Wazee Jijini Mwanza waigeukia Serikali
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Picha kutoka maktaba
Judith Ferdinand, Mwanza
UMOJA wa Wazee Kata ya Kirumba (UWAZEKI) uliopo wilayani Ilemela mkoani Mwanza, umesema serikali imekuwa haiwashirikishi kwenye miradi ya maendeleo inayotolewa katika maeneo yao zikiwemo tenda mbalimbali ambazo huwabagua na kuwapa kipaumbele vijana na akina mama.
Malalamiko ya wazee hao yalibainishwa wakati wakizungumza ofisini kwao mtaa wa Ngara katani hapo, ambapo walizungumzia changamoto mbalimbali wanazokutanazano huku wakiiomba serikali kuboresha dirisha la wazee ili wapate huduma stahiki.
Mwenyekiti wa Umoja huo Deodatus Mtamizi, akizungumza kwa niaba ya wazee hao alisema ni vema serikali kuweka uratatibu wa kuwapatia fedha kama asilimia 10 wanavyopatiwa vijana na wakinamama zinazotokana na mapato yanayokusanywa na halmashauri, ili nao waweze kujikwamua kiuchumi na kuacha kuwa tegemezi.
“Tunaomba serikali itushirikishe na sisi katika miradi ya maendeleo inayotolewa katika maeneo yetu kwa mfano tenda mbalimbali ambazo zinatolewa kwani hushirikisha vijana na akina mama lakini wazee tunawekwa pembeni kitendo ambacho siyo kizuri,”alisema Mtamizi.
Hata hivyo aliendelea kuiomba serikali kuwajali , kuwathamini na kuwafikiria wazee kwa kuwakatia bima ya afya kwani hawana uwezo wa kukata kutoka na kukosa fedha na uchumi kuyumba.
“Wazee wengi tunategemea kupewa fedha na watoto wetu, wajukuu na wasamalia wema kutokana na hali ya uchumi kuwa ngumu, imekuwa tatizo kwani wengi hufia ndani kwa kushindwa kwenda hospitali kwa kukosa fedha,alisema Mtamizi.
Vilevile alisema, wazee ni dhahabu ya kijani ni vema kuwathamini kwa kuwa karibu nao ili kuweza kutambua kero zao zinazowakabili na kuzitatua.
Aidha waliomba viongozi kuweka utaratibu wa kuwatembelea katika vyama vyao, ili kutambua kero zinazowakabili sambamba na kupata ushauri kutoka kwao katika kuendesha nchi hii, kwani wanajua mambo mengi ambayo yatasaidia kuleta maendeleo na kukuza uchumi wa viwanda.
"Ikumbukwe kuwa wazee tupo na tulikuwepo na tutaendelea kuwepo ni lazima watambue umuhimu wetu,”alisema Mtamizi.
No comments: