Mradi wa Boresha Chanjo wapata matokeo chanya mikoa ya Geita na Shinyanga
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Serafina Mkuwa ambaye ni Meneja Program ya Afya ya Mama na Mtoto kutoka shirika la Amref Health Africa nchini Tanzania akifafanua jambo kwenye kikao cha mrejesho wa mafanikio ya mradi wa majaribio wa Boresha Chanjo (mVacciNation) unaotekelezwa katika mikoa ya Shinyanga na Geita kwa kipindi cha miaka miwili 2016/18 kilichofanyika jana Jijini Mwanza.
Meneja mradi wa mVacciNation, Nyerere Mwera akifafanua jambo kwenye kikao hicho.
Mwakilishi kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bonaventura Nestory akizungumza kwenye kikao hicho.
Joseph Manirakiza ambaye ni Naibu Mkuu wa mfuko wa HDIF akizungumza kwenye kikao hicho.
Afisa Chanjo wilayani Geita akizungumza kwenye kikao hicho.
Judith Ferdinand, BMG
Shirika la
Amref Health Africa limefanikiwa kutekeleza vyema mradi wa majaribio wa “Boresha
Chanjo (mVacciNation)” katika mikoa ya
Shinyanga na Geita katika kipindi cha miaka miwili kuanzia 2016/18.
Meneja mradi
huo, Nyerere Mwera alisema kwa mkoa wa Geita utekelezaji wake umefanika katika
Vijiji vya Halmashauri za Bukombe na Mbongwe huku mkoa wa Shinyanga
ukitekelezwa katika Halmashauri za Msalala na Kahama.
Alisema
katika kipindi cha miaka miwili, mradi huo umesaidia kuongeza idadi ya watoto
waliofikiwa na huduma ya chanjo kutoka asilimia 93 hadi asilimia 98, kiwango
cha upungufu wa chanjo katika Vituo vya Afya kimeshuka kutoka asilimia 78 hadi
asilimia 28 huku usahihi wa taarifa za chanjo ukiongezeka kutoka asilimia 78
hadi asilimia 93.
Alisema
mradi huo unafadhiliwa na shirika la Human Development Innovation Fund (HDIF) pamoja na
GloxSmithKline (GSK) ukilenga pia kuboresha ukusanyaji na utoaji wa taarifa za chanjo kwa njia ya
kielektroniki ili kusaidia kupunguza magonjwa na vifo vya watoto chini ya miaka
mitano vinavyoweza kuzuilika.
Naye Mkuu wa
Kitengo cha Afya ya Mama na Mtoto kutoka shirika la Amref Africa nchini
Tanzania, Serafika Mkuwa alisema serikali imekuwa ikitumia mifumo mbalimbali ya
kielektroniki ili kuboresha ukusanyaji na utoaji taarifa sahihi za chanjo hivyo
Amref kwa kuunga juhudi hizo imekuwa ikitekeleza mfumo huo kuanzia ngazi ya
jamii na vituo vya kutolea huduma za
afya kupitia watoa huduma wa ngazi hizo
ili kuhakikisha kila mtoto anafikiwa na huduma ya chanjo.
Kwa upande
wake Naibu Mkuu wa mfuko wa HDIF, Joseph Manirakiza alisema mfumo wa teknolojia
ya kielektroniki unaoruhusu taarifa za chanjo kupatikana kwa njia rahisi
ikiwemo simu na hivyo kusaidia utoaji wa huduma kwani huduma ya chanjo ilikua
chini na kuigharimu serikali pesa nyingi kutibu magonjwa ambayo yanaweza
kuzuilika kupitia chanjo.
Afisa Afya
kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto kupitia
Mpango wa Taifa wa Chanjo, Bonaventura Nestory alishauri mfumo wa utekelezaji
wa mradi huo kuendelea kuimarishwa ili kusaidia upatikanaji wa huduma bora za
chanjo nchini kwani serikali imekuwa ikigharamia huduma ya chanjo hivyo ni
vyema ikawafikia wahitaji wengi.
Mganga
mkoani Geita Dkkt. Japhet Simeo alikiri kwamba mradi huo umesaidia kuibua
changamoto ambazo zitasaidia kuboresha upatikanaji wa huduma bora za chanjo katika
maeneo mbalimbali nchini.
Mratibu wa chanjo
halmashauri ya Kahama Mjini, Mukola Phelecian alitoa shukurani kwa shirika la Amref
kwa kuleta mradi huo akisema umesaidia kutunza dawa za chanjo kwa usahihi
katika majokofu pamoja na watoto
kuzipata kwa wakati huku mratibu wa shughuli za chanjo wilayani Msalala,
Deogratias Bwire akisema ili mradi huo uwafikie watoto wengi zaidi ni vyema
watoa huduma ngazi ya jamii wakawezeshwa usafiri na kujengewa uelewa wa kutosha
ili wasaidie kutoa hamasa kwa wananchi kuwasajili na kuwapeleka kliniki kwa
wakati watoto wao.
No comments: