari bila ya kujali mipaka ya nchi, uhuru wa kufanya mawasiliano na haki ya kutoingiliwa katika mawasiliano hayo.

Katiba pia inatoa haki kwa kila mtu kupewa taarifa wakati wote kuhusu matukio mbalimbali muhimu kwa maisha na shughuli za wananchi na pia kuhusu masuala muhimu katika jamii.

Baadhi ya vifungu katika sheria hiyo vinavyolalamikiwa ni pamoja na 7 (2) (b) (iii) (iv) and (v), 7 (3) (a), (b), (c), (f), (g), (h), (i), (j),8, 13, 14, 19, 20, 21, 24, 25, 26, 35, 36, 37, 38, 39, 40, 50, 52, 53, 54 58 na 59 vya sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari Na. 12 ya 2016.

UTPC na Hali Halisi Publishers Limited wanahimiza umuhimu wa kufuata kanuni za utawala bora, utawala wa kidemokrasia, utawala wa sheria, uwajibikaji, uwazi, haki kwa wote, usawa wa kijinsia na kulinda na kuheshimu haki za binadamu nchini kote.
Abubakar Karsan
Mkurugenzi Mtendaji
Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC)

No comments:

Powered by Blogger.