LIVE STREAM ADS

Header Ads

Dk. Gwajima awatunuku cheti cha heshima SMAUJATA Singida

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano 0757 43 26 94 ama ripotabmg@gmail.com
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalumu, Dk.Dorothy Gwajima (katikati) akiwakabidhi cheti cha heshima viongozi wa Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii (SMAUJATA) Mkoa wa Singida kwa kufanikiwa katika mapambano dhidi ya ukatili kwa watoto. Kutoka kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Smaujata Wilaya ya Manyoni, Tatu Ramadhani, Makamu Mwenyekiti wa Smaujata Mkoa wa Singida, Ambwene Kajula, Mwenyekiti wa Smaujata, Wilaya ya Manyoni, Juma Amrani na Mwenyekiti wa Smaujata, Wilaya ya Itigi, Hadija Kaherewa.

Na Dotto Mwaibale, Dodoma
Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalumu imetoa cheti cha heshima cha pongezi kwa Shujaa na Maendeleo ya Jamii Tanzania (SMAUJATA) Mkoa wa Singida kutokana na kufanikiwa katika mapambano dhidi ya ukatili kwa watoto.

SMAUJATA Mkoa wa Singida imepewa cheti hicho katika kilele cha Siku ya Mtoto wa Afrika kilichofanyika Jijini Dodoma na kuhudhuriwa na Waziri wa wizara hiyo, Dk. Dorothy Gwajima ambaye alimkabidhi Makamu Mwenyekiti wa SMAUJATA Mkoa wa Singida, Ambwene Kajula.

Akizungumza wakati akikabidhi cheti hicho, Dk. Gwajima aliwashukuru wanasmaujata wote nchi nzima kwa mchango wao mkubwa walioufanya katika kuwatetea watoto ambapo alitumia nafasi hiyo kuyaomba mashirika mbalimbali na watumishi wa Serikali na wizara kwa ujumla kuwatumia wanasmaujata katika kufanya kazi za jamii hasa zinazowahusu watoto kwani tayari wameonesha umahiri na uaminifu katika suala zima la kupinga ukatili dhidi ya watoto.

Aidha, Gwajima aliwataka Smaujata wote nchini kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kwa weledi na kuwa tuzo za Smaujata Day bado zipo zitatolewa wakati wa siku 16 za maadhimisho ya kupinga ukatili wa kijinsia itakayofanyika baadae.

Naye Mwenyekiti wa Smaujata Taifa, Sospeter Bulugu, aliwataka wanasmaujata kuendelea kushikamana na kwamba kwa sasa wako kwenye mchakato wa kuanzisha jumuiya ambayo itasaidia kuwaweka pamoja na kujitanua zaidi katika shughuli zao.

Pia Bulugu aliwataka wanasmaujata kurejea kwenye malengo yao kwani kupinga ukatili ni moja ya kipengele kidogo kati ya mambo mengi waliyonayo na akatumia nafasi hiyo kuwahimiza wananchi kujiunga na Smaujata kwani ni ya watanzania wote.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa SMAUJATA Mkoa Singida, Shujaa Dismas Kombe ameishukuru Wizara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalumu kwa kutambua mchango mkubwa wa Smaujata mkoani hapa katika mapambano dhidi ya ukatili kwa watoto na kuamua kuwatunuku cheti hicho cha heshima.

“ Heshima hii pamoja na pongezi hizi ziwafikie mashujaa na wadau wote katika mkoa wetu wakiwemo maafisa ustawi wa viongozi wa dini,walimu, viongozi wa chama na Serikali ambao kwa namna moja ama nyingine wameshirikiana na SMAUJATA katika mapambano haya ya ukatili dhidi ya watoto,” alisema Kombe.

Alisema cheti hicho walichotunukiwa kitakuwa chachu ya kuongeza mapambano dhidi ya vitendo hivyo ambavyo vimekithiri katika maeneo mengi na kuwa ushirikiano baina yao ndio njia pekee itakayosaidia kuutokomeza ukatili huo katika jamii.

Katika kilele hicho cha Siku ya Mtoto wa Afrika Mwasisi wa kaulimbiu ya kupinga ukatili Kitaifa ya 'Don't Touch' ambaye alipongezwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ya kupinga ukatili, Mkaguzi wa Polisi, Francis Msuku kutoka Kata ya Gambushi mkoani Simiyu, Bariadi alikuwa kivutio huku kila mshiriki wa siku hiyo akitaka kuzungumza na kupiga picha naye,

Kutokana na kazi nzuri iliyotukuka anayoifanya ya mapambano ya ukatili katika kata hiyo Machifu na Viongozi wa Utamaduni walifurahishwa na utendaji kazi wa Polisi Jamii chini ya uongozi wake na kufikia hatua ya kumtunuku heshima ya kuwa chifu kutokana na kukomesha vitendo vyote vya ukatili ndani ya kata hiyo.
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalumu, Dk.Dorothy Gwajima,akimkabidhi cheti cha heshima, Mwenyekiti wa SMAUJATA Taifa, Sospeter Mlugu katika hafla hiyo.
Mashujaa wa Smaujata wa Mkoa wa Singida wakiwa katika picha ya pamoja huku wakionesha cheti hicho cha heshima.
Makamu Mwenyekiti wa Smaujata Wilaya ya Manyoni akionesha cheti hicho.
Mashujaa wa Smaujata wakifurahia jambo na Mkaguzi wa Polisi, Francis Msuku kutoka Kata ya Gambushi mkoani Simiyu, Bariadi ambaye ni Mwasisi wa Kaulimbiu ya kupinga ukatili kitaifa ya 'Don't Touch' na shujaa namba moja katika mapambano ya ukatili wa kijinsia hapa nchini.
Mashujaa wakionesha ngao iliyotolewa na Dk.Dorothy Gwajima kwa SMAUJATA Taifa kutokana na mapambano wanayofanya katika kutokemeza vitendo vya ukatili.
Ngao hiyo ikioneshwa.
Ngao hiyo ikiendelea kuoneshwa.
Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalumu, Dk.Dorothy Gwajima (katikati), akionesha upendo kwa kupiga picha na baadhi ya mashujaa wa SMAUJATA.
Maaashujaa wakiwa katika picha ya pamoja.

No comments:

Powered by Blogger.