LIVE STREAM ADS

Header Ads

WALIOKAMATWA KATIKA MKUTANO WA CHADEMA MJINI KAHAMA WAPANDISHWA KIZIMBANI.


Na Shaban Njia
Wafuasi 22 wa Chama cha Demokrasia na Maendelea CHADEMA wakiongozwa na Mratibu wa Chama hicho, Kanda ya Serengeti, Renatus Pesa Nzemo, waliokamatwa katika jana katika mkutano wa chama hicho uliozuiliwa kufanyika na polisi, leo wamepandishwa kizimbani.

Walikamatwa jana na Jeshi la polisi kwa tuhuma za  kufanya mkusanyiko kinyume cha sheria  ambapo wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Kahama.

Waliofikishwa Mahakamani Renatus Pesa Nzemo(42), Godwin Godson(34), Amos Sipemba(41), Hamis Dominick (45), Rashid Ally (35), Emanuel Jidisha(48), Method Marco(39), Athuman Martin(38), Ally Juma(29), Mashaka Masudi(23) na Cosmas Thomas(26).

Wengine ni Simon Apolinary(24), Charles Elikana(27), Jovin Joel(20), Enock Mosha(29), Zakayo Deogratius(44), Abeid Kapina(18),  Omary Hassan(45), Kulwa Frank(28) , Yusuph Ibrahim(38), Peter Jonas(41)  pamoja na Anthony Lauwo(35).

Wakisomewa Shitaka hilo na  Mwendesha Mashitaka wa Jeshi la Polisi, Dismas Aniceth, mbele ya Hakimu Mkazi mfawidhi wa Wilaya ya Kahama,  Evodia Kyaruzi, ilidaiwa kuwa watuhumiwa hao walitenda kosa hilo jana majira ya saa 9.30 katika Uwanja wa CDT uliopo Mjini Kahama.

Katika kesi hiyo namba 319 ya mwaka 2016, ilidawa kuwa watuhumiwa hao walifanya mkusanyiko huo katika viwanja hivyo kwa lengo la kufanya uvunjifu wa amani hali iliyosababisha  jeshi la Polisi kutumia nguvu kuwatawanya wanachama na wafuasi wa chama hicho waliokusanyika kuwasikiliza viongozi wao.

Baada ya kusomewa Shitaka hilo Mahakamani hapo, Washitakiwa wote walikana shitaka hilo na kufanya Mwendesha mashitaka kuomba tarehe kwa ajili ya usiklizwaji wa awali kwa kuwa upelelezi wa Shauri hilo ulikuwa umekamilika.

Aidha Hakimu Kyaruzi aliwaambia Washitakiwa dhamana ipo wazi kwa kila  mmoja ambapo kila mshitakiwa alitakiwa kuwa Mdhamini mmoja na dhamana ya shilingi 500,000 hata hivyo kesi hiyo imeahirishwa hadi tarehe juni 16 mwaka huu kwa ajili ya usikilizwaji wa awali.

Hadi tunakwenda mitamboni, watumiwa watatu kati ya 22 ndio waliokuwa wamepata dhamana Mahakamani hapo, ambao ni Amas Sipemba, Zakayo Kasano pamoja na Peter Jonas huku wengine wakiongozwa na Mratibu wa Kanda ya Serengeti, Renatus Pesa, wakiendelea kusubiri wadhamini wao.

No comments:

Powered by Blogger.