Mabatini Stars yazidi kupasua anga Ndondo Cup Jijini Mwanza
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Wachezaji wa timu ya Mabatini Stars wakisikiliza maelekezo kutoka kwa viongozi wa timu hiyo
Judith Ferdinand,Mwanza
Timu ya Mabatini Stars imefanikiwa kufuzu kuingia nusu fainali katika mashindano ya Ndondo Cup 2017, yanayoendelea kutimua vumbi uwanja wa Nyamagana Jijini Mwanza, baada ya kuichapa Iseni Fc goli 1-0.
Katika mchezo huo wa hatua ya robo fainali ya mashindano hayo, ulizikutanisha timu hizo,ambapo Mabatini Stars ilifunga goli lililoipa ushindi timu hiyo dakika ya 42 kupitia mshambuliaji wake Frank Kulwa.
Licha ya ushindi huo Mabatini star,ilionekana kucheza chini ya kiwango na kuzidiwa mashambulizi na Iseni Fc japo bahati haikua upande wao.
Hata hivyo Salum Kipemba kutoka Mabatini Stars aliibuka mchezaji bora wa mechi hiyo, na kujinyakulia kitita cha shilingi 50000 ambapo 30000 kutoka kwa HASFU Barber Shop na 20000 alipatiwa na msanii wa bongo flava H- Baba.
Kipemba alisema,ataendelea kuisaidia timu yake,ili iweze kuibuka mabingwa wa mashindano hayo.
Kwa upande wake Nahodha wa timu ya Mabatini Stars Frank Kulwa alisema, anashukuru kwa ushindi walioupata,licha ya kutofanya vizuri kutokana na wachezaji kujisahau baada ya kufunga goli,hivyo wanaenda kujipanga kwa kufanya mazoezi ili waweze kufanya vizuri kwa hatua zinazofuatia na hatimaye kuibuka mabingwa.
Naye Kocha wa Mabatini star Omar Bakar alisema, walipata wakati mgumu kutokana na wapinzani wao Iseni Fc kucheza vizuri, ila anamshukuru Mungu bahati ilikua upande wao.
Aidha Kocha wa Iseni Fc Mhando Nikisalala alisema, anamshukuru Mungu japo hawakutegemea kupata matokeo hayo,kwani wao walijipanga kushinda pia vijana hao wamejitahidi licha ya kukutana na timu kongwe.
No comments: