LIVE STREAM ADS

Header Ads

Serikali kuendelea kuwalinda Wanasayansi watafiti wa ndani na nje ya nchi.

Ikiwa Una Habari, Tukio, Picha, Maoni au Tangazo, Wasiliana Na BMG Kwa Nambari za Simu 0757 432694 Au Email binagimediagroup@gmail.com
dsc_2081Na Andrew Chale
Makamu wa Rais Mh. Mama Samia Suluhu Hassan amewahakikishia Wanasayansi Watafiti waliopo nchini kuwa Serikali ya Tanzania inatambua mchango wao  na wataendelea na juhudi za kuwalinda kwani ni nguzo muhimu ya kufikia malengo ya milenia katika Nyanja mbalimbali ikiwemo Uchumi, Afya, Elimu na Maendeleo endelevu.

Makamu wa Rais ameyasema hayo mapema leo Jijini Dar es Salaam wakati alipozindua rasmi Kongamano la 30 la Kimataifa la Wanasayansi Watafiti lililoandaliwa na Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) ambalo ni la siku tatu kuanzia  Oktoba 4 hadi 6.2016.

Akiwahutubia Wanasayansi hao watafiti zaidi ya 300 kutoka Tanzania na Mataifa ya Nje,  amesema kuwa Taifa bila watafiti hakuna maendeleoo hivyo uwepo wa watafiti hao ni kielelezo tosha cha kufikia maendeleo hivyo anaamini kuwa baada ya mkutano huo, Wataalam hao watakuwa chachu ya kichocheo cha uchumi kupitia tafiti zao.

Akiwaondoa hofu wanasayansi watafiti hao, Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu amebainisha kuwa, Serikali imesikitishwa na tukio lililotokea hivi karibuni la kuchomwa moto baadhi ya watafiti huko Mkoani Dodoma kuwa ni la kinyama na halivumiliki na sheria itachukua mkondo wake na wahusika wote watafikishwa mikononi mwa sheria.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mh. Dk. Hamisi Kigwangalla katika mkutano huo amebainisha kuwa,  Wizara yake inashirikiana bega kwa bega na wanasayansi na imekuwa ikiwatumia katika mikakati mbalimbali ya kitaifa na hata kujenga sera za Afya na mambo mengine ya kimaendeleo.

“Wanasayansi  watafiti kwa uzoefu wao tunautumia kwa kiwango kikubwa sana hapa nchini. Kwani wamekuwa chachu kubwa sana na hata mfumo wa Kiserikali umekuwa ukitengeneza mfumo mahususi wa kufanya kazi kwa pamoja kwani hata sera na mikakati ya nchi pia tumekuwa tukiwatumia wanasayansi hao” amesema Dk.  Kigwangalla.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NIMR, Dk. Mwele Malecela amesema kongamano hilo linajumuisha nchi mbalimbali za Afrika, Ulaya na Amerika ambapo washiriki zaidi ya 300 wanashiriki  huku mada zaidi ya 220 zitawasilishwa na kujadiliwa kwa pamoja na wataalam hao.

“Jumla ya mada 220 zinawasilishwa kuanzia leo na kujadiliwa katika Kongamano hili la Siku tatu ambalo pia litahusisha mkutano Mkuu wa mwaka wa NIMR”. Amesema Dk. Mwele.

Katika kongamano la mwaka huu, linaongozwa na kauli mbiu ya “Uwekezaji katika tafiti zenye ubunifu ili kufikia malengo endelevu ya dunia”.

Nchi ambazo zinashiriki kongamano hilo kuwa ni Afrika Kusini, Kenya, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Uganda, Australia, Denmark, Ubeljiji, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani, Uswis, Kanada, Sweden, Norway, Marekani, Bangladesh, Thailand na wenyeji Tanzania.

No comments:

Powered by Blogger.