LIVE STREAM ADS

Header Ads

Biteko atembelea banda la Barrick kwenye maonesho ya OSHA

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dk. Doto Biteko, ameipongeza Kampuni ya Barrick chini kupitia migodi yake ya Bulyanhulu, North Mara na Buzwagi kwa kuzingatia kanuni za Afya na usalama kwa ufasaha kupitia sera yake ya ‘Journey to zero’.

Biteko alitoa pongezi hizo baada ya kutembelea banda la Barrick Tanzania katika maonesho ya afya na usalama mahali pa kazi yanayoendelea jijini Arusha.

Waziri Biteko ambaye pia alikuwa mgeni rasmi katika kilele cha maonesho hayo, alitoa wito kwa Mamlaka za Serikali zinazosimamia Masuala ya Afya na Usalama kufanya kazi kwa weredi na kutoa ushirikiano mzuri kwa wadau kuelimisha jamii masuala ya usalama badala ya kutumia vitisho.

Akitoa maelezo ya utekelezaji wa Afya na Usalama kwa Dkt. Biteko,alipotembelea banda la maonesho la Barrick, Afisa Usalama na Afya wa Barrick, Michael Benard, alisema migodi ya Barrick kupitia kampeni yake ya ‘Journey to zero’ imefanikiwa kutokomeza matukio ya ajali katika migodi yake.

“Wafanyakazi wetu na wadau wetu wote wanaotembelea migodi yetu wakati wote tunahakikisha wanazingatia kanuni zetu za Afya na Usalama wakati wote na tumefanikiwa kukomesha matukio ya ajali katika maeneo yetu ya kazi” alisema Benard.

Barrick imekuwa ikitekeleza kampeni ya ‘Journey to zero’ ambayo inalenga kuhamasisha afya na usalama kwa wafanyakazi wake ambayo sasa imeanza kupelekwa kwa wadau na jamii nje ya migodi.

“Kampeni yetu ya 'Journey to Zero' inalenga kuhakikisha wafanyakazi wote wa kampuni wanakuwa salama wakati wote wanapokuwa kazini hadi wanaporudi nyumbani hivyo tumehakikisha kampeni hii inavuka mipaka hadi nje ya kampuni kuhakikisha jamii nzima inakuwa salama na ndio maana tunaendelea kuendesha mafunzo ya usalama kwa jamii ili kuhakikisha jamii yote inakuwa salama na tumetumia maonesho haya kuwapatia wananchi elimu ya afya na usalama” alisema Benard.

Wakati huo huo wageni mbalimbali wamekuwa wakiendelea kutembelea banda la maonesho la Barrick kupata elimu ya Afya na Usalama ambapo pia kamati ya majaji ya OSHA imetembelea banda hilo na kupata maelezo kutoka kwa timu ya Maofisa Usalama kutoka migodi ya Barrick ya North Mara, Bulyanhulu na Buzwagi.
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko akisikiliza maelezo kutoka kwa Afisa Afya na Usalama wa Barrick, Michael Benard wakati alipotembelea banda la kampuni hiyo kwenye maonesho ya OSHA yanayoendelea jijini Arusha. Dkt. Biteko aliongozana na ujumbe wa viongozi mbalimbali wa Serikali.
Wajumbe wa kamati ya majaji ya OSHA walipotembelea banda la Barrick kwenye maonesho hayo.

No comments:

Powered by Blogger.