LIVE STREAM ADS

Header Ads

Benki ya CRDB kuendelea kutoa huduma bora kwa wateja wake

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo (kulia) akipokea fomu ya uwekezaji katika hatifungani ya kijani ya "Kijani Bond" kutoka kwa kaimu Afisa Mtendaji Mkuu na Afisa Mkuu wa Bishara Benki ya CRDB, Boma Raballa wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Huduma kwa Wateja 2023 iliyofanyika katika tawi la benki hiyo la Azikiwe lililopo jijini Dar es Salaam.
Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo (wapili kulia) akipokea kadi yake ya 'TemboCard' kutoka kwa kaimu Afisa Mtendaji Mkuu na Afisa Mkuu wa Bishara Benki ya CRDB, Boma Raballa wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Huduma kwa Wateja 2023 iliyofanyika katika tawi la benki hiyo la Azikiwe lililopo jijini Dar es Salaam. Wengine pichani ni Afisa Mkuu wa Uendeshaji Benki ya CRDB, Bruce Mwile (wakwanza kulia), na Mkuu wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja Benki ya CRDB, Yolanda Uriyo (wapili kushoto).
Benki ya CRDB imewaahidi wateja wake kuendelea kutoa huduma na bidhaa bunifu zitakazowawezesha kufikia malengo yao ya kifedha.

Ahadi hiyo imetolewa na Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu na Afisa Mkuu wa Biashara wa benki hiyo, Boma Raballa wakati wa uzinduzi wa Wiki ya Huduma kwa Wateja 2023 uliofanyika katika tawi la benki hiyo la Azikiwe.

Akitoa ahadi hiyo, Raballa amesema Benki ya CRDB ikiwa kinara katika soko inaamini katika utoaji wa huduma bora kwa wateja wake na Watanzania kama njia ya kusaidia wateja kufikia malengo yao.
“Tunapoadhimisha wiki hii tumejipanga kuendelea kutoa huduma bora na kuziboresha kadri ya matakwa ya wateja wetu ili tuendelee kuwaridhisha na kufanya huduma zetu kuwa na viwango zaidi” amesema Raballa.

Raballa amesema Benki hiyo sasa hivi imetilia mkazo katika uwekezaji wa mifumo ya kidijitali ili kurahisisha upatikanaji kwa wateja. Benki hiyo pia imeendelea kutanua wigo wa huduma kupitia matawi zaidi ya 260, na “CRDB Wakala” ambao wamefikia zaidi ya 28,000 kote nchini.
“Malengo yetu ni kuona tunawafikia wateja kwa urahisi na kutoa huduma zinazoendana na mahitaji halisi ya wateja. Tunaendelea kuwekeza katika ubunifu wa huduma na bidhaa, na hivi karibuni tumezindua hatifungani ya kwanza ya kijani “Kijani Bond” nchini inayotoa fursa ya uwezeshaji wa miradi inayozingatia utunzaji wa mazingira” amesema.

Aidha, Raballa amegusia kuwa Benki hiyo pia imewekeza vyakutosha katika mafunzo kwa wafanyakazi ili kuwajengea weledi na kuwawezesha kutoa huduma bora kwa wateja.
Akizindua Wiki hiyo ya Huduma kwa Wateja, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo ameipongeza Benki ya CRDB kwa kuwa mstari wa mbele kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii kupitia huduma na bidhaa bora zinazotolewa na benki hiyo.

Mpogolo ameiomba Benki ya CRDB kuendelea kuwekeza katika huduma za kidijitali ili kuendana na mahitaji ya wateja ambayo yamekuwa yakibadilika kila uchwao. Amewataka wananchi pia kuchangamkia fursa zinazotolewa na Benki ya CRDB ikiwamo mikopo ili kuboresha maisha yao.
Mkuu wa Wilaya huyo alitumia fursa hiyo kuwekeza katika hatifungani ya kijani ya Benki ya CRDB “Kijani Bond” ambayo imebaki siku tano tu dirisha la uwekezaji kufungua. Mpogolo amewahimiza wananchi kuchangamkia fursa hiyo na kunufaika na riba shindani ya asilimia 10.25 kwa mwaka.

Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja, Yolanda Uriyo amesema Wiki ya Huduma kwa Wateja ni fursa kwa Benki hiyo kuwashukuru wateja wake kwa kuichagua Benki ya CRDB na hivyo kuifanya kuendelea kuwa Benki bora, huku akiwakaribisha kupata huduma katika matawi ya Benki ili kupata huduma bora, na kutoa maoni au ushauri.
Aidha, Yolanda amesema katika Wiki hii ya Huduma kwa Wateja Benki ya CRDB pia imejipanga kutembelea wateja wake katika maeneo yao kuwashukuru, kusikililiza mahitaji yao na kutoa elimu juu ya huduma na bidhaa mbalimbali zinazotolewa na Benki ya CRDB.

No comments:

Powered by Blogger.