MAADHIMISHO YA VYOMBO VYA HABARI 2016 KUFANYIKA MKOANI MWANZA.
Taarifa kwa Vyombo vya Habari; Dar es Salaam, Aprili 27, 2016
Wanahabari na wadau wa habari mwaka huu watakutana jijini
Mwanza kuadhimisha Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani (WPFD).
Maadhimisho hayo yatafanyika katika hoteli ya Malaika Beach Resort jijini humo
kuanzia Mei 2 hadi 3, 2016.
Mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya mwaka huu ni
Mheshimiwa Jaji Mkuu wa Tanzania Mohamed Chande Othman. Wageni wengine
mashuhuri watakaohudhuria maadhimisho hayo ni pamoja na Waziri wa Habari,
Michezo, Utamaduni na Wasanii, Mhe. Nape Nnauye (mbunge), Mratibu Mkazi wa
Umoja wa Mataifa, mh. Alvaro Rodriguez, Balozi wa Umoja wa Ulaya (EU) mh.
Roeland van de Geer, Mwakilishi Mkazi wa UNESCO Zulmira Rodrigues.
Wengine ni watu mashuhuri mbalimbali kutoka Serikalini,
wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa na Mabalozi wanaowakilisha nchi zao
Tanzania wamethibitisha kushiriki. Wengine ni pamoja na watendaji wa vyombo vya
habari, Wabunge, wakuu wa Taasisi za kitaifa zisizo za Kiserikali, Vyuo vya
Uandishi wa Habari, wajumbe wa asasi za kiraia, waandishi wa habari wakongwe.
Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani ni tukio kubwa la
mwaka kwa vyombo vya habari na kauli mbiu ya mwaka huu ni Kupata taarifa ni
haki yako ya msingi: Idai.
Wakati wa maadhimisho haya, tunakumbuka gharama ambayo watu
binafsi wanalipa kwa kutoa habari, na kuwakumbuka kwa namna ya pekee watu hao
ambao wakati mwingine kwa kutoa kwao habari wanahatarisha maisha yao na kuweka
hatarini uhuru wao wenyewe, ili sisi tuweze kupata habari vizuri na kuufahamu
ukweli.
Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani, inayoadhimishwa
Mei 3 kila mwaka duniani kote, ilianzishwa na Umoja wa Mataifa kusherehekea
kanuni za uhuru wa habari na kuwakumbuka wale waliokufa wakati wakijaribu
kutekeleza kanuni hizo. Siku hii hutumika kama jukwaa ambalo hutumiwa na wadau
wa vyombo vya habari kushinikiza mataifa kutengeneza sheria rafiki za vyombo
vya habari zinazoweza huhakikisha uhuru wa habari katika nchi zao.
Maadhimisho ya siku hii kwa mwaka huu wa 2016,
yanaadhimishwa sawia na matukio muhimu matatu ya kihistoria:
Maadhimisho ya miaka 250 sheria ya kwanza ya uhuru wa habari
duniani, ikijumuisha nchi za sasa za Sweden na Finland.
Maadhimisho ya miaka 25 ya kupitishwa kwa Azimio la Windhoek
Azimio la kanuni ya uhuru wa habari.
Mwaka 2016 pia ni mwaka wa kwanza wa mzunguko wa miaka 15 wa
Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs).
Kutokana na hali hii, Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari
Duniani kwa mwaka 2016 inaonyesha uhusiano kati ya uhuru wa habari, utamaduni
wa uwazi na haki ya uhuru wa habari, na maendeleo endelevu katika wakati wa
digitali. Jambo muhimu katika haya yote ni jukumu la msingi kwa waandishi wa
habari, na umuhimu wa kuwalinda wale ambao huleta huduma hii kwa umma.
Mkutano huo pia utatoa nafasi ya kujadili na kushauriana
kuhusu maana ya sheria ambazo serikali imezipitisha na kuwasilishwa kwa mara ya
kwanza katika Bunge mwaka jana. Zinajumuisha Sheria ya Makosa ya Mtandao,
Sheria ya Takwimu, Muswada wa Huduma ya Habari na Sheria ya Upatikanaji wa
Habari.
Wakati wa tukio hilo waathirika wa ukiukwaji wa uhuru wa
habari watatoa ushuhuda juu ya changamoto walizokabiliana nazo wakati wa
utekelezaji wa majukumu yao.
Taarifa kuhusu ya hali ya vyombo vya habari katika Kusini
mwa Afrika iliyoandaliwa na Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika -
MISA inayojulikana kama Je Hii ni Demokrasia? itazinduliwa sambamba na Sera ya
Jinsia kwa Vyombo Vya Habari vya Jamii.
Maadhimisho haya yanatarajiwa kuhudhuriwa na wadau
wasiopungua 250, wa hapa nchini.
Maadhimisho haya yameandaliwa kwa pamoja na MISA-Tanzania,
UNESCO, Baraza la Habari Tanzania (MCT), Mfuko wa Vyombo vya Habari Tanzania
(TMF), Umoja wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Umoja wa Mataifa
Ofisi ya Tanzania, Taasisi ya Konrad-Adenauer-Stiftung Tanzania (KAS), Chama
cha Wamiliki wa Habari Tanzania (MOAT), Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF),
Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), Klabu ya Waandishi wa
Habari Mwanza na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Imetolewa na Muungano wa Vilabu vya Waandishi wa Habari nchini UTPC
No comments: