LIVE STREAM ADS

Header Ads

Benki ya Stabic yatoa Bima za Afya kwa watoto Jijini Mwanza

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Judith Ferdinand, BMG
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ametoa wito kwa jamii kuwa na utaratibu wa kuchangiana kwenye matibabu hususani bima ya afya.

Mwalimu ametoa wito huo leo mkoani Mwanza wakati akiwakabidhi kadi ya bima za afya watoto 105 zilizotolewa na benki ya Stanbic na kuongeza kwamba watanzania wamekuwa na utaratibu wa kuchangiana kwenye misiba tu hivyo wabadilike na kuchangiana pia katika matibabu hususani ya mtu kupata bima ya afya ambayo inasaidia jamii kupata huduma ya afya wakati wote.

Ametumia fursa hiyo kuipongeza benki ya Stanbic kwa kutoa bima kwa watoto hao kwani wamekuwa ni moja ya wadau ambao wameunga juhudi za Serikali za kuhakikisha jamii inapata huduma ya matibabu bila gharama na kwa wakati, kwani changamoto iliyopo ni wananchi kutokupata huduma hiyo kutokana na kukosa fedha.

Pia aMEsema Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015/20 inaitaka Serikali kuweka mfumo wa wananchi kupata matibabu kwa urahisi hivyo imeamua kuja na mfumo wa bima na kila mwananchi anapaswa kuwa nayo ambapo mpaka sasa wameisha anza mchakato wa sheria ambayo itakuwa tayari kabla ya mwezi Semptemba mwaka huu.

"Bima ya afya inasaidia kupata huduma nzuri ya matibabu hivyo tutaweka utaratibu ambao ni sheria wa kila mwananchi kuwa na bima, ambapo kwa mtoto ni shilingi 50,400 kwa mwaka ambapo atapata matibabu katika hospitali zote ndani ya nchi na atahudumiwa hata kama gharama za matibabu ni kubwa". Amesema Mwalimu na kuongeza

"Pia tumeboresha bima ya CHF ambayo gharama yake ni 30,000 kwa mwaka ambapo watu sita watahudumiwa katika Vituo vya Afya vya serikali ndani ya mkoa husika, na katika kuunga mkono juhudi za Stanbic nitawalipia watoto wanane bima ikiwa wanne kutoka wilaya ya Ilemela na wanne Nyamagana huku pia Mbunge wa Jimbo la Nyamagana atawalipia watoto wanne". Amesema Mwalimu.

Kwa upande wake Meneja wa Benki ya Stanbic tawi la Mwanza,  Alphonce Mokok amesema katika kuhakikisha uchumi unakua na maendeleo ya taifa, wanaamini kuwekeza katika sekta ya afya ambapo wameamua kuchangia watoto hao 105 katika bima ya afya ili iwe rahisi kupata matibabu.

Meneja Miradi wa Cheka Sana Tanzania,  Catherine Mongella ameshukuru benki hiyo kwa kuwasaidia watoto bima ya afya ambayo itarahisisha upatikanaji wa matibabu ambapo kituo chao kina uwezo wa kulea watoto 35 ambapo kwa mwaka wanatumia milioni 14 kwa ajili ya huduma za afya.

Hata hivyo Mkuu wa Wilaya Nyamagana, Dkt. Philis Nyimbi akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mwanza,  John Mongela amesema watoto 253 kati ya 726 wanaoishi katika makao ya kulelea watoto wamepatiwa bima za afya ambapo wanapata matibabu katika Vituo mbalimbali vya Afya mkoani Mwanza hivyo ameishukuru benki hiyo kwa kujitolea bima kwa watoto hao.
#PamojaDaimaBMG

No comments:

Powered by Blogger.