LIVE STREAM ADS

Header Ads

NSSF yatumia zaidi ya Bilioni 50 kulipa mafao kwa miezi sita

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), umelipa shilingi bilioni 56.689 kama mafao ya wastaafu katika kipindi cha miezi sita iliyoanzia mwezi Julai mpaka Disemba 2023.

Mkurugenzi wa Uendeshaji wa NSSF, Omari Mziya alisema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Makao Makuu ya NSSF yaliyopo jengo la Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.

Aidha alisema Mfuko umeandaa mpango mahususi kwa ajili ya kusikiliza na kutatua kero mbalimbali za wanachama na tayari mpango huo unaendelea kutekelezwa kwenye ofisi mbalimbali za NSSF kwa lengo la kuzipatia ufumbuzi changamoto hizo.

Mziya alisema NSSF inawathamini wanachama wake, hivyo inawaomba waajiri wote wa sekta binafsi kutimiza wajibu wao kwa kuwasilisha michango ya wafanyakazi wao kila mwezi ili kuwaondolea usumbufu watakapostaafu waweze kulipwa mafao yao kwa wakati.

Alisema Mfuko unaendelea kulipa pensheni kwa wastaafu, ambapo katika kipindi cha mwezi Januari 2024, imelipa shilingi bilioni 9.93.

“NSSF tunajivunia kuwa na wastaafu ambao tunawalipa kwa wakati kila inapofika tarehe 25 ya kila mwezi, dhamira na lengo letu ni kuona wafanyakazi wote katika sekta binafsi na sekta isiyo rasmi wanaingia katika malipo ya pensheni ili kupunguza umasikini utokanao na uzee au kukosa kipato” alisema Mziya.

Alisema Mfuko upo katika zoezi la uhakiki wastaafu ambalo lilianza tarehe 1 Februari na litaendelea mpaka tarehe 30 Aprili, 2024, ambapo alitoa wito kwa wastaafu na wategemezi kutumia kipindi hiki kufanya uhakiki kwenye ofisi zote za NSSF zilizopo Tanzania Bara na waliopo Zanzibar wafike katika ofisi za ZSSF.

Mziya alisema uandikishwaji wanachama umerahisishwa ambapo Mfuko hutumia mifumo ya TEHAMA kuandikisha wanachama na kupitia mifumo hiyo mwajiri anaweza kumuandikisha mwanachama kupitia mfumo wa Employer Portal.

“Natoa rai kwa waajiri ambao hawajaingia kwenye mfumo huu wa Employer Portal wajiunge kwa sababu ni mfumo wenye faida nyingi sana ikiwemo ya kurahisisha uandikishaji wanachama” alisisitiza.

Mziya alisema ukusanyaji wa michango ni jukumu muhimu la NSSF na kazi hiyo inaifanywa kwa ushirikiano kutoka kwa waajiri kwa sababu michango ni makato ya mshahara ya watumishi ambayo yanasimamiwa na waajiri wenyewe.

Alitoa wito kwa waajiri wote wa sekta binafsi kuhakikisha wanawaandikisha wafanyakazi wao katika Mfuko na kuwasilisha michango yao kila mwezi.

Naye Mzee Nicholas Kingazi, mkazi wa Tabata alisema anafurahishwa na huduma zinazotolewa na NSSF hasa kwa wazee wastaafu ambapo wasiojiweza wamekuwa wakifuatwa majumbani kwa ajili ya kuhakikiwa taarifa zao.

“Nimefarijika sana kwa sababu kitendo mlichokifanya NSSF cha kufuata wazee wasiojiweza kuwahakiki majumbani kwao” alisema mzee Kingazi.

Alitoa shukran zake kwa uongozi wa NSSF na wafanyakazi kwa ujumla kutokana na kujali wanachama wao wakiwemo wazee wastaafu, huku akishukuru kwa namna ambavyo Mfuko umekuwa ukiwalipa wastaafu wake kila ifikapo tarehe 25 ya kila mwezi.

No comments:

Powered by Blogger.