LIVE STREAM ADS

Header Ads

Kongamano la Fursa Arusha kupambwa na burudani ya kukata na mundu

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Online Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO) Stella Joel.
Mlezi wa TAMUFO, Dkt. Frank Richard.
Edson Mwasabwite, Muimbaji wa nyimbo za injili mmoja wa wanamuziki atakayetoa burudani.
Mgeni rasmi mtarajiwa kwenye kongamano hilo, msomi na mdau wa maendeleo hapa nchini Dkt. Jonathan Lema.
Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Lake Manyara Dkt.Noelia Myonga.

Na Dotto Mwaibale, Arusha
Wananchi wa Jiji la Arusha na viunga vyake wanatarajia kuanza kupata burudani ya muziki wa aina mbalimbali utakaokuwa ukitolewa katika Kongamano kubwa la Fursa litakaloanza kufanyika mwishoni mwa mwezi huu.

Hayo yamebainishwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanamuziki Tanzania (TAMUFO) Stella Joel wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa jana.

"Maandalizi ya kongamano hilo yanaendelea vizuri kwani litawahusisha wanamuziki binafsi na vikundi mbalimbali vya kwaya" alisema Joel.

Alisema kongamano hilo lililoandaliwa na TAMUFO linarajia kuanza Novemba 25, ambapo litafanyika hadi Novemba 28, 2021 kuanzia saa 3 asubuhi hadi saa 11 jioni.

Mlezi wa TAMUFO, Dkt. Frank Richard alisema katika kongamano hilo kutakuwa na fursa mbalimbali zikiwemo za wanamuziki kupata bima ya afya ya NHIF kwa gharama nafuu, kupata vipimo vya matibabu katika Hospitali za Serikali na watu binafsi.

Alitaja fursa zingine kuwa ni elimu ya mauzo mtandaoni itakayotolewa na maofisa kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na kuwa fursa nyingine lukuki zitakuwepo.

Mgeni rasmi katika kongamano hilo atakuwa ni Kijana Msomi na Mdau wa maendeleo hapa nchini Dkt. Jonathan Lema.

Wadau wengine walioalikwa kwenye kongamano hilo ni Mkurugenzi wa Makumbusho ya Taifa ya Elimu Viumbe Arusha Dkt.Christina Ngereza pamoja na Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Lake Manyara Dkt.Noelia Myonga.

Dkt.Richard alisema kongamano hilo litafanyika Makumbusho ya Taifa ya Elimu Viumbe karibu na Viavia jijini Arusha.

Katibu Mkuu wa TAMUFO Stella Joel alitumia nafasi hiyokuwakaribisha wananchi wote wa jiji la Arusha kufika kwenye kongamano hilo na kuwa chakula kitapatikana kwa gharama nafuu na hakutakuwa na kiingilio.

No comments:

Powered by Blogger.