LIVE STREAM ADS

Header Ads

BARRICK YATOA UFADHILI KWA WANAFUNZI WATANO KUSOMA UTAALAMU WA FANI YA MADINI NJE YA NCHI

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) waliopata ufadhili wa kwenda kusoma nchini Afrika ya Kusini
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) , Profesa William Anangisye akizungumza na kutoa nasaha zake katika hafla ya kuwaaga wanafunzi wa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) waliopata ufadhili wa kwenda kusoma shahada ya kwanza ya Jiolojia na Madini
Meneja wa Barrick nchini , Dkt. Melkiory Ngido akizungumza na waandishi wa habari , wanafunzi waliopata udhamini kwa kwenda kusoma nchini , Afrika Kusini na wageni kwenye hafla ya kuwaaga wanafunzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam
Meneja Rasilimali watu wa Barrick nchini , Lumbu Kambula akizungumza kwenye hafla ya ufadhili wa wanafunzi watano wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) iliyofanyika jijini Dar es Salaam
Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) waliopata ufadhili wa kwenda kusoma nchini Afrika ya Kusini wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Barrick na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM)

**
-Kuendelea kuwekeza katika kizazi kijacho cha wataalamu wa sekta ya madini

Kampuni ya Barrick nchini inayoendesha shughuli zake kwa ubia na Serikali ya Tanzania kupitia Twiga Minerals imetoa ufadhili kwa wanafunzi watano kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kwenda kusoma Shahada ya kwanza ya Elimu ya Madini na Jiolojia katika Chuo Kikuu cha Johannesburg Afrika ya Kusini kupitia progamu yake ya kuwezesha wasomi vijana inayotekelezwa kanda ya Afrika na Mashariki ya kati.

Akizungumza kwenye hafla ya kutangaza ufadhili huo na kuwaaga wanafunzi waliofanikiwa kupata fursa hiyo jijini Dar es Salaam , Meneja wa Barrick nchini, Dkt. Melkiory Ngido amesema ufadhili huu ni ushuhuda na uthibitisho kwamba Barrick imelenga kukuza sekta ya madini kupitia uwekezaji wake sambamba na kuhakikisha sekta ya madini inatoa mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi.

“Uwajibikaji wetu hauishii kuendesha migodi yetu kwa viwango vya kimataifa bali pia tumejikita kuhakikisha tunawekeza katika kuwapatia watanzania ujuzi hususani kwa vijana ambao watakuwa wataalamu wa siku za usoni,ndio maana kupitia udhamini wa elimu kama huu kunawezesha kuwa na wataalamu wa fani ya madini na wabunifu watakaochangia kuleta maendeleo katika siku za usoni”, amesema Dkt.Ngido.

Amesema Barrick itakuwa karibu na Wanafunzi hao na pindi wakapomaliza masomo yao watapatiwa fursa ya kuwajengea uwezo wa kupata ujuzi zaidi kwa kuwapatia ajira katika migodi yake nchini.

Ameongeza kwamba dhamira ya kampuni ya Barrick ni kuendelea na ushirikiano wenye tija kwa kufanya uwekezaji endelevu wenye tija kwa Tanzania na watu wake kwa kuhakikisha kwamba katika programu hii taifa linaweza kupata wataalamu mbalimbali kwenye fani ya Uinjinia wa madini na Jiolojia hapa nchini.

Pamoja na mambo mengine amefafanua kuwa kupitia programu hiyo kampuni ya Barrick kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wataendelea na kuhakikisha wanazalisha wataalamu wapya kwenye sekta ya madini hapa nchini.

Kwa upande wake , Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Profesa William Anangisye ameshukuru kwa kampuni ya Barrick kuwapa ufadhili wanafunzi watano kutoka kwenye Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) baada ya kushindanishwa na wenzao kutoka Vyuo vikuu vingine hapa nchini.

“Tumefurahi na ufadhili huu na ni Imani yangu watakwenda kusoma kwa bidhii na hakuna atayerudishwa kwa kushindwa masomo nawataka muwe mabalozi wazuri kwa Chuo chetu na nchini kwa ujumla,” amesema Profesa Anangisye.

Amesema ufadhili wa wanafunzi hawa umekuwa baada ya mchujo wa wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali hapa nchini na hatimaye hawa wameshinda , hawa ni kati ya wanafunzi bora waliopita kwenye mchujo na kupata ufadhili kwa kwenda kusoma shahada ya kwanza kwenye madini,” .

“Ni furaha yangu kuona kwamba kati ya wanafunzi hawa waliopata ufadhili kuna wasichana hii ni moja ya sera ya pale mlimani kuweka uwiano wa jinsia kwenye masomo ili kuhakikisha watoto wa kike na wenye uwezo wanapata fursa za kusonga mbele,” amesisitiza.

Mmoja ya wanafunzi akiongea kwa niaba ya wenzake, Samson Abeid amesema programu hiyo ni fursa ya kipekee kwa wanafunzi wa kitanzania kwa kusoma kwa bidii na kuhakikisha kwamba wanatoa mchango katika maendeleo ya taifa.

“Programu hii itachochea chachu katika sekta ya elimu hapa nchini na kutoa fursa kwa wanafunzi wa kitanzania kupata elimu , maarifa na ujuzi nje ya nchini,” amesema Abeid.
Mmoja wa wanufaika akipokea nyaraka za ufadhili, katika hafla hiyo

No comments:

Powered by Blogger.