LIVE STREAM ADS

Header Ads

SERIKALI KUFUTA ADA KWA SHULE ZA SEKONDARI HAPA NCHINI.

Serikali imesema kuwa itahakikisha kwamba inaondoa ada kwa shule za Sekondari hapa nchini ili kila mwanafunzi anaeanza darasa la kwanza aweze kupata fursa ya kusoma hadi kufikia kidato cha nne.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr.Jakaya Mrisho Kikwete aliyasema hayo hii leo, wakati akizindua Sera ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi ya mwaka 2014 katika hafla iliyofanyika katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Majani ya Chai iliyopo Jijini Dar es Salaam.

Rais Kikwete alisema kuwa kupitia Sera hiyo, Serikali imeadhimia kwamba suala la elimu ya kidato cha nne liwe suala la lazima kwa kila mwanafunzi hivyo ili suala hilo liweze kufanikiwa Serikali imeona ni vyema kuanzia mwakani ikaondoa ada kwa Shule za Sekondari zinazomilikiwa na Umma.

Alisema Sera ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi inatoa mwanzo na Matumaini mapya katika Sekta ya Elimu hapa nchini ambapo ameongeza kuwa Sera hiyo ni nyenzo mhimu kulipeleka Taifa katika Ukombozi ifikapo mwaka 2025.

Aidha alibainisha kwamba Sera hiyo imeadhimia kuwa kila mtoto anapaswa kuanza darasa la awali kabla ya kuanza darasa la kwanza huku akibainisha kwamba mwanafunzi ambae atamaliza darasa la saba bila kujua kusoma na kuandika hataweza kuruhusiwa kuendelea na Masomo ya Sekondari.

Kuhusu Mkanganyiko wa Vitabu vya kufundishia mashuleni, Rais Kikwete alisema kuwa yanahitajika mabadiliko ili kuhakikisha kwamba shule zote hapa nchini zinakuwa na Vitabu vya aina moja (vyenye mtaala mmoja) ambavyo vitatumika kufundishia katika Shule zote hapa nchini.

Aidha aliongeza kuwa Sera hiyo ya Elimu inalenga kutoa mwongozo wa kupanga viwango vya ada kwa shule zinazomilikiwa na taasisi ama watu binafsi badala ya kila shule kujipangia ada yake kadri inavyotaka jambo ambalo limekuwa likilalamikiwa na wadau mbalimbali wa elimu.

Lakini pia Rais Kikwete aliwasihi waalimu kutambua umuhimu wao katika kuleta mabadiliko chanya katika jamii na Taifa kwa ujumla ambapo amewataka kutimiza wajibu wao ipasavyo kwa kuwa Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya wao kufanyia kazi huku akitoa rai kwa wamiliki wa shule binafsi na wao kutimiza ipasavyo wajibu wao na hivyo wajiepushe na kuifanya elimu kuwa biashara.

Sera ya Elimu ya Mwaka 2014 ambayo imezinduliwa rasmi hii leo na Rais Kikwete imelenga kuboresha kiwango cha elimu hapa nchini ikiwa ni pamoja na kuongeza miundominu ya elimu ikiwemo Maabara, Madarasa, Madawati pamoja na Waalimu.


Hafla hiyo ya Uzinduzi wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 pia ilihudhuriwa na Waziri wa elimu na Mafunzo ya Ufundi Mh. Shukuru Kawambwa, Naibu wake Kassim Majaliwa pamoja na Katibu Mkuu Wizara hiyo pamoja viongozi mbalimbali wa Kitaifa na Kimataifa.
N: George Binagi-GB Pazzo

No comments:

Powered by Blogger.