LIVE STREAM ADS

Header Ads

LHRC yazindua ripoti ya haki za binadamu tanzania 2019

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga (katikati) akikata utepe kama ishara ya uzinduzi wa Ripoti ya Haki za Binadamu Tanzania 2019. Uzinduzi huo uliofanyika leo Aprili 29, 2020 katika ofisi za LHRC jijini Dar es Salaam na wadau kufuatilia kwa njia ya mtandao. 
Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga (katikati), Afisa Utafiti, Fundikila Wazambi (kushoto) na Mkurugenzi wa Uwajibikaji na Uwezeshaji wa Kituo hicho, Felista Mauya (kulia) wakionesha nakala za Ripoti ya Haki za Binadamu Tanzania 2019 mara baada ya uzinduzi leo Jumatano leo Aprili 29, 2020 katika ofisi za LHRC jijini Dar es Salaam na wadau kufuatilia kwa njia ya mtandao. 

Na Kadama Malunde, Malunde 1 Blog
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimezindua Ripoti ya Haki za Binadamu Tanzania 2019 inayoangazia hali ya haki za binadamu kwa mwaka 2019 na kufanya ulinganisho wa hali ilivyokuwa mwaka 2018. 

Uzinduzi huo umefanyika leo Jumatano, Aprili 29, 2020 kwa njia ya mtandao kufuatia mlipuko wa virusi vya Corona. 

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC amesema ripoti hiyo inahusisha matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu sambamba na mapendekezo kwa ajili ya uboreshaji wa sera, sheria na utendaji katika jamii. 

Anna amesema ripoti hiyo inaangazia hali ya haki za binadamu katika nyanja za haki za kiraia na kisiasa; haki za kiuchumi, kijamii na kiutamaduni; haki za makundi yaliyo hatarini; mifumo ya Ulinzi wa Haki za binadamu na haki za kijumla. 

“Ripoti hii ni matokeo ya taarifa mbalimbali zilizokusanywa na LHRC ikiwemo taarifa kutoka kwa waangalizi wa haki za binadamu walio nchi nzima, wasaidizi wa kisheria walio katika wilaya mbalimbali, taarifa rasmi toka taasisi za Serikali, Bunge, Mahakama, jeshi la polisi, vyombo vya habari na asasi mbalimbali za kiraia zisizo za Serikali. Taarifa hii pia hutumia taarifa mbalimbali za kitaifa lakini pia na za kimataifa, hasa zinazolenga kuelezea hali ya haki za binadamu nchini”, amesema Anna Henga. 

Kwa mujibu wa Ripoti hiyo, haki tano zilizokiukwa zaidi kwa mwaka 2019 ni pamoja na: 

Haki ya Kuishi ambapo matukio kama vile mauaji ya wanawake, mauaji ya watoto, mauaji yanayotokana na kujichukulia sheria mkononi, mauaji yanayotokana na imani za kishirikina pia yameendelea kuripotiwa. 

Uhuru dhidi ya ukatili; ambapo matukio yaliyoripotiwa ni Ukatili wa kingono na kimwili dhidi ya watoto; ukatili wa kingono na kimwili dhidi ya wanawake. Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2017 hadi mwezi Juni 2019, jumla ya matukio 88,612 ya ukatili wa kijinsia yameripotiwa. Matukio ya ukatili wa kingono dhidi ya watoto jumla ya matukio 3,709 ya ubakaji yaliripotiwa katika vituo vya polisi nchini ikiwa ni matukio 126 zaidi ya yale yaliyoripotiwa katika kipindi kama hicho mwaka 2018. ukatili dhidi ya watu wenye ulemavu na wazee nao umeendelea kushika kasi katika tukio moja, bibi wa miaka aliripotiwa kubakwa hadi kufariki. 

Uhuru wa Kujieleza; muendelezo wa uminywaji wa uhuru wa kujieleza ambapo kumekuwepo na Sheria kandamizi, ukamataji na uwekaji kizuizini waandishi wa habari kinyume na sheria pamoja na kufungiwa kwa vyombo vya habari. 

Haki ya kuwa Huru na Salama; Ripoti imeripoti matukio kadhaa yanayopelekea kuminywa kwa haki hiyo kama vile Mashambulizi na mauaji ya madereva bodaboda pamoja na Matukio ya utekaji, watu waliopotea na matukio ya ukamataji na uwekaji kizuizini kinyume na sheria. 

Haki ya Kujumuika na Kukusanyika; zimeendelea kukiukwa hasa kipindi hiki ambapo tunaelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2020. Vyama vya siasa, hususan vya upinzani, viliendelea kulalamikia maamuzi haya kwamba yanakiuka haki yao inayolindwa na Katiba, jambo linaloathiri pia ushindani wao kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020. Vyama hivi pia vililalamika kwamba marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa yanaminya uhuru wao wa kujumuika na kukusanyika. 

LHRC kupitia Mkurugenzi Mtendaji wake, Anna Henga wametoa rai kwa serikali na wanajamii kwa ujumla kuchukua hatua katika kulinda na kudumisha haki za binadamu. 

“Tunatoa rai kwa serikali, taasisi na jamii ya Watanzania kuendelea kulinda haki za binadamu na kuwawajibisha wale ambao wameshindwa kuheshimu haki hizo bila ubaguzi wa kikabila, kidini, kisiasa na kijinsia ili tuweze kuifikia jamii yenye haki na usawa”,amesisitiza Anna Henga. 

Ripoti ya Haki za Binadamu Tanzania 2019 ni muendelezo wa ripoti za kituo hicho zinazotolewa kila mwaka kwa lengo la kuonesha hali na kutoa mapendekezo ya maboresho.

No comments:

Powered by Blogger.