Kampuni za madini zajitokeza kwa wingi kuwekeza Tanzania
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini Profesa Idris Kikula (kushoto) akielezea takwimu za leseni
zilizotolewa na Tume ya Madini tangu kuanzishwa kwake kwenye mkutano wa
waandishi wa habari uliofanyika jijini Dodoma mapema tarehe 04 Oktoba, 2018.
Kulia ni Katibu Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya.
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini Profesa Idris Kikula (katikati) akitoa ufafanuzi alipokuwa
akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma. Kulia ni Katibu Mtendaji wa
Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya na kushoto ni Mkurugenzi wa Leseni na TEHAMA wa Tume ya
Madini, Torece Ngole.
Na Greyson Mwase, Dodoma
Mwenyekiti
wa Tume ya Madini, Profesa Idris Kikula amesema kuwa kati ya kipindi cha mwezi
Mei hadi Septemba mwaka huu, Tume ya Madini, imetoa leseni 7879 ambazo maombi
yake yaliidhinishwa kupitia kikao cha Tume kilichofanyika tarehe 25 Septemba,
2018 kilicholenga kujadili taarifa za
Kamati za Tume na utendaji kazi katika kipindi cha mwezi Mei hadi Septemba,
2018.
Profesa
Kikula ameyasema hayo leo tarehe 04 Oktoba, 2018 kupitia mkutano wa waandishi
wa habari uliofanyika katika Ofisi za
Tume ya Madini zilizopo jijini Dodoma.
Akielezea
kuhusu maombi ya leseni za madini 7879
yaliyoidhinishwa katika kikao cha Tume, Profesa Kikula alieleza kuwa ni pamoja na Leseni za Utafutaji wa Madini (Prospecting
License - (PL) 263; Leseni Kubwa (Special Mining License – (SML)
03;(ziliidhinishwa ili kupelekwa
kwenye mamlaka husika ambayo ni Baraza la Mawaziri) Leseni za Uchimbaji
wa Kati (Mining License - (ML) 14 pamoja na leseni 1 ya Sihia (Transfer) ya
uchimbaji wa Kati.
Aliendelea
kufafanua kuwa, maombi leseni za
uchimbaji wa kati 14 yaliyopitishwa kuwa ni pamoja na kampuni za Dangote Industries Limited kwa
ajili ya uchimbaji wa madini ya chokaa katika eneo la Mtwara; Nazareth Mining Investment Co Limited kwa
ajili ya uchimbaji wa madini ya kinywe (graphite) katika eneo la Ruangwa mkoani
Lindi na kampuni ya Sunshine Mining (T) Limited kwa ajili ya uchimbaji wa
madini dhahabu katika eneo la Chunya mkoani Mbeya.
Aliendelea
kutaja kampuni nyingine kuwa ni pamoja na Said Seif Abdallah kwa ajili ya
uchimbaji wa madini ya ujenzi katika eneo la Masasi mkoani Mtwara; Off Route
Technologies (T) Limited kwa ajili ya uchimbaji wa makaa ya mawe katika eneo la
Ileje mkoani Mbeya; leseni yenye ubia kati ya Shabani Daud Ibrahim, Andrew
Bollen, Dunstan M. Mongi na Vedastus Mtesigwa kwa ajili ya uchimbaji wa madini
ya dhahabu katika mkoa wa Geita.
Maombi
mengine yaliyopitishwa ni pamoja na leseni yenye ubia kati ya Jumbo Limited, na Ally Mbarak Mohamed kwa
ajili ya uchimbaji wa madini ya kinywe (graphite) katika eneo la Ruangwa mkoani
Lindi, Jacana Resources (Tanzania) Limited kwa ajili ya uchimbaji wa mchanga
bahari (mineral sand) katika eneo la Temeke lililopo jijini Dar es Salaam na P.
B. Mining Company kwa ajili ya uchimbaji wa madini ya fedha, dhahabu, shaba, zinki na galena katika
eneo la Chunya lililopo mkoani Mbeya.
Profesa Kikula
alisisitiza kuwa, kikao hicho pia kilipitisha ombi la kubadili umiliki kutoka
kwa Mbarouk Saleh Mbarouk kwenda katika kampuni ya M. B. Mining (T) Limited kwa
ajili ya uchimbaji wa madini ya ujenzi katika eneo la Morogoro.
Profesa
Kikula aliendelea kutaja maombi ya leseni nyingine zilizopitishwa katika kikao
hicho kuwa ni pamoja na Leseni za Uchimbaji Mdogo (Primary Mining License –
(PML) 6313; Leseni za Uchenjuaji wa Madini (Processing License) 08 na leseni za
Biashara ya Madini ambapo leseni kubwa (Dealers License) ni 557; na leseni Ndogo (Broker’s License) 720.
Katika hatua
nyingine Profesa Kikula alisema kuwa, Mipango ya Ushirikishwaji wa Utoaji wa
Huduma na Bidhaa kwa Wazawa katika Miradi ya Madini (local content plan) 19
ilipitishwa kati ya mipango 26 iliyowasilishwa kutoka katika kampuni mbalimbali
za utafutaji na uchimbaji wa kati na mkubwa wa madini.
Alielekeza
waombaji leseni za madini kuwasilisha mipango yao kwa wakati ili iweze kupitiwa
na kamati husika na kuwezesha leseni kutolewa mapema. Pia
aliwataka waombaji wote wa leseni za madini kufuatilia leseni zao kwenye Ofisi
za Madini zilizopo mikoani walikoombea leseni zao na kusisitiza kuwa orodha ya
leseni zilizoidhinishwa inapatikana katika tovuti ya Tume.
Wakati
huohuo Profesa Kikula alisema kuwa Tume ya Madini imejipanga katika kuhakikisha
kila mtanzania ananufaika ipasavyo na rasilimali za madini nchini Aliongeza
kuwa, Tume imeweka mikakati ya kuwasaidia wachimbaji wadogo wa madini kwa
kuwatengea maeneo kwa ajili ya uchimbaji madini na kuwataka kuunda vikundi na
kusajiliwa kupitia viongozi wao hivyo kuwezesha upatikanaji wa leseni za madini
na kufanya shughuli zao pasipo kikwazo chochote.
“Sisi kama
Tume ya Madini tunatambua mchango mkubwa wa wachimbaji wadogo wa madini na ndio
maana tumekuwa tukifanya ziara katika maeneo ya wachimbaji wadogo na kutatua changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja
na migogoro; tunataka wafanye kazi katika mazingira salama kabisa,” alisema
Profesa Kikula.
Naye Katibu
Mtendaji wa Tume ya Madini, Profesa Shukrani Manya akielezea mchango wa Sheria
Mpya ya Madini alisema kuwa tangu kuanza kwa utekelezaji wa sheria mpya
iliyoweka ongezeko la kutoka asilimia nne hadi sita za mrabaha na tozo la
asilimia moja la kodi ya ukaguzi wa madini,
makusanyo yameongezeka kutoka shilingi bilioni 194 hadi shilingi bilioni 301 kwa mwaka
likiwa ni ongezeko la asilimia 55.
Pia Mkurugenzi wa Leseni na TEHAMA kutoka Tume ya Madini, Torece Ngole akielezea
mikakati ya Tume katika kukabiliana na changamoto ya migogoro kwenye uchimbaji
wa madini inayosababishwa na wachimbaji wadogo kwa kuvamia maeneo yenye leseni
kubwa, alisema kuwa Tume imeshaanza kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji
wadogo na kusisitiza kuwa mpaka sasa imeshatenga maeneo 74.
Alisisitiza
kuwa Tume imekuwa ikiwaelimisha wachimbaji wadogo kuhusu sheria na kanuni za
madini na kusisitiza kuunda vikundi ili waweze kupatiwa maeneo na leseni za
uchimbaji madini.
No comments: