LIVE STREAM ADS

Header Ads

JICHO LA BMG: HAKUNA HAJA KILA MARA POLISI KUTUMIA NGUVU KUBWA KUZUIA MIKUTANO YA VYAMA VYA UPINZANI.


Jeshi la polisi kikosi cha kuzuia ghasia (FFU) Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, jana limetumia mabomu ya machozi na maji ya kuwasha, kuwatawanya viongozi na wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema, ili wasifanye mkutano wa uzinduzi wa "Oparesheni Okoa Demokrasia" nchini.

Mkutano huo ambao ulikuwa umepangwa kufanyika katika uwanja wa CDT, ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Chadema, akiwemo Mwenyekiti wa chama hicho taifa, Freeman Mbowe, ambapo pamoja na mambo mengine ulilenga kuwaeleza wananchi juu ya hatua za wabunge wa upinzani waliopewa adhabu ya kutohudhuria vikao kadhaa vya bunge.

Hayo yalijiri sanjari na zuio la jeshi la polisi nchini kupitia kwa Kamishina wa Operesheni na MafunzoNsato Mssanzya, kupiga marufuku maandamano na mikutano ya hadhara kuanzia tarehe jana june 07, 2016 hadi hapo hali ya usalama itakapokuwa sawa.

Wakati zuio hilo linatolewa na polisi, tayari vyama vya upinzani kama Chadema na ACT Wazalendo, vilikuwa vimepewa ridhaa ya kufanya mikutano yake ya hadhara ambapo duru za habari zinaeleza kuwa kuliibuka ombi jingine la Chama cha Mapinduzi CCM, kuomba ridhaa ya kufanya mikutano yake ya hadhara, jambo ambalo kiusalama lilitafsiriwa tofauti kuwa huenda linaweza kusababisha fujo kwa kuwa CCM ina lengo la kujibu yale yatakayokuwa yakizungumzwa katika mikutamo ya vyama vya upinzani. Ni kutokana na duru hizo, jeshi la polisi likaamua kuzuia mikutano yote ya hadhara iliyokuwa imeratibiwa na vyama vya upinzani nchini.

Suala kubwa hapa si kuzuia mikutano ya upinzani na kutumia nguvu kubwa kuwapiga mabomu wananchi wasio na hatia, bali busara ilipaswa kutumika kwa jeshi la polisi kutoa vibali kwa vyama vya siasa kufanya mikutano yake kwa awamu huku jeshi hilo likichukua jukumu la kuhakikisha usalama katika mikutano hiyo inakuwepo.

Hatua zinazochukuliwa na polisi kila mara hususani vyama vya upinzani vinapokuwa vinaratibu mikutano yake ya hadhara itafika pahala zitatafsiriwa vibaya kuwa ni ukandamizaji wa demokrasia nchini na kwamba chombo hicho muhimu kiusalama katika nchini kinatumika vibaya katika kuukandamiza upinzani.

Hakuna haja ya jeshi la polisi kila mara (kama ilivyotokea Kahama), kutumia nguvu kubwa ikiwemo mabomu ya machozi na magari yenye maji ya washawasha kuutawanya umati mkubwa wa wananchi wasio na hatia kwa kigezo cha kuhofia kikundi kidogo cha watu kufanya fujo na badala yake ni vyema nguvu hiyo ikatumika kupambana na kikundi hicho kidogo kinachodhaniwa kwamba kimejiandaa kufanya fujo katika mikutano hiyo.

No comments:

Powered by Blogger.