LIVE STREAM ADS

Header Ads

Mradi wa Boresha Chanjo wapata matokeo chanya mikoa ya Geita na Shinyanga

Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.

Serafina Mkuwa ambaye ni Meneja Program ya Afya ya Mama na Mtoto kutoka shirika la Amref Health Africa nchini Tanzania akifafanua jambo kwenye kikao cha mrejesho wa mafanikio ya mradi wa majaribio wa Boresha Chanjo (mVacciNation) unaotekelezwa katika mikoa ya Shinyanga na Geita kwa kipindi cha miaka miwili 2016/18 kilichofanyika jana Jijini Mwanza.
Meneja mradi wa mVacciNation, Nyerere Mwera akifafanua jambo kwenye kikao hicho.
Mwakilishi kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bonaventura Nestory akizungumza kwenye kikao hicho.
Joseph Manirakiza ambaye ni Naibu Mkuu wa mfuko wa HDIF akizungumza kwenye kikao hicho.
Afisa Chanjo wilayani Geita akizungumza kwenye kikao hicho.

Judith Ferdinand, BMG
Shirika la Amref Health Africa limefanikiwa kutekeleza vyema mradi wa majaribio wa “Boresha Chanjo (mVacciNation)”  katika mikoa ya Shinyanga na Geita katika kipindi cha miaka miwili kuanzia 2016/18.

Meneja mradi huo, Nyerere Mwera alisema kwa mkoa wa Geita utekelezaji wake umefanika katika Vijiji vya Halmashauri za Bukombe na Mbongwe huku mkoa wa Shinyanga ukitekelezwa katika Halmashauri za Msalala na Kahama.

Alisema katika kipindi cha miaka miwili, mradi huo umesaidia kuongeza idadi ya watoto waliofikiwa na huduma ya chanjo kutoka asilimia 93 hadi asilimia 98, kiwango cha upungufu wa chanjo katika Vituo vya Afya kimeshuka kutoka asilimia 78 hadi asilimia 28 huku usahihi wa taarifa za chanjo ukiongezeka kutoka asilimia 78 hadi asilimia 93.

Alisema mradi huo unafadhiliwa na shirika la Human Development Innovation  Fund (HDIF) pamoja na GloxSmithKline (GSK) ukilenga pia kuboresha ukusanyaji  na utoaji wa taarifa za chanjo kwa njia ya kielektroniki ili kusaidia kupunguza magonjwa na vifo vya watoto chini ya miaka mitano vinavyoweza kuzuilika.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Afya ya Mama na Mtoto kutoka shirika la Amref Africa nchini Tanzania, Serafika Mkuwa alisema serikali imekuwa ikitumia mifumo mbalimbali ya kielektroniki ili kuboresha ukusanyaji na utoaji taarifa sahihi za chanjo hivyo Amref kwa kuunga juhudi hizo imekuwa ikitekeleza mfumo huo kuanzia ngazi ya jamii  na vituo vya kutolea huduma za afya  kupitia watoa huduma wa ngazi hizo ili kuhakikisha kila mtoto anafikiwa na huduma ya chanjo.

Kwa upande wake Naibu Mkuu wa mfuko wa HDIF, Joseph Manirakiza alisema mfumo wa teknolojia ya kielektroniki unaoruhusu taarifa za chanjo kupatikana kwa njia rahisi ikiwemo simu na hivyo kusaidia utoaji wa huduma kwani huduma ya chanjo ilikua chini na kuigharimu serikali pesa nyingi kutibu magonjwa ambayo yanaweza kuzuilika kupitia chanjo.

Afisa Afya kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto kupitia Mpango wa Taifa wa Chanjo, Bonaventura Nestory alishauri mfumo wa utekelezaji wa mradi huo kuendelea kuimarishwa ili kusaidia upatikanaji wa huduma bora za chanjo nchini kwani serikali imekuwa ikigharamia huduma ya chanjo hivyo ni vyema ikawafikia wahitaji wengi.

Mganga mkoani Geita Dkkt. Japhet Simeo alikiri kwamba mradi huo umesaidia kuibua changamoto ambazo zitasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma bora za chanjo katika maeneo mbalimbali nchini.

Mratibu wa chanjo halmashauri ya Kahama Mjini, Mukola Phelecian alitoa shukurani kwa shirika la Amref kwa kuleta mradi huo akisema umesaidia kutunza dawa za chanjo kwa usahihi katika majokofu  pamoja na watoto kuzipata kwa wakati huku mratibu wa shughuli za chanjo wilayani Msalala, Deogratias Bwire akisema ili mradi huo uwafikie watoto wengi zaidi ni vyema watoa huduma ngazi ya jamii wakawezeshwa usafiri na kujengewa uelewa wa kutosha ili wasaidie kutoa hamasa kwa wananchi kuwasajili na kuwapeleka kliniki kwa wakati watoto wao.

No comments:

Powered by Blogger.