LIVE STREAM ADS

Header Ads

TAMWA yapongeza wanawake kuteuliwa Ofisi ya Mashtaka

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Online Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Chama cha Waandishi wa Wahabari Wanawake Tanzania ofisi ya Zanzibar, (TAMWA ZNZ) kinawapongeza Bi. Salma Ali Hassan Khamis na Bi. Mwanamkaa Abdulrahman Mohammed kwa kuteuliwa kuiongoza Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar.

Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar ina majukumu mengi yakiwemo ya kupokea na kukagua faili zote zinazotoka polisi, kuchambua ushahidi wa upelelezi uliotoka polisi, kupeleka faili za kesi mahakamani, kuendesha kesi Mahakamani kwa kuuwakilisha upande wa Serikali na kukata rufaa iwapo haitaridhika na maamuzi ya Mahakama kuhusiana na shauri lolote

Kupitia uteuzi huo uiliofanywa na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar,Dkt Hussein Ali Mwinyi hivi karibuni, Bi Salma Ali Hassan Khamis ameteuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Afisi hiyo na Bi Mwanamkaa Abdulrahman Mohammed kuwa Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka katika Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar.

Hawa ni viongozi wa kwanza wanawake kuongoza Afisi hiyo katika nafasi hizo kuu kabisa na hivyo kuongeza uwepo wa wanawake katika nafasi za uongozi kwa jumla, hali ambayo inahimizwa kwa maendeleo ya mwanamke na nchi kwa jumla.

TAMWA - ZNZ inaamini kuwa kuwepo kwa viongozi hao, kesi za udhalilishaji na ukatili wa wanawake na watoto zitapata msukumo mpya katika ufuatiliaji na uchunguzi na kwa muda mfupi ili kukomesha kabisa vitendo hivyo vilivyokithiri nchini na ambavyo vinawaathiri zaidi wanawake na watoto.

Kwa mujibu wa takwimu kutoka Afisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali, jumla ya kesi 838 za udhalilishaji ziliripotiwa kuanzia mwezi wa Januari hadi Agosti, 2021 ambapo wanawake walioathirika ni 679 sawa na asilimia 81 na wanaume ni 166 sawa na asilimia 19.8.

Ukatili mwingine ni wanawake na watoto kupigwa kwa mapanga kutokana na sababu zisizokuwa za msingi na kwamba wengi wa wahalifu bado hawajakamatwa. Hivyo, tunashauri Wakurugenzi wa Mashtaka kuandaa utaratibu maalum wa kushirikiana na Jeshi la Polisi ili kurahisisha uchunguzi katika matukio ya aina hii.

TAMWA - ZNZ inawatakia kila la kheri Wakurugenzi hao katika majukumu yao mapya na muhimu na Mwenyezi Mungu awaongeze hekima, busara, ushirikishaji na uadilifu zaidi.

No comments:

Powered by Blogger.