LIVE STREAM ADS

Header Ads

Zaidi ya watoto 3,000 Kongwa warejea Shule

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Online Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Siku chache baada ya baraza la madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma kupitisha azimio la operesheni tokomeza utoro, imeelezwa kuwa watoto 3,628 ambao ni sawa na 98% wamerudi shuleni kuendelea na masomo wakiwemo wa darasa la saba ambao wanajiandaa na mtihani wa Taifa mwaka huu.

Hayo yalibainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Dkt Omary Nkullo wakati wa mkutano wa mwaka wa Halmashauri kwa mwaka wa fedha 2021/2022 uliofanyika Kktika ukumbi wa Halmashauri wilayani humo.

Alisema katika kikao kilichokaa Septemba 08, 2022 cha kupokea taarifa ya robo ya nne ya mwaka, suala la utoro mashuleni lilikuwa ni mojawapo ya ajenda iliyojadiliwa ambapo watoto 3,703 waliripotiwa kutokuwepo shuleni.

“Mhe. Mwenyekiti tulipitisha azimio na kutoa maelekezo kwa watendaji wa kata na vijiji kwenda kusimamia sheria ya elimu kuhakikisha watoto wanarudi shuleni na hivi tunavyoongea baadhi ya shule karibia watoto wote wamerudi shuleni kuendelea na masomo” alisema Dkt. Nkullo

Aidha alisema kila siku wanapokea taarifa jioni kutoka kwa watendaji wa kata kwani waliwapa idadi ya watoro wa kudumu Katika maeneo yao, akitolea mfano wa shule ya Iduo na Msingisa.

Akiwasilisha taarifa ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2021/2022, Dkt Nkullo alisema katika kipindi cha mwaka ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa ilipokea fedha jumla ya Tshs 36,521,240,291.1 kutokana na vyanzo mbalimbali sawa na 90.1% ya makisio ya mwaka ya jumla ya Tshs 40,546,871,777.

Alisema kati ya fedha hizi, Tshs 3,431,790,010.8 sawa na 107% ya lengo la Tshs 3,207,487,500 kwa mwaka zimetokana na vyanzo vya ndani vya Halmashauri na Tshs 21,689,163,547 sawa na 85.7% ya lengo la Tshs 25,316,277,777 ni ruzuku toka Serikali kuu kwa ajili ya kulipia mishahara.

Aidha kwa upande wa matumizi ya kawaida (OC) Halmashauri ilipokea kiasi cha Tsh 665,579,951.6 ambayo ni sawa na 43.8% ya lengo la Tsh 1,519,143,000 kwa mwaka. Aidha kutoka kwa wahisani mbalimbali na Serikali Kuu, zilipokelewa Tshs 10,734,706,781.7 kwa ajili ya miradi ya maendeleo sawa na 102.2% ya makisio ya Tshs 10,503,963,500 kwa mwaka.

Kwa upande wa matumizi alisema, jumla ya Tshs 34,066,674,494.6 zilitumika katika kipindi cha mwaka wa fedha ulioishia 30 Juni, 2022 kwa ajili ya kulipia mishahara, miradi ya maendeleo na matumizi mengineyo sawa na 84% ya makisio ya jumla ya Tshs 40,546,871,777 kwa mwaka.

Kati ya matumizi hayo Tsh 2,828,169,432.10 sawa na 88.2% ya lengo la Tshs 3,207,487,500 zimetokana na vyanzo vya ndani vya Halmashauri.

Aidha kiasi cha Tshs 21,689,163,547 sawa na 85.7% ya lengo la Tshs 25,316,277,777 ni ruzuku ya mishahara. kwa upande wa fedha za matumizi ya kawaida (OC) Halmashauri ilitumia kiasi cha Tsh 647,219,033.4 ambayo ni sawa na 42.6% ya makisio ya Tshs 1,519,143,000 kwa mwaka.

Alisema kwa upande wa miradi ya maendeleo Halmashauri ilitumia kiasi cha Tshs 8,902,122,482 ambayo ni sawa na 84.8 % ya jumla ya makisio ya Tshs 10,503,963,500 kwa mwaka.

Mbali na hilo aliwashukuru madiwani, Wakuu wa Idara, Mhe. Mbunge na wataalamu wote wa Halmashauri kwa ushirikiano kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo hilo na Spika Mstaafu Mhe. Job Ndugai aliwataka Madiwani wa Jimbo hilo kuendelea kushirikiana kwa pamoja na kumshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu kuendelea kutoa fedha za maendeleo jimboni humo.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo ambaye pia ni diwani wa Kata ya Kongwa Mhe. White Zuberi Mwanzalila alimshukuru Mhe. Rais kwa kutoa fedha kwa wakati ambazo zimesaidia kwa kiwango kikubwa kutatua baadhi ya kero katika Halmashauri hiyo.

Katika mkutano huo, madiwani hao waliweza kufanya uchaguzi kwa mujibu wa sheria wa kumchagua makamu Mwenyekiti wa Halmashauri pamoja na wenyeviti wa kamati mbalimbali ambapo nafasi ya makamu Mwenyekiti ilichukuliwa na Mhe. Richard Fanuel Mwite Diwani Kata ya Mkoka
Na Maganga Gwensaga, Dodoma
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kongwa, White Zuberi Mwanzalila.
Mbunge wa Kongwa na Spika Mstaafu Mhe. Job Ndugai.
Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Kongwa Dkt. Omary Nkullo.
Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri Mhe. Richard Fanuel Mwite.
Waheshimiwa Madiwani.

No comments:

Powered by Blogger.