LIVE STREAM ADS

Header Ads

Waziri Biteko awataka wachimbaji madini kuzingatia Sheria

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko amewasisitiza wachimbaji wa madini nchini kuzingatia Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo inayosimamia Sekta ya Madini ili wachimbe rasilimali hiyo kwa manufaa ya wachimbaji na jamii kwa ujumla.

Dkt. Biteko amesema hayo Januari 03, 2022 katika ziara yake Wilayani Nyang'hwale mkoa wa Geita alipotembelea na kuzungumza na wachimbaji wadogo katika mgodi wa dhahabu wa Isonda.

Amewataka wachimbaji kuheshimu maeneo yenye leseni ili kuepusha migogoro inayojitokeza mara kwa mara kwa wawekezaji wa madini katika maeneo yenye shughuli za uchimbaji.

"Mwenye leseni ana wajibu wa kulinda leseni yake na sisi tuna wajibu wa kutovamia leseni ya mtu mwingine," amesema Dkt. Biteko.

Vilevile, amewataka wachimbaji katika mgodi wa Isonda wanaochimba katika leseni hiyo ya utafiti kutomsumbua mwekezaji huyo kutoka kampuni ya Henan Yukuang International Mining Investment Ltd ili wasitolewe katika eneo hilo.

Aidha, amemwagiza Mkuu wa Wilaya hiyo na Afisa Madini kusimamia shughuli hizo ili wachimbaji wachimbe kwa amani na kampuni ya Henan ifanye utafiti.

Akieleza namna Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anavyowapenda wachimbaji, amesema kuwa Rais amemwelekeza kuwalea wachimbaji wadogo ili wachimbaji hao wafanikiwe.
Amesema, Serikali itaendelea kutoa maeneo mengine kwa wachimbaji nchini ili kuendelea kuchimba rasilimali hiyo iliyopo nchini na kubadilisha maisha yao.

Aidha, ameutaka uongozi wa mgodi huo kukutana na Serikali ya kijiji ili mgodi huo uandae mpango wa kuchangia huduma za jamii ili wananchi wanaozunguka eneo la mgodi huo wanufaike.

Akizungumza suala la ukwale, Waziri Biteko ameagiza wanawake wanaojihusisha na ukwale kuacha kusumbuliwa ili wafanye shughuli zao vizuri na kuhahakikisha wale wote wanaojihusisha na wizi wanaacha mara moja.

Ukwale ni mawe ya madini yanayosadikika kuwa na kiasi kidogo sana cha madini ya dhahabu.

Aidha, amemuagiza Afisa Madini Mkazi wa Mbogwe kusimamia suala hilo ili shughuli ya ukwale ifanyike bila usumbufu.

Naye, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Nyang'hwale, Fabian Sospeter amesema kuwa, shughuli za uchimbaji madini zinazofanyika katika wilaya hiyo zimesaidia kuongeza mapato ya Halmashauri ambapo hadi sasa kiasi cha Shilingi bilioni 1.5 kati ya malengo ya bilioni 1.9 zimekusanywa na kati ya hizo, Shilingi bilioni 1 imetokana na shughuli za madini.

Ziara hiyo ya kutembelea mgodi wa Isonda na eneo lenye mgogoro wa mpaka kijiji cha Kharumwa na Izunya imehudhuriwa na Wataalamu kutoka Wizara ya Madini, Tume ya Madini, Afisa Madini Mkazi Mbogwe na wataalam wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang'hwale.

No comments:

Powered by Blogger.