LIVE STREAM ADS

Header Ads

NSSF yawasisitiza watumishi kutojihusisha na vitendo vya rushwa

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Singida, Dk. Mohammed Kilolile (katikati) ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya ufunguzi wa maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja iliyofanyika Ofisi ya NSSF Mkoa wa Singida Oktoba 02, 2023 na Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa (kushoto) na Meneja wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Mkoa wa Singida, Beda Mgonja wakikata keki maalum iliyoandaliwa kwa ajili ya uzinduzi huo.


Na Dotto Mwaibale, Singida
Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii, (NSSF) umewasisitizia wafanyakazi wake kutojihusisha na rushwa na masuala mbalimbali yanayoweza kuchafua taswira ya mfuko huo hasa baada ya mafanikio makubwa ambayo umeyafikia kwa kipindi cha mwaka 2022/2023.

Hayo yamebainishwa na Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Singida, Dk.Mohammed Kilolile ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya ufunguzi wa maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja iliyofanyika Ofisi ya NSSF Mkoa wa Singida Oktoba 2, 2023.

“Nichukue fursa hii kusisitiza juu ya masuala mbalimbali yanayochafua taswira ya mfuko wetu licha ya mafanikio makubwa ambayo umeyafikia kwa kipindi cha mwaka 2022/2023 nitoe rai kwa kila mmoja wenu kujitathimini na kuweza kuchukua hatua za dhati na za haraka kukabiliana na mambo yote yanayoweza kudhoofisha kazi zenu” amesema Kilolile.

Kilolile ametaja baadhi ya mambo hayo yanayoweza kutoa imani na kudumisha imani kwa wanachama na wadau wao ni rushwa na kuwa ina madhara makubwa kwa mfuko huo na kwa kila mmoja wao na pia ni adui mkubwa wa haki na inaharibu sifa nzuri ya mfuko ambayo imejengeka kwa muda mrefu.

Kilolile amesema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan inapinga rushwa kwa vitendo, nao wanaunga mkono juhudi hizo kwa kupinga na kukemea masuala yote ya rushwa ndani ya mfuko huo na kuwa katika suala hilo hawatakuwa na huruma, watawabaini na kuwashughulikia wote wanaojihusisha na vitendo vya rushwa kwa kushirikiana na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU).

“Nitoe rai kwa mtumishi yeyote wa mfuko kuacha mara moja vitendo vyote vya rushwa au vinavyoashiria mazingira ya rushwa katika kutoa huduma. Niwaombe pia wanachama na wateja wetu wote kutambua kuwa huduma zinazotolewa na mfuko ni bure na ni wajibu wa kila mtumishi kutoa huduma kulingana na mkataba wa huduma kwa wateja uliopo katika tovuti yetu” amesema Kilolile.

Amesema mfuko huo umeweka utaratibu wa ndani wa kutoa taarifa dhidi ya watumishi wanaojihusisha na vitendo vya rushwa na unaahidi kushughulikia taarifa hizo kwa usiri ili kulinda utambulisho wa watoa taarifa hivyo alisisitiza watumishi wote kutoa taarifa za vitendo vya rushwa vinavyotendeka katika maeneo yao ya kazi kwani kutokutoa taarifa ni kushiriki rushwa. sambamba na hilo, mfuko utaandaa utaratibu wa kuwazawadia watoa taarifa na zoezi hilo pia litafanyika kwa usiri.

Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida Oscar Kalimilwa amesema wiki ya huduma kwa wateja ilianzishwa rasmi kimataifa mwaka 1984 kwa lengo la kutambua umuhimu wa huduma bora kwa wateja na juhudi za wafanyakazi wanaotoa huduma bora kwa wateja.

Amesema kwa mwaka huu 2023 maadhimisho yanaanza Oktoba 2, 2023 na kilele chake ni Oktoba 06 , 2023.

Kalimilwa amesema katika kutambua umuhimu wa huduma bora na kazi kubwa inayofanywa na watumishi, mfuko umeandaa hafla hiyo fupi ili kuwashukuru wateja kwa ushirikiano wanaotoa kwa mfuko na kuwapa watumishi hamasa, kutambua mchango mkubwa wanaoufanya katika kuwahudumia wateja wao na kuamsha ari miongoni mwao ili kuendelea kutoa huduma bora na kuvaa viatu vya wateja wao wanapowahudumia huku wakizingatia miongozo na kanuni za ulipaji wa mafao na matekelezo.

“Kwa kuwa mtoa huduma namba moja ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, mfuko unatumia hafla hii kumpongeza na kumshukuru kwa juhudi kubwa zilizofanywa na zinazoendelea kufanywa na Serikali ya awamu ya sita kwa namna inavyotoa huduma za jamii” amesema Kalimilwa.

Amesema Sisi sote ni mashuhuda wa madarasa bora na ya kisasa yaliyokamilishwa, ukamilishaji wa miradi ya kimkakati kama miundo mbinu ambayo kwa pamoja ina lengo la kufikisha huduma kwa wananchi na kuchochea kuimarika kwa uchumi wa mwananchi mmoja mmoja na nchi kwa ujumla. Vilevile, mfuko unampongeza Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoshughulikia masuala ya Hifadhi ya Jamii ikiwemo malipo ya wastaafu kwa wakati, watumishi waliokuwa na changamoto za vyeti na pia anavyohakikisha masilahi ya wanachama wa Mifuko yanalindwa na kuboreshwa mara kwa mara.

Aidha, Kalimilwa ametumia nafasi hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu na Bodi ya wadhamini kuwashukuru na kuwapongeza watumishi wote kuanzia Menejimenti, Mameneja, Maafisa wakuu, Maafisa waandamizi, maafisa na watumishi wote kwa ujumla pamoja na watoa huduma mbalimbali kwenye ofisi zetu kama vile usafi, ulinzi nakadhalika kwa juhudi kubwa za pamoja wanazozifanya katika kuwahudumia wanachama wao, mfuko unatambua mchango wao katika kutekeleza majukumu waliyonayo.

Amesema katika siku hiyo ya ufunguzi wa maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja wanapenda kuwafahamisha wanachama wao kuwa wanatambua umuhimu na mchango wao kwenye mfuko, na kuwa bila wao hakuna uendelevu wa mfuko huo hivyo unawaahidi huduma bora zaidi na endelevu‘Ushirikiano kwa Huduma Bora, ‘Team work for service Excellency’ .

Meneja wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Mkoa wa Singida, Beda Mgonja ambaye alikuwa mgeni mualikwa kwenye hafla hiyo amesema kauli mbiu ya huduma kwa wateja kwa mwaka huu isemayo, Team Work inawapa faida kubwa kwani jambo hilo linawaondolea mambo mengi hata mtu akiwa na msongo wa mawazo huisha na hutoa huduma nzuri.

Mmoja wa wastaafu wa NSSF Mkoa Singida Joseph Gidatu ameipongeza NSSF kwa kuendelea kuhudumia na kujali wastaafu kwa kuwapatia mafao yao kwa wakati.

Wastaafu Mwamvita Singano, Erick Mnanka na Fatuma Daniel wameishukuru NSSF kwa huduma inayoitoa kwa kutoa pensheni zao kwa wakati na wakampongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha mifuko ya jamii.

Singano ametoa mwito kwa wananchi na wajasiriamali kwenda kujiunga na NSSF na kujiwekea akiba zao kila mwezi ya Sh.20,000 ambayo itakuja kuwasaidia baadae.
Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Singida, Dk.Mohammed Kilolile (kulia) ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye hafla ya ufunguzi wa maadhimisho ya wiki ya huduma kwa wateja iliyofanyika Ofisi ya NSSF Mkoa wa Singida Oktoba 02, 2023 akilisha keki Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida Oscar Kalimilwa.
Mstaafu wa NSSF Mkoa Singida, Joseph Gidatu akimlisha keki mgeni rasmi.
Meneja wa NSSF Mkoa wa Singida, Oscar Kalimilwa akimkaribisha mgeni rasmi kwenye hafla hiyo..
Wageni waalikwa wakikaribishwa.
Meneja wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) Mkoa wa Singida, Beda Mgonja, akizungumza kwenye hafla hiyo.
Wageni waalikwa wakikaribishwa.
Huduma zikiendelea kutolewa kwenye hafla hiyo.
Afisa Huduma kwa Wateja NSSF Mkoa wa Singida, Latifa Singano (kulia) akitoa huduma kwa mteja Fatuma Daniel wakati wa uzinduzi wa wiki ya huduma kwa wateja.
Katibu Muhtasi wa Meneja NSSF Mkoa wa Singida, Asha Iddi akilishwa keki.
Mshereheshaji ( MC) wa hafla hiyo, Abdulmalik Ameir akilishwa keki.
Wateja wakiendelea kupata huduma.
Viongozi wakiwa tayari kwa hafla ya uzinduzi huo.
Hafla ikiendelea.
Mgeni rami wa hafla hiyo akimlisha keki Mstaafu wa NSSF, Joseph Gidatu.
Wageni waalikwa wakiendelea kulishwa keki
Keki zikiliwa.
Hafla ikiendelea.
Picha ya pamoja na mgeni rasmi.

No comments:

Powered by Blogger.