LIVE STREAM ADS

Header Ads

Biteko atatua kero za wachimbaji wadogo katika Wilaya ya mbogwe mkoani Geita

Wasiliana na BMG Blog/ BMG Online TV kupitia 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com kwa huduma ya Habari na Matangazo.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita, Daniel Mapunda (kushoto) akibadilishana mawazo na Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Geita, Christopher Kadeo (kulia) kabla ya kuanza kwa ziara ya Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko kwenye machimbo ya dhahabu ya wachimbaji wadogo yaliyopo wilayani Mbogwe mkoani Geita. Katikati ni Mkaguzi wa Migodi kutoka Tume ya Madini Mhandisi Frederick Mwanjisi.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) akikagua nyaraka katika mgodi wa kuchenjua dhahabu unaomilikiwa na kikundi cha Isanja Badugu, uliopo Wilayani Mbogwe mkoani Geita.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto mbele) pamoja na msafara wake akiendelea na ziara katika mgodi wa kuchenjua dhahabu unaomilikiwa na kampuni ya Magimi Gold Partners uliopo wilayani Mbogwe mkoani Geita.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (kushoto) akitoa maelekezo kwa mkurugenzi  wa mgodi wa kuchenjua dhahabu unaomilikiwa na kampuni ya Magimi Gold Partners, Juma Galehe (hayupo pichani). Wengine kutoka kulia ni  Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita, Daniel Mapunda na Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe, Martha Mkupasi.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) akimsikiliza mmoja wa wachimbaji wa madini ya dhahabu katika machimbo ya Nyakafulu yaliyopo wilayani Mbogwe mkoani Geita.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko (katikati) akisalimiana na mmoja wa wachimbaji wadogo kwenye machimbo ya Nyakafulu yaliyopo wilayani Mbogwe mkoani Geita.
Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko akizungumza na sehemu ya wachimbaji wadogo wanaojishughulisha na uchimbaji wa madini ya dhahabu katika machimbo ya Nyakafulu yaliyopo wilayani Mbogwe mkoani Geita.


Greyson Mwase
Leo tarehe 26 Novemba, 2018 Naibu Waziri wa Madini, Doto Biteko amefanya ziara katika machimbo ya dhahabu ya wachimbaji wadogo yaliyopo wilayani Mbogwe mkoani Geita lengo likiwa ni kukagua shughuli za uchimbaji madini, kusikiliza na kutatua kero mbalimbali zinazowakabili wachimbaji wadogo. Katika ziara hiyo Naibu Waziri Biteko aliambatana na Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe, Martha Mkupasi, Mbunge wa Jimbo la Mbogwe, Augustino Masele, Katibu Tawala wa Wilaya ya Mbogwe, Christopher Bahali, na Mwenyekiti wa Chama cha Wachimbaji wa Madini Mkoa wa Geita, Christopher Kadeo.

Wengine ni pamoja na Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita, Daniel Mapunda, Mkaguzi wa Migodi kutoka Tume ya Madini Mhandisi Frederick Mwanjisi, Wataalam kutoka Wizara ya Madini na Tume ya Madini, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mbogwe pamoja na waandishi wa habari.

Mara baada ya kukamilisha ziara yake katika migodi ya kuchenjua dhahabu ya Isanja Badugu, na Magimi Gold Partners iliyopo katika eneo la Buluhe wilayani Mbogwe mkoani Geita, Naibu Waziri Biteko alielekeza migodi husika kuhakikisha inahifadhi nyaraka zote mgodini kama sheria ya madini inavyotaka.

Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Biteko alifanya ziara katika mgodi wa dhahabu wa Nyakafulu uliopo Wilayani Mbogwe Mkoani Geita unaomilikiwa na kikundi cha Isanja Badugu na kufanya mkutano wa hadhara ulioshirikisha wachimbaji wadogo wa madini wanaoendesha shughuli za uchimbaji madini katika eneo la mgodi huo na kutatua kero zao hapo hapo.

Mara baada ya kusikiliza na kutatua kero mbalimbali zilizowasilishwa na wachimbaji wadogo hao, Naibu Waziri Biteko alitoa maelekezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama vya Wilaya na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuhakikisha inafanya uchunguzi dhidi wizi uliofanywa na mmoja wa viongozi wa kikundi cha Isanja Badugu na kuchukua hatua za kisheria, wachimbaji wadogo kuhakikisha wanalipa kodi za madini Serikalini, wamiliki wa machimbo kuhakikisha hawawanyanyasi wachimbaji wadogo na kufanya nao kazi kwa mikataba na wamiliki wa machimbo kuhakikisha hawatoi rushwa.

Kero zilizowasilishwa na wachimbaji wadogo hao awali ni pamoja na baadhi ya wachimbaji wa madini kufanya kazi pasipokuwa na mikataba rasmi, ukosefu wa nishati ya umeme kwa ajili ya kuendeshea mitambo na baadhi ya wachimbaji wadogo kutokulipwa mara baada ya kusimamishwa kazi.

No comments:

Powered by Blogger.