LIVE STREAM ADS

Header Ads

Wadau wa habari waomba kukutana na Tume ya Taifa ya Uchaguzi NEC

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Wadau wa habari kutoka taasisi na vyombo mbalimbali vya habari nchini wameomba kukutana na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), ili kuimarisha mahusiano mema wakati ambao taifa linaelekea kwenye uchaguzi mdogo mwaka huu pamoja na uchaguzi mkuu hapo mwakani.

Pamoja na mambo mengine, wadau hao waliazimia hilo juzi kwenye warsha ya kuwajengea uwezo viongozi wa vyombo vya habari ili kuangalia na kuripoti kwa weledi habari za uchaguzi, iliyofanyika jijini Dodoma kwa siku tatu kuanzia Aprili 15, 2019 ikiandaliwa na taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (MISA) tawi la Tanzania kwa kushirikiana na Ubalozi wa Marekani.

Akisisitiza hilo, Mkurugenzi wa Mawasiliano kutoka taasisi ya Internews, Wenceslaus Mushi alisema wadau wa habari pamoja na maafisa kutoka NEC ni vyema wakakutana kwenye warsha ya pamoja na kujengeana weledi namna kila upande unaweza kutimiza majukumu yake kwa mujibu wa sheria katika kipindi cha uchaguzi na hivyo kuondoa mkanganyiko ambao wakati mwingine hujitokeza ikiwemo waandishi wa habari kuzuiliwa kuingia kwenye vyumba vya kupigia kura.

Mkurugenzi wa taasisi ya MISA Tanzania, Sengiyumva Gasirigwa alisema juhudi zitaendelea kufanyika ili kuwakutanisha wadau wa habari pamoja na wasimamizi wa uchaguzi ili kuimarisha mahusiano hatua itakayosaidia kila upande kutimiza vyema majukumu yake na hivyo kuwa na uchaguzi wa amani.
Mkurugenzi wa Mawasiliano kutoka taasisi ya Internews, Wenceslaus Mushi akizungumza kwenye warsha hiyo.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (MISA) tawi la Tanzania, Sengiyumva Gasirigwa akifuatilia kwa umakini majadiliano kwenye warsha hiyo.
Mkuu wa Idhaa ya Kiswahuli ya Sauti ya Amerika (V.O.A), Dkt. Mwamoyo Hamza akiwasilisha mada kuhusu aina ya maswali waandishi wa habari wanapaswa kuwauliza wagombea wakati wa uchaguzi. Alisema waandishi wa habari wanapaswa kuuliza maswali yanayojibu mahitaji ya wananchi na kuwasaidia kufanya maamuzi sahihi ya kuwachagua viongozi wanaowataka.
Mshauri wa masuala ya Habari kutoka TMF, Dastan Kamanzi akiwasilisha mada kwenye warsha hiyo, akisisitiza waandishi wa habari kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi/ kuleta mabadiliko chanya katika jamii.
Mkurugenzi wa taasisi ya "Tangible Initiatives For Local Development Tanzania",  Geline Fuko akiwasilisha mada kwenye warsha hiyo ambapo alisisitiza vyombo vya habari kutoa fursa sawa kwa wanawake na makundi maalumu ikiwemo watu wenye ulemavu katika kuripoti habari za uchaguzi.
Mtaalamu wa masuala ya Mitandao ya Kijamii, Innocent Munggy akiwasilisha mada kuhusu matumizi sahihi ya mitandao hiyo hususani wakati wa uchaguzi ambapo alihimiza taasisi mbalimbali ikiwemo MISA Tanzania kutoa tuzo kwa watumiaji wa mitandao ya kijamii ili kuhamasisha matumizi sahihi.
Mhariri kutoka kampuni ya Mwananchi Communication, Bakari Machumu akichangia mada kwenye warsha hiyo.
Baadhi ya watendaji kutoka MISA Tanzania wakiwa kwenye warsha hiyo.
Baadhi ya washiriki wa warsha hiyo.

No comments:

Powered by Blogger.