LIVE STREAM ADS

Header Ads

SAMAKI ZIWA VICTORIA HATARINI KUTOWEKA, WAZIRI WA MAENDELEO YA MIFUGO NA UVUVI AMUNG'UNYA MANENO KWA WAMILIKI WA VIWANDA VYA SAMAKI MKOANI MWANZA.



Dk.Titus Kamani
Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi Dk.Tutus Kamani amebainisha kwamba Mazao ya Samaki ndani ya Ziwa Victoria yameanza kupungua, kutokana na Uvuvi haramu na hivyo kuhatarisha Uchumi wa Taifa sanjari na kupunguza upatikanaji wa ajira kwa Wananchi.

Dk.Kamani ambae pia ni Mbunge wa Jimbo la Busega Mkoani Simiyu aliyasema hayo jana Mkoani Mwanza, wakati akizungumza katika kikao na wamiliki wa Viwanda vya Samaki Mkoani Mwanza, kikao ambacho kililenga katika kujadili na kupeana taarifa ya nini kifanyike ili kuboresha Sekta ya Uvuvi hapa nchini.

Katika kikao hicho Dk.Kamani alieleza kwamba katika Ziwa Victoria zipo changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya uvuvi ikiwemo kupungua kwa mapato kutokana na Mazao ya Samaki kupungua ziwani, jambo ambalo linatokana na ongezeko la wavuvi wanaovua bila kuwa na mpangilio mzuri wa Uvuvi endelevu sanjari na Uwepo wa Uvuvi haramu katika Ziwa hilo.

“Uvuvi ya zana haramu kwa maana ya uvuvi haramu unaathiri kiwango cha Samaki na mimi mwenyewe nimeshuhudia, tulienda na watu wa TAFIRI (Tanzania Fisheries Research Institute) tukaingia ziwani wakatumia utalaamu wao kwa muda wa nusu saa hatukupata hata samaki mmoja mwenye sifa ya kwenda kiwandani na hiyo ilikuwa ni ishara kwamba kuna tatizo”.Alisema Dk.Kamani huku akiongeza kuwa japo hiyo haitoshi kisayansi kutoa hitimisho kwamba hakuna samaki ziwa Victoria.
Dk.Kamani akizungumza na wanahabari
Huku akishindwa kutaja majina, Dk.Kamani alibainisha kwamba Suala la Uvuvi haramu linajumuisha watu wengi ambao ni pamoja na wananchi wenyewe, watendaji wa Serikali sanjari na baadhi ya Wamiliki wa Viwanda vya kuchakata Mazao ya Samaki, hali ambayo ameonya kuwa inaweza kuhatarisha uchumi wa Taifa pamoja na Upatikanaji wa ajira ambapo amebainisha kuwa muda si mrefu kila mmoja ataathirika kutokana na suala la uvuvi haramu na hivyo kuomba ushirikiano ili kutokomeza hali hiyo.


Katika hatua nyingine Dk.Kamani aliwasihi wamiliki wa viwanda kutojiingiza katika suala la kununua samaki wachanga kwa kuwa kuna baadhi ya taarifa kwamba baadhi ya viwanda vinajihusisha na ununuzi wa samaki wachanga (wanaovuliwa kwa njia haramu) jambo ambalo linahatarisha upatikanaji wa samaki katika Ziwa Victoria.

Ili kuboresha Sekta ya Uvuvi hapa nchini, Dk.Kamani alibainisha kwamba Serikali imeandaa Mkakati katika bajeti ijayo kwa ajili ya kupata fedha ambazo zitasaidia katika kuinua sekta ya Uvuvi hapa nchini, huku akitoa rai kwamba suala la kupambana na Uvuvi haramu katika ziwa Victoria lisiingiliwe na itikadi za kisiasa pale watendaji wa sekta ya uvuvi wanapokuwa wakitekeleza majukumu yao.
Dk.Kamani na Wanahabari katika Mahojiano.
 Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Mh.Baraka Konisaga aliahidi kushirikiana na wamiliki wa viwanda vya kuchakata Samaki Mkoani Mwanza, Sanjari na Wavuvi wenyewe kwa lengo la kuboresha Sekta hiyo ya Uvuvi Mkoani Mwanza.


‘Nitatumia ushawishi wangu pindi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Evarist Ndikilo ambae yuko nje ya nchi kwa shughuli za kiofisi, atakaporejea katika majukumu yake ili aweze kukutana na wavuvi pamoja na wamiliki wa viwanda vya samaki Mkoani Mwanza ili kujadili nini cha kufanya ili kuboresha sekta hii”. Alisema Konisaga huku akionyesha tabasamu kama ilivyo kawaida ya kiongozi huyo ambae anafahamika kwa jina la Mtumishi wa Mungu.
Dk.Kamani
Akitoa Mchango wake kama miongoni mwa wamiliki wa Viwanda Mkoani Mwanza ambao wamekutana na Dk.Kamani ambae ni Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi,  Murtaza Alloo ambae ni Mkurugenzi wa Kampuni ya VicFish alieleza kwamba viwanda vikubwa havijishughulishi na ununuzi wa samaki wachanga (wanaovuliwa kwa njia haramu), badala yake suala hilo hufanywa na baadhi ya viwanda vidogo vidogo vyenye leseni na hivyo kuomba Serikali kuvichukulia hatua viwanda hivyo.


Aidha alimtaka Waziri Kamani kubainisha viwanda ambavyo anadhani vinanunua samaki ambao ni wachanga, (wanaovuliwa kwa njia haramu), jambo ambalo Dk.Kamani amebainisha kwamba si vyema kuliweka hadharani na hivyo kuvionya viwanda hivyo kwa kuvitaka kuachana na tabia hiyo la sivyo vitachukuliwa hatua kali za kisheria.

Takribani wamiliki na wawakilishi wa Viwanda vinane vya Kuchakata mazao ya Samaki Mkoani Mwanza waliweza kujumuika kwa pamoja na Dk.Kamanin katika kikao hicho, ambapo suala kubwa lililosisitizwa ni juu ya kila mmoja kwa nafasi yake kuhakikisha kuwa anaisaidia Serikali katika kutokomeza uvuvi haramu ili kuwa na uvuvi endelevu hapa nchini, huku wamiliki hao wakisisitizwa zaidi kutonunua mazao ya samaki yaliyovuliwa kwa njia haramu.

Viwanda hivyo ni Nile Perch Feshers, Kagera Fish, Omega Fish, Tz Fish & Musoma Fish, VicFish na Victoria Fish ambapo mara baada ya Dk.Kamani kuzungumza na wawakilishi na wamiliki hao wa Viwanda, pia alipata fursa ya Kuzungumza na baadhi ya wavuvi na viongozi wao Mkoani Mwanza.

No comments:

Powered by Blogger.