LIVE STREAM ADS

Header Ads

Tanzania yakaribisha ushirikiano na Congo katika sekta ya madini

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Online Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Waziri wa Madini Tanzania, Dkt. Doto Biteko.
***

Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko amesema Wizara anayoiongoza iko tayari kutoa wataalamu wake ili wakakutane na wataalamu wa Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Congo (DRC) kwa lengo la kujadili namna bora ya kushirikiana katika biashara na mnyororo mzima wa biashara ya madini.

Dkt. Biteko aliyasema hayo kwenye kikao chake na Gavana wa Katanga kutoka DRC Jacques Katwe pamoja na ujumbe wake jijini Dodoma.

Aidha Dkt. Biteko alisema kutokana na utajiri wa madini uliopo nchini Tanzania, Mchango wa Sekta ya Madini kwenye Pato la Taifa umeendelea kuimarika kutoka asilimia 4.7 mwaka 2019 hadi kufikia asilimia 7.9 Septemba mwaka 2021.

Dkt. Biteko alisema Sekta ya Madini kwa miaka mitatu mfurulizo imekuwa ikiongoza katika kuliingizia Taifa fedha za kigeni.

“Tumeondoa urasimu kwenye biashara ya madini, mfanyabiashara akiomba kibali cha kusafirisha madini atapewa kibali kwa wakati, hivyo nitumie fursa hii kukuomba Mhe. Gavana kuwaleta wawekezaji kuja kuwekeza kwenye Sekta ya Madini” alisema Dkt. Biteko.

Aidha, Dkt. Biteko alisema ujenzi wa kiwanda cha kusafisha madini ya dhahabu cha Mwanza Precious Metal Refinery kitawasaidia wafanyabishara wa madini wa DRC kusafisha madini yao ambapo ametumia fursa hiyo kuwakaribisha wafanyabiashara wa madini wa DRC kuja Tanzania kusafisha madini yao.

Pamoja na mambo mengine, Dkt. Biteko alisema Tanzania inautajiri mkubwa wa madini ambapo wizara inajitahidi kusimamia Sheria, Kanuni na Taratibu ili madini hayo yaweze kuwanufaisha wananchi kwa kubadilisha maisha yao kiuchumi na kuwapatia ajira.
Kwa upande wake, Gavana wa Jimbo la Katanga nchini Congo, Jacques Katwe alimpongeza Waziri wa Madini kwa usimamizi madhubuti anaoufanya katika kuiongoza wizara hiyo ambayo imepata mafanikio makubwa.

“Lengo la ziara hii ni kujifunza jinsi gani Tanzania imefanikiwa kwenye Sekta ya Kilimo hivyo tukaona bora tufike na Wizara ya Madini ili tujifunze baada ya kutambua utajiri wa madini tulionao DRC na utajiri wa madini yaliyopo Tanzania” Katwe alisema.

Sambamba na hayo, Katwe amefurahishwa na ujenzi wa kiwanda cha kusafisha madini ya dhahabu cha Mwanza Precious Metal Refinery ambapo amesema atahakikisha anawasisitiza wafanyabiashara wa madini kuleta madini yao Tanzania kwa ajili ya kusafishwa.

Naye Kamishna wa Madini, Dkt. Abdulrahaman Mwanga alieza fursa ya kumueleza Gavana Katwe na ujumbe wake aina za madini zilizopo nchini Tanzania na kuwaeleza jinsi gani shughuli za uchimbaji, uchenjuaji, na uongezaji thamani madini zinavyofanyika ikiwemo ujenzi wa kiwanda cha kusafisha madini ya dhahabu cha Mwanza Precious Metal Refinery.
Picha ya pamoja.

No comments:

Powered by Blogger.