LIVE STREAM ADS

Header Ads

Dhahabu iliyosafishwa katika kiwanda cha Geita yasafirishwa nje ya nchi

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Online Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Serikali imewataka wachimbaji wote wa madini na wafanyabiashara nchini kusafisha dhahabu katika viwanda vya ndani badala ya kuuza malighafi kwenye viwanda vya nje.

Rai, hiyo imetolewa Julai 7, 2022 mkoani Geita na Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko wakati akishuhudia shughuli ya usafishaji wa dhahabu katika kiwanda Geita Gold Refinery (GGR).

Amesema, kwa sasa atakaekwenda kuuza dhahabu ghafi katika viwanda vya kusafisha dhahabu atalipa mrabaha asilimia 4 badala ya asilimia 6 ili wachimbaji wapate nafasi ya kusafisha katika viwanda hivyo.

"Ni muhimu sasa dhahabu tunayoichimba wenyewe iweze kusafishwa hapa iende ikiwa bidhaa ya mwisho" amesisitiza.
Aidha Dkt. Biteko amesema, kiwanda cha GGR kitatengeneza ajira kwa Watanzania pamoja na kulipa kodi mbalimbali Serikalini.

Katika hatua nyingine, Dkt.Biteko ameupongeza mkoa wa Geita kwa usimamizi wa sekta ya Madini. Amesema, mkoa unasimamia vizuri fedha zinazotolewa katika huduma za kijamii ambayo imesaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya mkoa kupitia Sekta ya Madini.

Mkurugenzi Mtendaji wa GGR Sarah Masasi amesema kiwanda hicho kina uwezo wa kusafisha dhahabu kilo 600 kwa siku. Amesema kiwanda kina wafanyakazi wenye uwezo wa hali ya juu ili kufanya kazi katika ubora wa kimataifa.

Naye Kaimu Mkuu wa Mkoa Geita, Said Nkumba amesema, kiwanda hicho kinakwenda kutangaza mkoa katika Sekta ya Madini. Amesema, wafanyabiashara wa madini na wachimbaji wadogo watumie nafasi hiyo kupeleka madini yao kusafishwa katika kiwanda cha GGR ili manufaa yaweze kubaki katika mkoa wa Geita na nchini kwa ujumla.

Kwa upande mwingine, Mbunge wa Jimbo la Geita, Constantine Kanyasu amempongeza Mama Masasi kwa kujenga kiwanda hicho katika mkoa huo.

Amesema, kiwanda hicho ni mkombozi wa wachimbaji na wafanyabiashara wa madini nchini ili waweze kusafisha dhahabu katika ubora wa kimataifa.
Kiwanda cha Geita kinamilikiwa na mwanamke mtanzania Sarah Masasi ambaye ni mwanamke wa kwanza Tanzania kujenga kiwanda cha kusafisha dhahabu nchini.
Na Steven Nyamiti, WM

No comments:

Powered by Blogger.