LIVE STREAM ADS

Header Ads

Naibu Waziri Biteko atatua mgogoro uchimbaji madini Tarime

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kulia) akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Glorious Luoga (kushoto) mara alipowasili katika wilaya hiyo kwa ajili ya kukagua shughuli za uchimbaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero mbalimbali za wachimbaji wa madini.

Na Greyson Mwase, Tarime
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko ametatua mgogoro kwenye machimbo ya madini  ya dhahabu  ya Msege  yaliyopo wilayani Tarime mkoani Mara  kwa kuitaka kampuni inayojishughulisha na uchimbaji wa madini hayo ya Everson Limited kuhakikisha inasaini mikataba kati yake na wachimbaji wadogo wa madini wanaoendesha shughuli za uchimbaji madini na kushirikiana kwa karibu zaidi.

Naibu Waziri Biteko ametoa agizo hilo mara baada ya kutembelea machimbo  hayo jana Septemba 19, 2018 na kusikiliza kero za wachimbai wadogo wa madini  ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika mikoa ya Mara  na Geita yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero mbalimbali  zinazowakabili wachimbaji wa madini.

Katika hatua nyingine, Biteko alimtaka mmiliki wa kampuni ya Everson Limited, Mwita Wambura kuhakikisha anasimamia makubaliano aliyojiwekea kati ya wachimbaji wadogo wa madini na kampuni yake huku akihakikisha sheria na kanuni za uchimbaji wa madini zinafuatwa.

Alisema kuwa mara baada ya kusikiliza maelezo ya pande zote mbili yaani kampuni na wachimbaji hao alibaini kuwa kampuni husika ilikataa kusaini mikataba kati yake na wachimbaji wadogo wa madini kinyume na makubaliano hali iliyopelekea mgogoro kutokuisha.

“Haiwezekani kama kampuni mnakaa katika vikao kwa kushirikisha viongozi wa serikali na kukubaliana kuandaa mikataba ili kusaini halafu baadaye mnashindwa kutekeleza makubaliano, kama Serikali tunataka kuhakikisha kila upande unanufaika, huku Serikali ikipata mapato yanayostahili,” alisisitiza Biteko.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali ina haki ya kuchukua leseni ya kampuni  yoyote pale inapoonekana makubaliano kati yake na wachimbaji wadogo hayafuatwi hali inayosimamisha kukwama kwa shughuli za uchimbaji madini na kukosa mapato yake.

Wakati huo huo wananchi kutoka sehemu mbalimbali katika Wilaya ya Tarime walimpongeza Naibu Waziri Biteko kwa kuhakikisha kuwa mgogoro huo uliodumu kwa muda mrefu pasipo kupatikana suluhu unatatuliwa ndani ya kipindi kifupi na kusisitiza kuwa wataendelea kutoa ushirikiano kwa Wizara ya Madini kwa kuhakikisha wanafuata sheria na kanuni za madini huku  wakilipa kodi zote serikalini.

Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji wa madini, Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Mara,  Stephan Msseti alimpongeza Biteko kwa kuhakikisha amefika kwenye machimbo hayo na kutatua mgogoro na kufafanua kuwa sasa wachimbaji wadogo wataanza kuchimba katika mazingira ya amani na kuchangia ukuaji wa uchumi wa nchi.

Msseti alimtaka mmiliki wa kampuni ya uchimbaji wa madini ya dhahabu ya Everson Limited, Mwita Wambura kuhakikisha anaheshimu mamlaka za serikali kwa kuhakikisha anatekeleza makubaliano yote wanayojiwekea.

Awali akizungumzia mgogoro huo, mmiliki wa kampuni ya uchimbaji wa madini ya dhahabu ya Everson Limited, Mwita Wambura alisema kuwa mara baada ya kufanya utafiti na kuanza uchimbaji wa madini ya dhahabu katika eneo hilo, wananchi walianza kuvamia eneo hilo hali  iliyopelekea mgororo.

Alisema kuwa aliwaruhusu wachimbaji wadogo kuchimba madini katika mashimo matano lakini wachimbaji hao wamekuwa wakidhuru wafanyakazi wa kampuni hiyo kwa kuwapiga kwa kuwa si wakazi wa kijiji husika kauli ambayo ilipingwa na Diwani wa Kata wa Nyarukoba kupitia CHADEMA, Matiko Marwa.

Marwa mbali na kupongeza kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano kupitia Wizara ya Madini alimtaka mwekezaji huyo kutii makubaliano kwa kusaini mikataba ili kumaliza mgogoro.
Kabla ya kufanya ziara katika machimbo hayo, Naibu Waziri Biteko alikutana na Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Glorious Luoga na kuelezwa changamoto mbalimbali zinazoikabili  Wilaya hiyo hususan kwenye uchimbaji wa madini.

Luoga alieleza changamoto hizo kuwa ni pamoja na  ukusanyaji wa maduhuli kuwa mdogo kutokana na wachimbaji wadogo wengi kuchimba madini pasipo kutambulika, baadhi ya wachimbaji wadogo kuwepo kwenye  leseni zenye uwekezaji, utoroshwaji wa mawe yenye dhahabu na migogoro katika baadhi ya maeneo yenye shughuli za uchimbaji madini.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Ofisi za Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Tarime.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati mbele) pamoja na msafara wake wakiendelea na ziara katika machimbo ya dhahabu ya Msege  yaliyopo wilayani Tarime mkoani Mara
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akiangalia sehemu ya nyaraka mbalimbali za uchimbaji madini katika machimbo ya dhahabu ya  Msege  yaliyopo wilayani Tarime mkoani Mara.
Mmoja wa wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu katika machimbo ya dhahabu ya Msege  yaliyopo wilayani Tarime mkoani Mara akiwasilisha kero yake mbele ya Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko 
Sehemu ya wananchi wa kijiji cha Msege kilichopo wilayani Tarime mkoani Mara wakisikiliza ufafanuzi uliokuwa unatolewa na Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko 
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akitoa maelekezo kwa mmiliki wa kampuni inayojishughulisha na uchimbaji wa madini ya dhahabu katika eneo la Kisege Wilayani Tarime Mkoani Mara ya Everson Limited, Mwita Wambura (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza katika mkutano wa hadhara

No comments:

Powered by Blogger.