Naibu Waziri Doto Biteko aahidi neema kwa wachimbaji wadogo nchini
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Naibu Waziri
wa Madini Mhe.Doto Biteko amewaagiza Maafisa Madini nchini kuhakikisha
wanatenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo, badala ya kutoa kipaumbele kwa
wachimbaji wakubwa pekee.
Aidha
Mhe.Biteko amesema serikali itaendelea kuwatufia leseni ya uchimbaji watu wote
waliohodhi maeneo makubwa yenye madini bila kuyaendeleza ili wachimbaji wadogo
wapatiwe maeneo hayo.
Mhe.Biteko
aliyasema hayo Julai 17, 2018 wakati akizungumza na wachimbaji wadogo katika
wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika
Kijiji cha Masugulu.
“Ilani ya
uchaguzi ya CCM ukurasa wa 35 tamko namba 25 imetuelekeza tukawatengee maeneo
ya kuchimba wachimbaji wadogo. Na mimi nimekuja kuwapa taarifa kwamba mtu
yeyote kwenye Wizara ya Madini asiyefuata utaratibu huo hataki kazi yake”.
Alisema Mhe. Biteko na kuongeza;
“Ninachukua
nafasi hii kuwaagiza Maafisa Madini wote nchini wakiwemo wa Songea, wasikilizeni
wachimbaji wadogo, marufuku kumuona tajiri wa maana kuliko masikini. Hawa
tukiwasimamia vizuri, matajiri watatoka humu”. Alisisitiza Mhe.Biteko.
Awali
Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji na Wafanyabiashara wa Madini mkoani Ruvuma
(RUVREMA), Isaack Ngerangera alimpongeza Rais Dkt.John Pombe Magufuli kwa
kuchukua hatua stahiki ili kulinda rasilimali madini nchini ikiwemo kufanya
marekebisho ya sheria ya madini.
Ngerangera
alisema wachimbaji wadogo mkoani Ruvuma wanaamini baadhi ya changamoto zinazowakabili
ikiwemo ukosefu wa maeneo ya uchimbaji zitatatuliwa ambapo aliomba wapewe baadhi
ya maeneo ambayo yamekaliwa na watu wenye leseni ambazo hawazifanyii kazi na
hivyo kuikosesha serikali mapato.
Naye Mkuu wa
Mkoa Ruvuma Mhe.Christina Mndeme alisema serikali itaendelea kupima maeneo kwa
ajili ya shughuli mbalimbali ikiwemo uchimbaji madini, ufugaji pamoja na kilimo
na hivyo kuwataka wananchi kuheshimu maeneo hayo kwa kufanya shughuli zao bila
kuingiliana ili kuepuka migogoro isiyo ya lazima.
Naibu Waziri wa Madini Mhe.Dotto Biteko akizungumza na wachimbaji wadogo wa madini katika Kijiji cha Masugulu wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma
Wachimbaji wadogo wilayani Mbinga wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa Ruvuma Mhe.Christina Mndeme baada ya Naibu Waziri wa Madini Mhe.Doto Biteko kukutana na wachimbaji hao akiwa ziarani mkoani humo
Mmoja wa wananchi akinasa ujio wa Naibu Waziri wa Madini katika Kijiji cha Masugulu wilayani Mbinga
No comments: