LIVE STREAM ADS

Header Ads

Shirika la WFT latambulisha mradi wake mkoani Shinyanga

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Shirika lisilo la kiserikali la Women Fund Tanzania (WFT) linalofanya shughuli za utetezi wa haki za wanawake na ujenzi wa tapo ya wanawake Tanzania lenye makao yake jijini Dar es salaam limetambulisha rasmi Mradi wa Kuwezesha Utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Kuzuia Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga. 

Mradi huo wa “Support for the implementation Fund for National Plan of Action to End Violence Against Women and Children” umezinduliwa na kutambulishwa rasmi leo Alhamis Mei 30,2019 wakati wa Kikao cha Wadau wa Haki za Wanawake na Watoto na upingaji wa ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto wilaya ya Shinyanga kilichofanyika katika Ukumbi wa Karena Hoteli Mjini Shinyanga.

Akizindua Mradi huo,Katibu Tawala Wilaya ya Shinyanga,Boniface Chambi kwa niaba ya Mkuu wa wilaya hiyo,alisema mradi huo utasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

“Tunawashukuru sana Women Fund Tanzania kwa kutuletea mradi huu katika halmashauri yetu,ninachoweza kusema huu ni mfuko wezeshi kwa jamii,sisi kama serikali tutatoa ushirikiano,kinachotakiwa sasa ni kuwa na mawasiliano kati ya Women Fund Tanzania na wadau watakaowezeshwa/ watakaopata ruzuku,toeni taarifa serikalini”,alisema Chambi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Progamu kutoka Women Fund Tanzania, Carol Francis Mango alisema mradi huo utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu kama majaribio katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.

“Tumeichagua halmashauri hii iwe ya mfano kwa sababu kuna matukio mengi ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto,ili kufanikisha mradi huu tutatoa ruzuku kwa mashirika ya wanawake na wasichana kwa ajili ya utekelezaji wa mikakati mbalimbali ya ukombozi wa mwanamke na msichana”,alieleza Mango.


“Miongoni mwa Watekelezaji wa mpango wa kitaifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto na ambao ndio walengwa wa mradi huo ni Halmashauri,Mashirika,taasisi na asasi zisizo za kiserikali ‘NGOs’,mabaraza ya watoto na jamii kwa ujumla”,aliongeza.

Aidha alisema lengo la WFT ni kuchangia harakati za kutetea haki za wanawake,kuwawezesha na kuendeleza mikakati ya ujenzi wa vuguvugu la utetezi wa nguvu za pamoja ili kukuza haki na usawa wa wanawake kimapinduzi nchini.

“Sisi ni mfuko wa kwanza na pekee unaolenga kutoa ruzuku kwa ajili ya kuendeza shughuli za utetezi wa haki za wanawake hususani waliopo kwenye ngazi ya jamii.Tunataka kuchangia katika kujenga tapo la wanawake imara nchini Tanzania kwa kufadhili na kuimarisha uwezo wa wanawake kwa njia ya kuendeleza mikakati ya kuunganisha nguvu za pamoja na kutafuta rasilimali”,aliongeza.

Aidha alisema shirika hilo liko mbioni kufungua ofisi mkoani Shinyanga ili kurahisisha uratibu wa shughuli za mradi huo mkoani Shinyanga.
Katibu Tawala Wilaya ya Shinyanga, Boniface Chambi akitambulisha na kuzindua Mradi wa Kusaidia Utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Kuzuia Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga unaotekelezwa na Shirika la Kijamii la Women Fund Tanzania. Kushoto ni Mkuu wa Progamu kutoka Women Fund Tanzania,Carol Francis Mango,kulia ni Kaimu Mkurugenzi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga,Deus Mhoja.
Sehemu ya Wadau wa Haki za Wanawake na Watoto wilaya ya Shinyanga wakiwa katika Ukumbi wa Karena Hoteli Mjini Shinyanga.
Mkuu wa Progamu kutoka Women Fund Tanzania,Carol Francis Mango akitoa wasilisho la Mradi wa Kusaidia Utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Kuzuia Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa Progamu kutoka Women Fund Tanzania,Carol Francis Mango akielezea kuhusu Mradi wa Kusaidia Utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Kuzuia Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Wadau wakimsikiliza Mkuu wa Progamu kutoka Women Fund Tanzania,Carol Francis Mango.
Mratibu wa Mradi wa Kusaidia Utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Kuzuia Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto mkoa wa Shinyanga, Glory Mbia akielezea malengo ya kikao cha wadau wa haki za wanawake na watoto.
Wadau wakiwa ukumbini.
Wadau wakifuatilia matukio ukumbini.
Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga,Ngasa Mboje akilishukuru shirika la Women Fund Tanzania kupeleka mradi katika halmashauri yao na kuahidi kutoa ushirikiano wakati wa utekelezaji wa mradi.
Mganga Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Dkt. Rashid Mfaume akitoa neno la shukrani kwa Women Fund Tanzania na kueleza kuwa uongozi wa mkoa wa Shinyanga umepokea mradi huo na wapo tayari kutoa ushirikiano wote kufanikisha malengo ya mradi huo unaolenga kuwakomboa wanawake na watoto.
Kaimu Mkurugenzi halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Deus Mhoja akiwahamasisha wadau wa haki za wanawake na watoto kuchangamkia fursa ili kuhakikisha jamii inaondokana na mambo maovu.
Picha ya pamoja baada ya uzinduzi wa Mradi wa Kusaidia Utekelezaji wa Mpango wa Kitaifa wa Kuzuia Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto.
Imeandaliwa na Kadama Malunde - Malunde1 blog

No comments:

Powered by Blogger.