LIVE STREAM ADS

Header Ads

Waziri Biteko afungua mkutano wa nchi za Maziwa Makuu

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com

Waziri wa Madini, Doto Biteko amefungua mkutano wa kimataaifa wa nchi wanachama wa Maziwa Makuu hii leo katika Hotel ya Morena Jijini Dodoma.
Waziri Doto Biteko akizungumza kwenye ufunguzi huo.
Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo akizungumza kwenye mkutano huo.
Picha ya pamoja.

Na Issa Mtuwa, Dodoma
Nchi wanachama wa Maziwa Makuu zimetakiwa kushikamana kuunganisha nguvu katika kulinda na kusimamia matumizi ya raslimali ardhi ikiwemo madini ili kunufaisha nchi hizo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Madini, Doto Biteko wakati akifungua mkutano wa Kimataifa wa nchi wanachama wa Maziwa Makuu (International Conference on the Great Lakes Region - ICGLR) unaofanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe 11-12 Machi 2019 katika Hotel ya Morena jijini Dodoma.

Biteko amezitaka nchi hizo kuunganisha nguvu ya pamoja katika kudhibiti raslimali ardhi ikiwemo madini na kujiwekea utaratibu utakao dhibiti shughuli za uzalishaji na biashara ya madini ili raslimali hizo zinufaishe mataifa yao na zisitumike vibaya.

"Unganisheni nguvu kwa pamoja, wekeni utaratibu utakao wafanya nchi wanachama kunufaika na raslimali ardhi/madini. Jitahidini kuhakikisha raslimali hizo hazitumiki vibaya kama ilivyo kubaliwa kwenye itifaki, hivyo lazima kuwe na utaratibu na sheria kwa kila nchi namna ya kudhibiti uzalishaji na biashara ya madini". Amesema Biteko.

Naye Mtaalam kutoka Wizara ya Madini, Mhandisi Assah Mwakilembe amesema Mkutano huo unalenga kujadili na kupitia mfumo wa udhibitisho wa mnyororo wa madini kwa lengo la kudhibiti uzalishaji na biashara ya madini katika nchi za maziwa makuu kufuatia kuwepo tetesi zilizo kuwa zinahusisha raslimali ardhi (Madini) na ufadhili wa vita katika nchi za aaziwa makuu. (Region Certification Manual)

Akizungumza mara baada ya kuwasilisha mada kuhusu marekebisho ya Sheria Madini ya Mwaka 2017 Mkurugenzi wa Idara ya Sheria kutoka Wizara ya Madini, Edwin Igenge amesema kwa upande wa Tanzania, imetekeleza itifaki ya pamoja ya nchi wanachama wa Maziwa Makuu kama ilivyo kubaliwa.

Ameongeza kuwa, utekelezaji wa itifaki kwa Tanzania ni pamoja na marekebisho ya sheria ya Madini ya Mwaka 2017 yaliyopelekea kuundwa kwa Tume ya Madini ambapo shuguli zote za usimamizi wa raslimali madini zimepewa Tume ya Madini ambapo kabla ya hapo shuguli hizo zilikuwa chini ya Kamishna wa Madini.

Igenge amesema kuanzishwa kwa itifaki katika nchi za maziwa makuu kulitokana na tetesi za uwepo wa matumizi mabaya ya raslimali ardhi ikiwemo madini ambapo kipato cha raslimali hizo inasadikika kuwa zilikuwa zinatumika kufadhili shuguli za za kivita katika nchi za maziwa makuu, hivyo kupelekea kuanzishwa kwa itifaki ya pamoja kwa lengo la kudhibiti.

Mkutano huo wa kimataaifa unahudhuriwa na wajumbe kutoka Tanzania, Burundi, Rwanda na wawakilishi wa Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ) na Sekretariati ya nchi wanachama wa Maziwa Makuu. Kwa upande wa Tanzania inawakilishwa na Wizara ya Madini, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Shirikisho la Wachimbaji Tanzania (FEMATA), Chama cha Wanunuzi na Wauzaji wa Madini Tanzania (TAMIDA), Tume ya Madini, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), Wakala wa Jiolojia na Utafiti wa Madini (GST).

Katika mkutano huo, Waziri Biteko aliambatana na Naibu Waziri wa Madini Stanslaus Nyongo, Kamishna wa Madini Mhandisi Daivid Mulabwa, Mkurugenzi wa Sheria kutoka Wizara ya Madini Edwin Igenge na baadhi ya maafisa kutoka wizara ya Madini.

No comments:

Powered by Blogger.