LIVE STREAM ADS

Header Ads

MWANZA “Kalemani aagiza wananchi kuunganishiwa umeme”

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com

 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani amegoma kuwasha umeme katika Kijiji cha Isamilo kilichopo Wilaya Misungwi mkoani Mwanza baada ya kukuta nyumba tatu kati ya 121 katika Kijiji hicho ndizo zimeunganishiwa na nishati hiyo.

Dkt. Kalemani amefikia maamuzi hayo Juni 26, 2020 alipofanya ziara ya kikazi wilayani Misungwi kufuatilia na kukagua utekelezaji wa mradi ya usambazaji umeme vijijini (REA) na kueleza kutoridhishwa na kasi ya mkandarasi aliyepewa kazi hiyo.

Kutokana na hatua hiyo, Dkt. Kalemani aliwaagiza viongozi wa TANESCO Wilaya Misungwi na Mkoa Mwanza kuhakikisha kazi ya kuunganisha nishati ya umeme katika nyumba zilizosalia inaanza kesho Juni 27, 2020 ili baada ya wiki moja arudi kijijini hapo kuwasha rasmi nishati hiyo.

 “Mkandarasi (NIPO GROUP) aliyekuwa anasambaza umeme katika Mkoa Mwanza ameshindwa kazi ambapo wiki iliyopita tumemfuta na kuikabidhi kwa shirika la umeme ETOCO. Tulimpa vijiji 127 lakini ameshindwa kusambaza umeme katika vijiji 70 kwani mkataba wake ulikuwa unaisha Juni 30, 2020” alisema Dkt. Kalemani.

Aidha Dkt. Kalemani alieleza kusikitishwa na hatua ya vijiji 41 kati ya 114 wilayani Misungwi kutojumuishwa kwenye mpango wa kuunganishiwa umeme na kuwatoa hofu wakazi wa vijiji hivyo kwamba watafikishiwa nishati hiyo haraka iwezekanavyo.

Hata hivyo baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Isamilo wilayani Misungwi akiwemo Bi. Restuta Wilbert wameeleza kuwa na matumaini makubwa ya nyumba zao kuunganishiwa umeme baada ya nishati hiyo kufikishwa kijijini hapo.

“Mimi tangu kuzaliwa umeme nilikuwa nauona tu mbali hivyo nashukuru sana kuuona kwenye maeneo yetu na naomba kazi aliyoisema (Dkt. Kalemani) waitekeleze ili tupate umeme” alisisitiza Bi. Restuta.
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
 Waziri wa Nishati, Dkt. Medard Kalemani (kulia) akizungumza na wakazi wa Kijiji cha Isamilo wilayani Misungwi (hawako pichani). Kushoto ni Katibu Tawala Wilaya Misungwi, Petro Sabatto aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya, Juma Sweda.
Tazama BMG ONLINE TV hapa chini

No comments:

Powered by Blogger.