LIVE STREAM ADS

Header Ads

Mbunge jimbo la Ilemela avutiwa na kasi ya wakazi wa Kiseke

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Judith Ferdinand, BMG
Mbunge wa Jimbo la Ilemela mkoani Mwanza Mhe.Angeline Mabula amewahimiza wakazi wa Kata ya Kiseke jimboni humo kutoa ushirikiano wa kutosha ili kufanikisha ujenzi wa shule ya sekondari ya Kata hiyo.

Mhe.Mabula ambaye pia ni Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ametoa rai hiyo alipofanya mkutano wa hadhara katika Kata hiyo na kubainisha kwamba urithi pekee kwa mtoto hivi sasa ni elimu.

Alisema ujenzi wa shule hiyo ukikamilika wanafunzi wataondokana na adha ya kutembelea umbali mrefu na hivyo kuondokana na changamoto kadhaa ikiwemo vishawishi hususani kwa watoto wa kike na hivyo kujiepusha na mimba za utotoni.

Mhe.Mabula alisema wananchi wakishiriki kwenye miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa madarasa kwa kunyanyua boma, serikali pamoja na ofisi yake itawaunga mkono kwa kukamilisha majengo hayo ambapo alitumia mkutano huo kuendesha harambee fupi na kufanikiwa kuchangisha shilingi 125,200, mifuko ya saluji 69 pamoja na tripu 12 za mawe.

Naye Mkurugenzi Manispaa ya Ilemela, John Wanga aliwapongeza wananchi wa manispaa hiyo kwa kujitoa kushirikiana na serikali katika miradi ya maendeleo na kuwahimiza kuendelea na desturi hiyo kwa manufaa yao.

Katika kuunga mkono juhudi za wananchi, Meneja wa benki ya NMB tawi la Rock City, Jacqueline Timoth alisema benki hiyo inaunga mkono juhudi za maendeleo katika jamii hivyo itasaidia ujenzi wa vyoo katika shule ya sekondari Kiseke.


Awali Afisa Mtendaji wa Kata ya Kiseke, Hellen Mcharo alisema zinahitajika shilingi Milioni 102.58 ili kukamilika kwa ujenzi wa shule hiyo ambayo itakuwa na vyumba vinne vya madarasa, ofisi vyumba vitatu na choo chenye matundu 12 ambapo matundu 10 yatakuwa ya wanafunzi na mawili walimu.

No comments:

Powered by Blogger.