LIVE STREAM ADS

Header Ads

Wizara ya Madini yapaa ukusanyaji Maduhuli

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Julai, 2020 hadi Aprili, 28 mwaka huu Tume ya Madini imefanikiwa kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 484.435 ambayo ni sawa na asilimia 91.97 ya lengo la ukusanyaji wa maduhuli ya kiasi cha shilingi bilioni 526.722 kwa mwaka wa fedha 2020-2021.

Profesa Kikula ameyasema hayo tarehe 28 Aprili, 2021 jijini Dodoma kwenye kikao kazi kilichoshirikisha Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa chenye lengo la kujadili changamoto za utendaji kazi na kuweka mikakati ya ukusanyaji wa maduhuli kwa mwaka wa fedha 2021-2021 ambapo Tume ya Madini imepangiwa kukusanya lengo la shilingi bilioni 650.

Alisema kuwa siri ya kasi nzuri ya ukusanyaji wa maduhuli inatokana na msaada mkubwa kutoka Wizara ya Madini na ushirikiano kutoka kwa Maafisa Madini Wakazi wa Mikoa na kuendelea kuwataka maafisa madini wakazi wa mikoa kuendelea kuwa wabunifu kwenye ukusanyaji wa maduhuli.
Katika hatua nyingine alisema kuwa ili kuweza kufikia lengo la ukusanyaji kwa mwaka wa fedha 2021-2022 mbali na kuweka mikakati mbalimbali ya ukusanyaji wa maduhuli, amewataka watumishi wa Tume ya Madini kuendelea kufanya kazi kwa ushirikiano na kuunganisha nguvu huku wakiwa wazelendo.

“Mfahamu ya kuwa macho yetu yote yapo kwa maafisa madini wakazi wa mikoa hususan kwenye ukusanyaji wa maduhuli ili mchango wa sekta ya madini kwenye pato la taifa uweze kufikia asilimia 10 ifikapo mwaka 2025,” amesema Profesa Kikula

Kamishna wa Tume ya Madini, Janeth Lekashingo akizungumza katika kikao hicho mbali na kupongeza kazi nzuri inayofanywa kwenye sekta ya madini aliwahimiza watendaji wa Tume na maafisa madini wakazi wa mikoa kuendelea kuchapa kazi na kusisitiza kuwa kama kamisheni wapo tayari kupokea na kutatua changamoto mbalimbali zitakazojitokeza wakati wa utendaji kazi.
Naye Kamishna wa Tume, Profesa Abdulkarim Mruma licha ya kupongeza kazi nzuri inayofanywa na Watumishi wa Tume ya Madini, alisisitiza kufanya kazi kwa usawa pasipo kuwepo kwa makundi ya viongozi na watumishi.

Kwa upande wake Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Mhandisi Yahya Samamba akizungumza katika mahojiano maalum alipongeza kazi kubwa inayofanywa na Waziri wa Madini, Doto Biteko, Naibu Waziri wa Madini, Profesa Shukrani Manya, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila, Mwenyekiti wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula na Kamisheni yote kwa msaada kwenye utatuzi wa changamoto mbalimbali hali iliyopelekea Tume ya Madini kuendelea kufanya vizuri zaidi kwenye ukusanyaji wa maduhuli.
“Mara kwa mara tumekuwa tukikutana na viongozi wa Wizara ambao wamekuwa wakitupa maelekezo na kutatua changamoto mbalimbali kwenye usimamizi wa Sekta ya Madini, tunaahidi kuendelea kuchapa kazi kwa ubunifu ili kuhakikisha kupitia Sekta ya Madini, wananchi wananufaika na rasilimali za madini zilizopo,” alisema Mhandisi Samamba.
Na Greyson Mwase, Dodoma

No comments:

Powered by Blogger.