LIVE STREAM ADS

Header Ads

RITA YAANZA KUSAJILI NA KUTOA VYETI VYA KUZALIWA MKOANI MWANZA. MULONGO ATETA JAMBO.

Naibu Waziri wa Katiba na sheria Mhe Ummy Mwalimu (Wa tano waliokaa) akiwa katika picha ya kumbukumbu na baadhi ya Wageni waliohudhuria uzinduzi wa Mkakati huo hivi karibuni Malaika Hotel Mkoani Mwanza.
Na:George GB Pazzo
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Magesa Mulongo amewataka watumishi wa Afya Mkoani Mwanza kuhakikisha kuwa wanazingatia maadili ya kazi yao, katika kuwasajili bure na kwa wakati watoto walio chini ya Umri wa Miaka Mitano ili waweze kupatiwa Vyeti vya Kuzaliwa.

Hayo yalibainishwa jana na Mkuu wa Wilaya ya Sengerema Zainab Telaki wakati akizungumza kwa niaba yake katika Uzinduzi wa Kampeni ya siku saba ya Usajili na Utoaji wa Vyeti vya Kuzaliwa bure kwa watoto waliochini ya Umri wa Miaka Mitano Mkoani Mwanza uliofanyika Wilayani humo.

Alisema kuwa watumishi wote katika Vituo vya Tiba watakaohusika katika Kampeni hiyo kuzingatia utaratibu uliowekwa ambao ni pamoja na kuepuka vitendo vilivyo kinyume na maadili ya utumishi wa Umma hususani vitendo vya Rushwa kwani zoezi hilo la kusajili na kutoaji wa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto walio na umri chini ya Miaka Mitano linaendeshwa bila malipo yoyote.

Nae Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini RITA Emmy Hudson alibainisha kuwa Kampeni  hiyo ya usajili kwa watoto waliochini ya Umri wa Miaka Mitano itaendeshwa kwa muda wa siku saba katika Wilaya zote Mkoani Mwanza.

Alisema baada ya Kampeni hiyo kukamilika zoezi litaendelea katika Vituo vyote vya Afya vipatavyo 282 Mkoani Mwanza ambapo takribani Watoto Laki tano na Elfu hamsini na Mbili wanatarajiwa kusajiliwa na kupewa Vyeti Mkoani Mwanza.

Wakizungumza baada ya watoto wao kusajiliwa na kupatiwa vyeti vya kuzaliwa, Rahel Charles Timba, Mzee Yohana pamoja na Magreth Kalist ambao wote ni Wazazi kutoka Wilayani Sengerema waliipongeza Serikali kwa kuendesha zoezi hilo bure na kuongeza kuwa wamefurahishwa zaidi kuona kwamba linaendeshwa katika Vituo vya Afya tofauti na ilivyokuwa hapo awali ambapo Vyeti vya kuzaliwa vilikuwa vikitolewa katika Ofisi za Wakuu wa Wilaya ambapo waliisihi Serikali kuangalia pia utaratibu wa zoezi kama hilo kufanyika kwa wananchi walio na Umri zaidi ya Miaka Mitano.

Kampeni ya Usajili na Utoaji wa Vyeti kwa Watoto walio chini ya Umri wa Miaka Mitano linasimamiwa na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini nchini RITA katika mfumo wa teknolojia ya Internet ambapo usajili hufanyika na mtoto kupewa Cheti cha Kuzaliwa papo hapo ambapo linaendeshwa katika Mikoa ya Tanzania bara.
Tazama picha za Uzinduzi wa Kampeni hiyo Mkoani Mwanza HAPA
                                                           Credit:Radio Metro

No comments:

Powered by Blogger.