LIVE STREAM ADS

Header Ads

DC Mongella akoshwa na utekelezaji wa miradi ya maendeleo

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Mkuu wa Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma, Gerald Mongella akimtwisha ndoo ya maji mmoja wa akina mama baada ya kuzindua mradi wa maji.

Na Gideon Gregory, Chemba
Mkuu wa Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma, Gerald Mongella amewahimiza wakazi wa kijiji cha Mrijo Juu wilayani Chemba kuhakikisha wanatunza vyema kisima cha maji ambacho kimechimbwa kwa msaada wa kituo cha ushauri nasaha, lishe na afya (CONSENUTH) kwa kushirikiana na nchi ya Ireland.

Mongella ameyasema hayo Agosti 24,2023 wakati wa uzinduzi wa kisima hicho ambapo amesema adui mkubwa ni yule atakayekwenda kuchezea chanzo cha maji na kuongeza kuwa tayari visima 12 vimeisha chimbwa huku vitano vikiwa vimesalia kufikia jumla 17.

"Naomba muungane na mimi kuwapongeza CONSENUTH kwa kuitekeleza Ilani ya CCM ya mwaka 2025 pamoja na bidii katika kumtua mama ndoo kichwani pamoja na katika miradi ya afya,elimu na mazingira" amesema Mongella.

Mongella,amesema wataendelea kutoa ushirikiano kwa Shirika hilo huku akiwataka wananchi kulinda miradi iliyotekelezwa.

"CONSENUTH mmetusaidia kuondoa utapiamlo na mmewekeza katika hali ya lishe hasa kwa wamama wajawazito na usawa wa kijinsia na pia mmetusaidia kuwajengea Stadi za maisha wanafunzi na upatikanaji wa Maji" amesema Mkuu huyo wa Wilaya.

Mkuu huyo wa wilaya ameomba wananchi kutunza kwa hali na mali vyanzo vya maji huku kwenye elimu akiwaomba wahusika wayatumie maarifa ambayo wameyapata.

Amewaomba katika miaka 25 ya mbeleni, CONSENUTH waone Chemba kama nyumbani kwao na wasipungukiwe kupeleka miradi.

"Miradi mliyotupatia mmetugusa sana,tunazidi kuomba, kwamba hata mkija kuongeza project yetu au majaribio msitusahau sisi Chemba kwa sababu mmefanya miradi ya mfano ndugu zangu akufaae kwa elimu, afya na mazingira huyo ni ndugu yako, CONSENUTH nyie ni ndugu zetu" amesema.

Amesema amezisikia changamoto ikiwemo ushiriki wa viongozi katika masuala ya kijinsia pamoja na wanaume kujojitokeza katika masuala ya kijinsia hivyo watayafanyia kazi.

"Napenda kuwahakikishia tunaenda katika Chemba mpya, hivyo ni mategemeo ya kupandisha Wilaya katika 5 Bora katika matokeo ya darasa la saba yatafanikiwa" amesema

Mhe. Mongella amewaomba wakazi wa Wilaya hiyo waache kuhamasisha watoto wasifanye vizuri katika mitihani na masomo.

"Naomba tuendelee kujitokeza katika shughuli zote za kujitolea.Endeleeni kudumisha amani na mshirikiane katika kuleta Maendeleo"amesema Mkuu huyo wa Wilaya.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa CONSENUTH, Shakila Mayumana amesema mradi wa lishe ya kijinsia umeanza kutekelezwa miaka 4 iliyopita ukiwa na lengo la kupunguza udumavu kwa watoto katika siku 1000 za mwanzo, hali ya lishe ya wanawake, vijana na watoto.

Amesema mradi huo umetekeleza katika shule 52 zilizopo katika Halmashauri za Chemba na kwamba unahamasisha matunzo kwa wanawake na watoto ili kuzuia utapiamlo.

Mkurugenzi huyo amesema kwenye afya za stadi za maisha shuleni zimewasaidia walimu kuwaongezea ujuzi wanafunzi.

''Kwenye tabia nchi tumetelekeza uchimbaji wa visima 12 katika vijiji 12 katika Halmashauri ya Chemba, uvunaji wa maji ya mvua na upandaji wa miti ya matunda na vivuli mashuleni'', amesema Shakila.

Amesema mradi huo umefanikiwa kuchangia kuijengea Halmashauri katika masuala ya lishe na kupunguza kwa asilimia 38 ya udumavu.

Amesema mradi umefanya utafiti wa maji katika vijiji 18 katika Halmashauri hiyo.

Kuhusu Changamoto amesema ni ushiriki hafifu kwa baadhi ya viongozi,mwamko mdogo kwa wanaume na wajawazito kuendelea kijifungulia nyumbani.

Amesema mapendekezo ni Halmashauri iendelee kushirikiana na wadau pamoja na kijijengea uwezo wa kuendesha miradi.

Naye Mwakilishi wa Ubalozi wa Ireland, Nancy Katalai amesema ubalozi wa nchi hiyo kwa muda mrefu umeelewa kuwa sababu za lishe duni na athari zake zinahusiana kwa karibu na sifa za kitamaduni ikiwemo kaya na jamii ambapo wanawake wanakosa mamlaka ya kufanya maamuzi ndani ya nyumba.

Awali akisoma risala ya mbele ya mgeni rasmi, Mtendaji Kata ya Mrijo JuuJesca Njiga amesema kisima hicho kimechimbwa na asasi ya COUNSENUTH kwa ufadhili wa Irish Aid kwa kushirikiana na serikali kupitia mradi wa lishe kijinsia.

“Kisima hiki kinauwezo wa kuzalisha lita 8000 kwa saa hivyo kitapunguza adha ya maji iliyokuwa ikiwakabili wananchi wetu kwa muda mrefu” amesema Njiga.

Njiga ameongeza kuwa kisima hicho hutumiwa na wafugaji kunyweshea mifugo yao, hivyo mradi huo utasaidia kuimarisha sekta ya ufugaji kijijini hapo.

Nao baadhi ya wanakijiji wa Mrijo Juu wameipongeza CONSENUTH kwa juhudi zao katika kuhakikisha wanatatua changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji ambayo wamesema itawasaidia pia kukabiliana na udumavu unaowakabili watoto.
Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Gerald Mongella akizungumza wakati wa maadhimisho ya mafanikio ya mradi wa lishe kijinsia Chemba unaosimamiwa na Kituo cha Ushauri Nasaha, Lishe na Afya (COUNSENUTH). 
Mkurugenzi Mtendaji wa COUNSENUTH, Shakila Mayumana akizungumza kwenye maadhimisho hayo.
Mwakilishi wa Ubalozi wa Ireland, Nancy Katalai akizungumza wakati wa maadhimisho hayo.

No comments:

Powered by Blogger.