Vyombo vya habari Tanzania vyatakiwa kuwa na mkakati wa kujikwamua kifedha
Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa Binagi Media Group. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama binagimediagroup@gmail.com
Na Ellukagha Kyusa, Mwanza
Waandishi wa Habari Tanzania wameeleza changamoto mbalimbali wanazo kumbana nazo katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku  yanavyo athiriwa  na ukosefu wa Uhuru wa Habari
 Changamoto hizo zilielezwa kwenye mkutano uliofanyika kwa njia ya mtandao Mei 03, 2021 ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Habari Duniani na kuibua changamoto mbalimbali kwa Waandishi wa Habari.
 Muwezeshaji  Getrude John alisema kuwa waandishi wanawekewa vikwazo katika kuifikia jamii moja kwa moja na kuiomba mamlaka husika kufanya marekebisho ya sheria kandamizi katika vyombo vya habari.
 Pia  aliongeza kuwa  waandishi wa habari na  vyombo  vya  habari  vimekumbwa na  uhaba  wa kifedha  hivyo  vinatakiwa  kuwa na mkakati wa  kujijengea  uwezo  wa  kupata  fedha  ili kuwasaidia waajiriwa wao ambao  ni waandishi wa habari  kupata  stahiki zao  ili wafanye  kazi  kwa ufanisi.
 Naye Mwezeshaji Jesse Kwayu ambaye pia ni Mjumbe wa Bodi ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) aliibua  uwepo  wa changamoto  nyingi  kwa  waandishi wa  habari   ikiwemo  suala  la  ukandamizwaji wa  kupata  taarifa kutoka  kwenye  mamlaka  mbalimbali.
 "Kumekuwa  na  sheria  nyingi ambazo  siyo  rafiki   kwenye  tasnia  ya  habari  zinazoleta   hofu  kwa waandishi  kutafuta  taarifa  sahihi  na kuzirusha  kupitia  vyombo  vyao   na hivyo  kujikuta  habari  nyingi  haziifikii  jamii" alisema Kwayu.
 Mratibu wa Mtandao  wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo  Olengurumwa alieleza kuwa waandishi  wa habari wakikosa uhuru wa kutoa taarifa inaathiri jamii kwa kukosa haki ya kupata taarifa na kukosa mahali pa kupaza sauti zao na pia kuongeza kuwa vita dhidi ya kutetea haki za binadamu havitawezekana bila kuwepo vyombo vya habari na kuwasihi waandishi kuungana ili kuijenga tasnia ya habari na kutatua changamoto wanazo kutana nazo.
 Maadhimisho ya mwaka huu ni maadhimisho ya 30 tangu kupitishwa kwa azimio la Windhoek nchini Namibia ambapo Mei 3 kila mwaka vyombo vya habari huadhimisha Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani.
 Kongamano hilo liliandaliwa na Klabu ya Waandishi wa Habari ya Mkoa wa Mwanza kwa kushirikiana na Shirika la kimataifa la Internews na kuhudhuriwa na zaidi ya washiriki 60 kutoka mashirika na taasisi mbalimbali Tanzania.
No comments: