LIVE STREAM ADS

Header Ads

Waziri Slaa awaonya watumishi wazembe

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa (katikati) akizungumza Oktoba 10, 2023 na viongozi na watumishi wa sekta ya ardhi Mkoa wa Singida akiwa kwenye ziara yake ya kikazi ya siku moja ya kufuatilia utekelezaji wa maamuzi ya Baraza la Mawaziri kuhusu utatuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi katika vijiji 975. 

Kulia ni Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Shamim Hoza na Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mkoa wa Singida, Judith Mwalongo.
***


Na Dotto Mwaibale, Singida
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa amesema kuanzia sasa mtumishi yeyote wa wizara hiyo atakaye kiuka miiko na maadili ya kazi hatavumiliwa.

Silaa ameyasema hayo Oktoba 10, 2023 wakati akizungumza na viongozi na watumishi wa sekta ya ardhi Mkoa wa Singida akiwa kwenye ziara yake ya kikazi ya siku moja ya kufuatilia utekelezaji wa maamuzi ya Baraza la Mawaziri kuhusu utatuzi wa migogoro ya matumizi ya ardhi katika vijiji 975.

Amesema kuna migogoro ya ardhi ambayo inatatulika na mingi inasababishwa na utendaji mbovu wa baadhi ya waliopewa kusimamia kazi hiyo na wanapofanya makosa wamekuwa wakihamishwa kutoka sehemu alipofanyia kosa na kupelekwa kituo kingine cha kazi jambo ambalo katika kipindi atakachokuwepo kwenye wizara hiyo hatakiendekeza.

“Mfanyakazi atakayefanya kosa nitamalizana naye papo hapo sitahitaji kumpeleka kwingine” amesema Silaa ingawa hakufafanua atamalizana naye kivipi mfanyakazi huyo atakayebainika kutenda kosa.

Silaa amewataka wafanyakazi wa wizara hiyo kufanya kazi zao kwa kufuata sheria na haki akiamini kuwa ni wanataaluma na si vinginevyo.

Aidha amesisitiza watendaji wa sekta ya ardhi nchini kuhakikisha ndani ya siku mia moja kuanzia Septemba 04, 2023 wanatatua migogoro ya ardhi ili kuwafanya wananchi wawe na imani na Serikali yao na kuifurahia wizara hiyo.

Amesema hatapenda kuona wananchi wakiinua mabango pale viongozi wakitaifa wanapokuwa kwenye ziara katika maeneo mbalimbali wakilalamikia migogoro ya ardhi.

Hata hivyo amepongeza ofisi ya Kamishna wa Ardhi Mkoa wa Singida kwa umahiri na ustadi wa utendaji katika zana pana ya kushughulikia migogoro mbalimbali ya ardhi sambamba na hatua nzuri za upimaji, umilikishaji na usimamizi wa matumizi bora ya ardhi mkoani hapa.

Pia amelipongeza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa ukusanyaji madhubuti wa mapato na ufanisi wa kiutendaji huku akiwataka watendaji kuendelea kuchapa kazi wakati Serikali inaangalia namna ya kutatua changamoto zilizopo.

Hata hivyo Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Shamim Hoza pamoja na kumshukuru waziri kwa ziara hiyo amemuhakikishia kwamba wafanyakazi watazingatia maagizo yote yaliyotolewa kwa tija, ukuaji na mstakabari mzuri wa sekta nzima ya ardhi ndani ya Mkoa wa Singida.

Pia Hoza ameshauri uwepo wa dhana ya ushirikishwaji baina ya watumishi wa sekta ya ardhi katika kutekeleza majukumu mbalimbali ili kuondoa migongano ambayo huathiri utendaji ndani ya sekta hiyo.

Akizungumzia mafanikio amesema ofisi yao kwa mwaka 2021 imefanikiwa kuandaa michoro 61 kwenye viwanja 19,620 na kueleza kuwa idadi hiyo inapanda kadri wanavyoendelea kutoa elimu kwa wananchi na kuwa changamoto kubwa waliyonayo ni uhaba wa watumishi katika kada zote, kuwa na gari moja na ufinyu wa bajeti.

Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mkoa wa Singida, Judith Mwalongo alisema Mkoa wa Singida una jumla ya majengo 39 yakiwa na jumla ya nyumba (units) 171, ambapo asilimia 90 ya nyumba hizo zipo katikati ya mji wa Singida.

Mwalongo amesema Mkoa umeongeza mapato kwa mwaka 2022/2023 kwa kuongeza bili ya mwezi kutoka Sh.Milioni 45.8 (kabla ya VAT) mwezi Juni 2023 mpaka Sh.Milioni 54.9 (kabla ya VAT) mwezi Juni 2023 sawa na ongezeko la asilimia 20 kwa kipindi cha Julai 2023 mpaka Septemba, bili ya mwezi imeongezeka kutoka sh. Milioni 54.9 (kabla ya VAT) mpaka Sh.Milioni 58.071 (kabla ya VAT)_ sawa na ongezeko la asilimia 6.

Akizungumzia makusanyo ya kodi amesema kwa mwaka wa fedha 2022/2023 mkoa ulitakiwa kukusanya jumla ya Sh.Milioni 611,4 (pamoja na VAT) na mpaka wanafunga mwaka huo wa fedha wamefanikiwa kukusanya jumla ya Sh.Milioni 756,6 (pamoja na VAT) ambayo ni sawa na 123.7 asilimia.

Amesema mwaka huu wa fedha kwa kipindi cha Julai mpaka Septemba 2023 walitakiwa kukusanya Sh.Milioni 186,3 (pamoja na VAT) mpaka sasa wamekusanya jumla ya Sh.Milioni 239,5.

Mwalongo amesema Mkoa wa Singida utaendelea kuhakikisha unatekeleza majukumu yake ikiwemo kuhakikisha kodi inakusanywa kikamilifu pamoja na kuhakikisha madeni hayoongezeki bali yanapungua.

Amesema mkoa utaendelea kulishirikisha shirika juu ya fursa zilizopo mkoani Singida (uwepo wa viwanja vya wazi, uwepo wa viwanja vyenye majengo chakavu katika maeneo ya kimkakati na uhitaji wa nyumba za makazi na biashara) ili waweze kuzitumia kikamilifu katika kuhakikisha wanaongeza mapato ya mkoa na shirika kwa ujumla.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa akisalimiana na Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Shamim Hoza mara alipowasili ofisi za Ardhi Mkoa wa Singida wakati wa ziara hiyo. Katikati ni Mpima ardhi Mkoa wa Singida, Sesaria Williams na kushoto ni Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi Wilaya ya Singida, Bahati Colex.
Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Shamim Hoza akisoma taarifa ya utekelezaji wa mipango ya Sekta ya Ardhi kwa mwaka 2023/2024.
Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Mkoa wa Singida, Judith Mwalongo akisoma taarifa ya utekelezaji ya shirika hilo.
Wafanyakazi wa Ofisi ya Ardhi Mkoa wa Singida wakiwa tayari kwa mapokezi ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa. Kushoto ni Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi Wilaya ya Singida, Bahati Colex.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa akisalimiana na wafanyakazi wa ofisi hiyo.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa akisalimiana na Msaidizi wa Kumbukumbu Ofisi ya Kamishna Msaidizi wa Ardhi Mkoa wa Singida, Hasna Adam.
Wafanyakazi wa Sekta ya Ardhi Mkoa wa Singida wakiomba sala maalumu ya kuiombea ofisi na watumishi.
Watumishi sekta ya ardhi wakiwa kwenye kikao hicho.
Kikao kikiendelea.
Watumishi sekta ya ardhi wakiwa kwenye kikao hicho.
Kikao kikiendelea.
Taswira ya kikao hicho.
Picha ya pamoja na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa.
Picha ya pamoja.
Picha ya pamoja na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa.
Picha ya pamoja.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi wa Sekta ya Ardhi Wilaya ya Ikungi.

No comments:

Powered by Blogger.