NI AIBU KWA SERIKALI YA "HAPA KAZI TU" KUSHINDWA KUAINISHA MPANGO WAKE WA MAENDELEO.
Shughuli ya kwanza ya Serikali
baada ya uchaguzi ni kuwasilisha Mpango wa Maendeleo wa miaka mitano (kutafsiri
ilani yake kwenda kwenye Mpango wa utekelezaji).
Bunge linapaswa kujadili na kuidhinisha Mpango wa Maendeleo wa miaka Mitano na kisha Mpango wa mwaka mmoja kuanza kutekeleza Mpango huo wa miaka 5. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (JMT) Ibara ya 63(3)(c), Mpango wa Maendeleo wa miaka Mitano hutungiwa sheria kwa ajili ya utekelezaji.
Leo Serikali ya Rais John Magufuli ilipangiwa kuwasilisha Mpango
huo wa Maendeleo wa miaka Mitano. Imeshindwa. Imeleta mwelekeo wa Mpango. Haikuleta
sheria na Kamati ya Bajeti Imeleta maelezo yake kuhusu Mpango wa Maendeleo wa mwaka
mmoja ilhali hakuna Mpango wa Miaka Mitano.
Mwenyekiti wa bunge Andrew Chenge alitaka wabunge
wajadili kwa mujibu wa kanuni ya 94 ambayo kimsingi ni Kanuni inayohusu Mpango
wa mwaka mmoja. Serikali imejichanganya. Uongozi wa Bunge umechanganyikiwa.
Bunge linapaswa kuagiza Serikali ikalete Mpango wa Maendeleo wa miaka Mitano ili uidhinishwe na utungiwe Sheria kabla ya kuanza kujadili mipango ya mwaka
mmoja mmoja.
Ni aibu kubwa kwa Serikali ya #HapaKaziTu kushindwa kuleta Bungeni
Mpango wake wa Maendeleo wa miaka Mitano na hata ule wa mwaka wake wa kwanza.
Itapangaje bajeti zake? Itatekeleza vipi ilani yake? Kuongoza nchi sio kutumbua
majipu tu, ni kuendesha nchi.
Zitto Kabwe (Mb)
Kigoma Mjini
No comments: