Watu wenye ulemavu waomba kukumbukwa kwenye ajira
Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Online Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Makamu Mwenyekiti Chama cha watu wenye Ulemavu Tanzania (CHAWATA) Mkoa wa Iringa Leo Sambala.
Na Fredy Mgunda, Iringa.
***
Na Fredy, Mgunda, Iringa
Chama cha watu wenye ulemavu (CHAWATA) Mkoa wa Iringa kimeiomba Serikali kutoa nafasi sawa za ajira kwa watu wenye ulemavu kwani nao wana uwezo wa kufanya kazi kama watu wengine na kuondokana na changamoto ya ukosefu wa ajira.
Mwenyekiti wa chama hicho, Iringa Rukia Makweta amesema moja ya malengo ya elimu jumuishi ni kuanda Taifa la watu wenye mahitaji maalaumu na walemavu kujiajiri au kuajiriwa na kuondokana na utegemezi.
Makweta amesema kuwa muda mrefu nchini Tanzania kumekuwa na dhana kuwa mlemavu ni mtu anayepaswa kuwa tegemezi katika jamii jambo ambalo si kweli.
Amesema baadhi ya watu huenda mbali zaidi na kuwaficha watu wenye ulemavu ili wasionekane na jamii kiasi cha kuwakosesha fursa za kijamii na kiuchumi ikiwemo elimu na mitaji,ajira.
Makweta amesema kuwa licha ya kuwa nyuma katika fursa mbalimbali kutokana na mitazamo hasi ya jamii dhidi yao, idadi ya watu wenye ulemavu wanaojitosa katika shughuli za kiuchumi Tanzania imezidi kuongezeka kwa kasi ndani ya miaka saba iliyopita.
Kwa upande wake Katibu wa shirikisho la watu wenye ulemavu (SHIVYAWATA) Mkoa wa
Iringa, Leo Sambala amesema kuwa ripoti ya utafiti wa watu wenye uwezo wa kufanya kazi ya mwaka 2020/21 iliyotolewa na Ofisi ya Taifa ya takwimu (NBS), inabainisha kuwa idadi ya watu wenye ulemavu wenye ajira imeongezeka hadi takriban theluthi mbili au asilimia 63.2 mwaka 2020/21 kutoka asilimia 59.1 mwaka 2014.
Sambala amesema kuwa inamaanisha hadi mwaka jana takriban watu sita kati ya 10 wenye ulemavu walikuwa na ajira ama kwa kujiajiri au kuajiariwa.
Katika kipindi hicho, kiwango cha watu wenye ulemavu wenye umri miaka 15 na zaidi ambao hawakuwa na ajira nacho kilishuka. Takwimu hizo zinaeleza zaidi kiwango cha watu wenye ulemavu mwaka 2020/21 kilikuwa asilimia 6,nusu ya kile kilichokuwepo mwaka 2014 ambacho kilikuwa asilimia 12.4.
Kwa nyakati tofauti Serikali imekua inawahamasisha walemavu kuchangamkia fursa za ajira zinazotangazwa na serikali kwa sababu ni wachache wanaojitokeza ikiashiria Mwamko mdogo wa walemavu katika uombaji wa ajira.serikali inasisitiza kwamba endapo mtu mwenye ulemavu au mahitaji maalumu atakua ametimiza vigezo bila kuogopa changamoto zinazowakabili kuomba ajira hizo kwani mchakato wote wa maombi ya ajira unafanywa kwa kufuata kanuni na Sheria za Nchi ambayo inampa kila mtu haki ya kupata ajira,
Alisema Sheria ya ajira namba tisa ya mwaka 2010 inasema “Mwajiri yoyote awe wa Umma au Binafsi mwenye waajiriwa kuanzia 20 na kuendelea lazima asilimia 3 ya waajiriwa hao iwe kwa ajili ya watu wenye ulemavu” hii inaonyesha kuwa walemavu wana haki ya kuajiriwa mahali popote.
Lakini Sambala amesema ni vyema walemavu kuzitaja changamoto zao kweye fomu za maombi ili serikali iweze kuwaandalia mazingira rafiki kwa ajili ya mchakato mzima wa upatikanaji wa ajira na baada ya kupata ajira waweze kupangiwa sehemu ambazo hazitakua changamoto kwao.
Aidha Serikali inawapa kipaumbele walemavu kuanzia wakati mchakato wa usajili hadi wakati wa kupanga ajira hivyo basi walemavu wenye vigezo vilivyoanishwa kwenye matangazo ya ajira wajitokeze kutuma maombi ya nafasi hizo.
Walemavu wanahaki kisheria hivyo waachane na mawazo ya kudhani wakitaja changamoto zao kwenye maombi hawatapatiwa nafasi.
Sambala alisema kuwa Serikali inatambua nafasi ya walemavu katika kuchangia maendeleo ya nchi na ina wahamasisha kutumia fursa mbalimbali zinazojitokeza ili kujikwamua kiuchumi.
Katika kutambua umuhimu wa vyombo vya habari, taasisi ya Iringa Development of Youth Disabled and Children Care (IDYDC), shirika lisilo la kiserikali linalotekeleza mradi wa Inclusive Media Project unaofadhiliwa na Internew Tanzania katika Mkoa wa Iringa kupitia Mratibu wa mradi Reuben Magayane alisema kuwa vyombo vya habari vinapaswa kuwasemea watu wenye ulemavu ili waweze kupata ajira kama watu wengine.
Magayane alisema kuwa waandishi wa habari na vyombo vya habari vinaweza kuwasaidia watu wenye ulemavu kwa kufikisha ujumbe moja kwa moja kwa serikali husika.
No comments: