Dkt. Tizeba aagiza wataalamu wa Tume ya Umwagiliaji kuzuru mkoani Iringa
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Waziri wa Kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba akikagua mfereji wa maji wa Mkombozi na Mboliboli Tarafa ya Pawaga Mkoani Iringa kwa ajili ya umwagiliaji wa mashamba ya mpunga katika ziara ya kikazi ya kukagua hali ya upatikanaji wa mbolea katika mikoa ya Nyanda za juu kusini.
Waziri wa Kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba akikagua mashamba ya mpunga alipotembelea Tarafa ya Pawaga Mkoani Iringa.
Waziri wa kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba akiteta jambo na Mkuu wa Wilaya ya Iringa Mhe Richard Kasesela.
Na Mathias Canal-WK,
Iringa
Waziri wa Kilimo Mhandisi Dkt Charles Tizeba amewaagiza
wataalamu wa umwagiliaji kuzuru Tarafa ya Pawaga ili kutembelea na kukagua
mfereji wa maji wa Mkombozi na Mboliboli Tarafa ya Pawaga ili kuanzisha skimu
ya umwagiliaji.
Waziri Tizeba alitoa agizo hilo juzi wakati alipotembela
eneo la mashamba ya mpunga wakati akiwa katika ziara ya kikazi ya siku mbili
Mkoani Iringa ya kukagua hali ya upatikanaji wa mbolea katika mikoa ya Nyanda
za juu kusini.
Alisema kuwa mfereji huo unaohudumia wakulima wa mpunga
katika vijiji vya mboliboli, Usolanga, Mbugani na Mkumbwani unapaswa kuwekewa
mkakati wa haraka ili kujengwa skimu ya umwagiliaji kwa ajili ya mashamba ya
wakulima yanayotajwa kuwa na ukubwa wa hekari 11,000.
"Kwa bahati nzuri Tume ya umwagiliaji sasa rasmi
imehamishiwa kwangu haina hata siku tano nitawasimamia kweli kweli ili kuwa na
matokeo makubwa na ya haraka kwenye kilimo ambacho ndicho mkombozi wa
mkulima" Alikaririwa Dkt Tizeba.
Aidha, aliwashauri wakulima katika Tarafa hiyo ya Pawaga
kuingia katika kilimo cha pamoja ili pindi wanapovuna waweza kuuza kwa pamoja
jambo litakalowafanya kuwa na maamuzi ya kupanga bei waitakayo ya Mazao.
Waziri Tizeba ameitaka Tume ya umwagiliaji kufanya uhakiki
wa maeneo yote ya mashamba hayo ya wakulima kwa kuyapima kabla ya kuingia
katika kilimo cha pamoja ikiwa ni pamoja na kuainisha gharama za ukamilifu wa
mfereji huo wa Mkombozi na Mboliboli.
Alisema kuwa faida ya kulima kwa pamoja wakulima wanapata
fursa ya kukopeshwa kirahisi na Mabenki kuliko kufanya kuomba mkopo kwa mkulima
mmoja mmoja kwani masharti yake yanakuwa magumu zaidi.
Kadhalika, Waziri Tizeba amemuagiza Mshauri wa Kilimo wa
Mkoa wa Iringa Bi Grace Macha kuanisha uhitaji wa mbegu katika Mkoa huo ili
taarifa zitolewe haraka kwa Wakala wa Taifa wa Mbegu (ASA) ili waweze kutoa
mbegu punde msimu unapoanza.
No comments: