LIVE STREAM ADS

Header Ads

MAADHIMISHO YA SIKU YA WAZEE DUNIANI YAFANA MKOANI SHINYANGA

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Kila tarehe Moja ya Mwezi Oktoba (Oktoba Mosi) ni siku ambayo dunia nzima huadhimisha siku ya Wazee kwa lengo la kuwatambua na kuwaenzi wazee.

Mkoa wa Shinyanga umeadhimisha siku hii muhimu jana katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Shinyanga ambapo mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack.
Kauli mbiu ya mwaka huu ni “Kuelekea uchumi wa viwanda;Tuthamini mchango,uzoefu na ushiriki wa wazee kwa maendeleo ya taifa”.

Akihutubia katika maadhimisho hayo,Matiro alisema serikali inatambua umri wa mzee ni kuanzia miaka 60 na kuendelea na kwamba kila mmoja anapaswa kutambua kuwa siku moja ataufikia uzee hivyo wazee wanapaswa waheshimiwe,watunzwe na kuenziwa.

“Nawasihi tutumie hekima na ushauri walionao wazee wetu na siyo kuanza kuwafanyia vitendo vya ukatili kwa kuwanyanyasa,kuwatenga na kuwaua kwa imani potofu,na serikali itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa watakaonyanyasa wazee kwa namna yoyote ile”,alisema Matiro.

Katika hatua nyingine aliziagiza halmashauri za wilaya mkoani Shinyanga ambazo hazijatekeleza zoezi la kutambua wazee na kuwapatia kadi za matibabu bila malipo.

“Mkoa wetu una wazee 59,871 waliotambuliwa,kati yao waliopata kadi za matibabu bila malipo ni 7,553,waliopatiwa kadi z za mfuko wa afya ya jamii ni 4,613,bado idadi ni ndogo..Nawaagiza wakuu wa wilaya kuhakikisha kuwa kila mzee aliyetambuliwa anapata kadi ya matibabu bila malipo kabla ya tarehe 30.10.2017”,alieleza Matiro akisoma hotuba kwa niaba ya mkuu wa mkoa.

Aidha aliwahakikishia wazee kuwa mkoa wa Shinyanga utaendelea kuhakikisha kuwa dawa zote za magonjwa ya wazee zinapatika kwenye vituo afya huku akiwataka wakurugenzi wa halmashauri kufanya ukaguzi wa dawa na fedha kwa kila robo ya mwaka.
Alitoa rai kwa uongozi wa idara za afya kuanzia ngazi ya mkoa kuhakikisha kuwa uwepo wa vyumba maalum vya kutolea huduma za afya kwa wazee na kuwapa kipaumbele na kuweka ujumbe wa “Mpishe Mzee Apate Huduma Kwanza”.

"Kuelekea uchumi wa viwanda;Tuthamini mchango,uzoefu na ushiriki wa wazee kwa maendeleo ya taifa,kila mmoja atimize wajibu wake ili wazee wetu wapate huduma bora katika nyanja zote",aliongeza.

Akisoma risala,Katibu mkuu wa Baraza la Ushauri la Wazee mkoa wa Shinyanga,Underson Lyimo aliomba changomoto zinazowakumba wazee zishughulikiwe ili wazee waishi kwa amani na usalama.

“Bado wazee hawaheshimiki,wanatengwa na kunyanyaswa na hata kuuawa,tunaomba tabia hizi zikomeshwe,hatua stahiki ziendelee kuchukuliwa kwa wanaokiuka haki za binadamu na elimu itolewe kwa jamii kuhusu sera ya taifa ya wazee,haki na wajibu wa kuwalinda wazee”,alisema Lyimo.

Maadhimisho ya siku ya wazee duniani mkoa wa Shinyanga yameenda sambamba na zoezi la kugawa kadi za matibabu bure kwa wazee 7,553.

Pia kumefanyika zoezi la upimaji afya kwa wazee wote pamoja na wananchi wengine ambapo washiriki wa maadhimisho hayo wamepima bure magonjwa yasiyoambukiza kama kisukari,shinikizo la damu,magonjwa ya macho na mengineyo. 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza katika maadhimisho ya siku ya wazee duniani mkoa wa Shinyanga kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack.Kushoto ni Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la Wazee mkoa wa Shinyanga, Faustine Masale Sengerema,kushoto ni Katibu mkuu wa Baraza la Ushauri la Wazee mkoa wa Shinyanga,Underson Lyimo. 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro alitumia fursa hiyo kuwaomba wazee kushiriki katika kampeni ya upandaji miti inayoendelea mkoani Shinyanga.
Wazee wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza katika maadhimisho hayo ya siku ya wazee.
Aliyesimama ni Kaimu katibu tawala mkoa wa Shinyanga Alfred Shayo akizungumza katika maadhimisho hayo ya siku ya wazee ambapo alisema 'Wazee ni hazina na uzee ni dawa hivyo jamii inategemea ushauri wa wazee ili kujenga taifa".
Wazee wakiwa katika maadhimisho hayo.
Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la Wazee mkoa wa Shinyanga, Faustine Masale Sengerema akizungumza katika maadhimisho ya siku ya wazee ambapo alisema wazee wanaunga mkono jitihada mbalimbali zinazofanywa na rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. John Pombe Magufuli katika kuwaletea maendeleo wananchi.
Wazee wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea....
Katibu mkuu wa Baraza la Ushauri la Wazee mkoa wa Shinyanga,Underson Lyimo akisoma risala ambapo alizipongeza halmashauri zilizofanikisha zoezi la kutoa kadi za matibabu bila malipo kwa wazee zikiongozwa na halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.Aliyeshikilia kipaza sauti ni Afisa Maendeleo ya Jamii Sekretarieti ya mkoa wa Shinyanga Glory Mbia.
Mganga mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Dkt. Rashid Mfaume,Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la Wazee mkoa wa Shinyanga, Faustine Masale SengeremaMkuu wa wilaya ya Shinyanga,Josephine Matiro wakifuatilia risala.
Mganga mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Dkt. Rashid Mfaume akizungumzia kuhusu upatikanaji wa dawa mkoani humo.Alisema suala la changamoto ya dawa limepungua kutokana na vituo vya afya kuwa na fedha za kutosha za kununulia dawa na vifaa tiba.
Madaktari wakiwa katika eneo la tukio
Afisa ustawi wa Jamii mkoa wa Shinyanga,Lydia Kwezigabo akielezea kuhusu zoezi la kutambua wazee katika mkoa wa Shinyanga ambapo alisema jumla ya wazee 59,871 wametambuliwa na kati yao 7,553 sawa na asilimia 12.8 wamewakabidhi kadi za matibabu bila malipo na kuitaji wilaya ya Shinyanga kuwa ndiyo yenye idadi kubwa ya wazee waliopatiwa kadi hizo.Kulia ni Afisa Maendeleo ya Jamii Sekretarieti ya mkoa wa Shinyanga Glory Mbia.
Mganga mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Dkt. Rashid Mfaume akionesha moja ya kadi za matibabu bila malipo zilizoandaliwa kwa ajili ya kuwapatia wazee waliotambuliwa.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akikabidhi kadi ya matibabu bila malipo kwa mzee Faustine Masale Sengerema ambaye ni miongoni mwa wazee 7,553 wanaopatiwa kadi hizo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akikabidhi kadi ya matibabu bila malipo kwa mzee Philipo Njabuga
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akikabidhi kadi ya matibabu bila malipo kwa Bi. Sayi Zengo
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akikabidhi kadi ya matibabu bila malipo kwa Bi. Suzana Shija.
Wataalam wa afya wakiwa katika eneo la tukio.
Wazee wakiteta jambo wakati wa zoezi la upimaji afya kwa magonjwa yasiyoambukiza.
Mtaalam akimpima macho mmoja wa wazee waliojitokeza kupima afya zao.
Zoezi la upimaji afya likiendelea
Vijana wa Compassion wakiimba wimbo kuhusu "Amani"
Waandishi wa habari wakiwa eneo la tukio.
Na Kadama Malunde - Malunde1 blog

No comments:

Powered by Blogger.