“Serikali haitamwonea aibu asiyelipa kodi ya madini”- Nyongo
Wasiliana na BMG kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma za Habari na Mangazo.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo akizungumza na
wachimbaji wadogo wa madini katika machimbo ya Reef D, yaliyopo katika kata ya
Magamba mkoani Katavi ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika mkoa huo yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini, kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa
madini.
Sehemu ya wachimbaji wadogo wa madini kutoka machimbo ya
Reef D, yaliyopo katika kata ya Magamba mkoani Katavi wakifuatilia ufafanuzi
uliokuwa unatolewa na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo kwenye mkutano wa hadhara.
Mmoja
wa wachimbaji wadogo wa madini katika machimbo ya Reef D, yaliyopo katika kata
ya Magamba mkoani Katavi akiwasilisha kero yake mbele ya Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo
Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (katikati)
akioneshwa mchoro wa ramani ya jengo linalojengwa la Ofisi ya Afisa Madini
Mkazi wa Mkoa wa Katavi na Mhandisi
Andrew Mpangalala kutoka SUMA JKT (wa kwanza kulia) ambao ndio wajenzi wa
jengo hilo katika eneo la Msasani mjini Mpanda mkoani Katavi.
Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo (katikati) akiwa
katika picha ya pamoja na watumishi wa Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa
Katavi mara baada ya kufanya nao kikao kilicholenga kujadili utendaji kazi.
Na Greyson Mwase
Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo amesema kuwa
Serikali kupitia Wizara ya Madini haitamwonea aibu mchimbaji yeyote wa madini
atakayekwepa kulipa kodi Serikalini kwa kuwa ni kinyume na Sheria ya
Madini pamoja na kanuni zake.
Aliyasema hayo jana katika mkutano wake na wachimbaji
wadogo wa madini wanaoendesha shughuli zao katika machimbo ya Reef D, yaliyopo
katika kata ya Magamba mkoani Katavi ikiwa ni sehemu ya ziara yake katika
mkoa huo yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini,
kusikiliza na kutatua kero za wachimbaji wa madini.
Katika ziara yake Nyongo aliambatana na Mkuu wa Wilaya ya
Tanganyika, Salehe Mhando, Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa
Madini Mkoa wa Katavi (KATAREMA), William Mbongo, Kaimu Afisa Madini Mkazi wa
Mkoa wa Katavi, Mhandisi Giliard Luyoka, Wataalam wa Madini, Vyombo vya Ulinzi
na Usalama pamoja na waandishi wa habari.
Alisema kuwa, kumekuwa na tabia ya baadhi ya wachimbaji
wadogo wa madini wasio waaminifu wanaokwepa kulipa kodi serikalini hali
inayokwamisha upatikanaji wa huduma nyingine muhimu katika jamii kama
vile elimu, maji, barabara.
“Mchimbaji ambaye anakwepa kulipa kodi mbalimbali kama
Sheria ya Madini na kanuni zake inavyofafanua ni adui namba moja katika ukuaji
wa maendeleo ya nchi, hivyo sisi kama Wizara ya Madini tumejipanga kuchukua
hatua za kisheria nia ikiwa ni kutaka kila mwananchi anufaike na rasilimali za
madini kupitia uboreshaji wa huduma mbalimbali,”alisema Nyongo.
Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Nyongo aliwataka maafisa
madini wakazi katika mikoa yote kuwa wabunifu kwenye ukusanyaji wa maduhuli
kwani Sekta ya Madini inatarajiwa mno kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi.
Aliendelea kusema kuwa, Serikali inaamini kuwa iwapo Sekta
ya Madini itasimamiwa kikamilifu, inaweza kuleta mabadiliko makubwa
kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi kupitia uimarishaji wa sekta nyingine
muhimu.
Aidha, aliwataka maafisa madini nchini kushirikiana na
vyombo vya ulinzi na usalama katika wilaya kwenye zoezi la ukaguzi wa shughuli
za madini ili kuongeza tija kwenye ukaguzi.
Katika mkutano huo mbali na wachimbaji wadogo kumpongeza kwa
kazi kubwa anayofanya ya kusikiliza na kutatua changamoto kwenye shughuli
za uchimbaji madini katika mkoa wa Katavi, wachimbaji hao waliwasilisha
changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na mahitaji ya mikopo katika shughuli za
utafutaji na uchimbaji wa madini, mafunzo kuhusu sheria ya madini na kanuni
zake, uchimbaji salama na vifaa vya kisasa kwa ajili ya uchimbaji wa madini.
Akizungumza kwa niaba ya wachimbaji wadogo katika eneo hilo,
Imso Masumbuko kutoka kikundi cha Kagera Group alisema kuwa wana uhitaji mkubwa
wa elimu kuhusu uchimbaji wa madini salama pamoja na vifaa vya kisasa ili
waweze kuzalisha na kulipa kodi zaidi Serikalini.
Masumbuko mbali na kuainisha changamoto hizo aliiomba Wizara
ya Madini kuiomba Wizara ya Nishati ili iweze kufikisha umeme katika machimbo
hayo kupitia Mradi wa Usambazaji wa Umeme Vijijini unaosimamiwa na Wakala
wa Nishati Vijijini Awamu ya Tatu (REA III).
Alifafanua kuwa, kutokana na ukosefu wa nishati ya umeme
katika eneo lao wamekuwa wakitumia gharama kubwa kwenye uzalishaji wa madini
kutokana na matumizi ya dizeli hivyo kupata faida kidogo sana.
Naye Karusum Daudi ambaye ni mchimbaji wa madini ya dhahabu
katika eneo hilo aliiomba Serikali kupitia Wizara ya Madini iangalie uwezekano
wa kuwapatia mikopo ili waweze kuchimba kwa kutumia vifaa vya kisasa.
Katika hatua nyingine Naibu Waziri Nyongo alifanya ziara
katika Ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Katavi na kusikiliza kero
mbalimbali za watumishi ikiwa ni pamoja na kuzitatua.
Pia Naibu Waziri Nyongo alikutana na wachimbaji wadogo wa
madini mjini Mpanda lengo likiwa ni kusikiliza na kutatua changamoto mbalimbali
zinazowakabili kwenye shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini.
Mbali na kuwasilisha changamoto mbalimbali zilizotatuliwa na
Naibu Waziri Nyongo papo hapo wachimbaji wadogo wa madini walimpongeza
Naibu Waziri Nyongo na kumwomba kuendelea na ari ya kusikiliza kero zao na
kuzitatua.
Akizungumza katika kikao hicho, Nyongo alisema Wizara ya
Madini haitachoka kutatua changamoto zinazowakabili wachimbaji wa madini nchini
kwa kuwa inataka wachimbe katika mazingira mazuri na kulipa kodi Serikalini.
No comments: