LIVE STREAM ADS

Header Ads

TGNP yajivunia ongezeko la wanawake katika huduma za kifedha

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

Katika kuadhimisha Siku Wanawake Duniani, Mtandao wa Jinsia Tanzania- TGNP kwa kushirikiana na wadau wake wamejipanga kuwa na mtiririko wa matukio mbalimbali kuanzia ngazi ya jamii kupitia Vituo vya Taarifa na Maarifa pamoja na kuwezesha mazungumzo rika yanayounganisha wanawake vijana na wanawake wabobevu katika nyanja mbalimbali.

Ameyasema hayo leo Machi 6,2024 Jijini Dar es Salaam wakati TGNP wakiadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP-Mtandao, Bi. Lilian Liundi amesema maadhimisho hayo yanawapa nafasi ya kutafakari kwa ujumla kuhusu changamoto zinazokwamisha ushiriki wa wanawake katika nafasi za maamuzi na uongozi na kuweka mikakati ya namna ya kuzitatua.

Aidha amesema mpaka sasa kumekuwa na mafanikio makubwa katika kuhakikisha mwanamke anapewa haki zake za msingi, mafanikio hayo ni pamoja na kuongezeka kwa idadi ya wanawake wanaoshiriki katika nafasi mbalimbali za uongozi.

"Nchi yetu imeweka historia ya kuwa na Rais Mwanamke kwa mara ya kwanza, Dkt Samia Suluhu Hassan, ambaye ameonesha dhamira ya kuongeza usawa wa kijinsia; tumesha kuwa na Maspika wa Bunge wawili wanawake, ambao ni Mhe. Anne Makinda na Mhe. Dkt Tulia Ackson; mawaziri wanawake walioshika nafasi katika wizara zinazoamikika kuwa ni za wanaume, kama Wizara ya Ulinzi- Mhe. Stigomena Tax, Wizara ya Mambo ya nje, Mhe, Liberata Mulamula". Amesema

Amesema mafanikio mengine ni pamoja na Umiliki wa Rasilimali za Uzalishaji ambapo takwimu zinaonesha kuwa asilimia 27 tu ya wanawake wanamiki ardhi. Kwa upande mwingine, kumekuwa na jitihada za kuwezesha wanawake kupata na kunufaika na huduma za kifedha, ambapo jitihada hizo zimepunguza pengo la kijinsia kutoka asilimia 10 mwaka 2017 hadi asilimia 3.6 mwaka 2023.

"Kwa mfano, tunatambua mchango wa Halmashauri kupitia vyanzo vya ndani ya mapato ambao hadi 2022, serikali imetoa jumla ya shilingi bilioni 63.4 ikiwa ni mikopo yenye masharti nafuu kwa vikundi 26,733 vya wanawake vinavyojumuisha wanawake 938,802 katika Halmashauri mbalimbali, vikundi vya vijana 10,741 na watu wenye ulemavu 1,270". Amesema Dada Gemma.

Pamoja na hayo amesema kuwa kwa upande wa upatikanaji wa huduma ya afya, bado kuna changamoto ya vifo vya wanawake wakati wa kujifungua, wanawake 238 katika kila wanawake 100,000 hupoteza maisha wakati wa kujifungua, hatujaweza kufikia lengo tulilojiwekea la kupunguza vifo hadi 200 kati ya vizazi 100,000.

"Inasikitisha sana kuona wanawake wanaoleta nguvu kazi ya taifa wanapoteza maisha yao wakati wa uzazi. Takribani asilimia 20 ya wanawake hujifungulia nje ya huduma rasmi za afya jambo ambalo linahatarisha maisha yao". Ameeleza.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi TGNP, Bi. Gemma Akilimali amesema kwa kutambua umuhimu na mchango mkubwa wa wanawake, ambao ni zaidi ya nusu ya watanzania wote (51.3% kwa mujibu wa Sensa ya 2022), katika maendeleo ya nchi, Serikali imetia saini mikataba mbalimbali ya Kimataifa na Kikanda inayoweka misingi ya usawa kwa binadamu ikiwemo haki na usawa katika ushiriki kwenye uongozi wa ngazi zote.

"Miongoni mwa mikataba hiyo ni Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu (UDHR: 1948), Mkataba wa Kimataifa wa Kutokomeza aina zote za Ubaguzi dhidi ya Wanawake (CEDAW: 1979), Mpango Kazi wa Beijing (1995), Mkataba wa Ziada wa Maputo, na Mkataba wa Hiari wa Jinsia na Maendeleo kusini mwa Afrika (SADC Gender and Development Protocol 2003,) ambayo inaelekeza serikali husika kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi sawa na wanaume katika ngazi mbalimbali za uongozi". Amesema Dada Gemma.

Hata hivyo Bi. Liundi ameeleza kuwa Tanzania kupitia Dira ya Maendeleo ya 2025 (TDV 2025) ukurasa wa 16 imetambua kuwa mojawapo ya vichocheo vya ukuaji wa uchumi ni pamoja na jamii yenye muono wa kimaendeleo ambapo pamoja na mambo mengine unakuwa na tamaduni wezeshi hususani kwa wanawake na makundi mengine.
Mwenyekiti wa Bodi TGNP, Bi. Gemma Akilimali akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo TGNP wameanzisha leo Machi 6, 2024 kwenye viwanja vya TGNP-Mtandao Jijini Dar es Salaam. Maadhimisho ya Mwaka huu yankwenda na kauli mbiu isemayo "Wekeza kwa Wanawake, Kuharakisha Maendeleo ya Taifa na Ustawi wa Jamii’.
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP-Mtandao, Bi. Lilian Liundi akizungumza wakati wa maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo TGNP wameanzisha leo Machi 6, 2024 kwenye viwanja vya TGNP-Mtandao Jijini Dar es Salaam. Maadhimisho ya Mwaka huu yankwenda na kauli mbiu isemayo "Wekeza kwa Wanawake, Kuharakisha Maendeleo ya Taifa na Ustawi wa Jamii’.
Picha mbalimbali za wadau ambao wameshiriki maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo TGNP wameadhimisha leo Machi 6, 2024 kwenye viwanja vya TGNP-Mtandao Jijini Dar es Salaam. Maadhimisho ya Mwaka huu yankwenda na kauli mbiu isemayo "Wekeza kwa Wanawake, Kuharakisha Maendeleo ya Taifa na Ustawi wa Jamii’.
Picha mbalimbali za wadau ambao wameshiriki maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo TGNP wameadhimisha leo Machi 6, 2024 kwenye viwanja vya TGNP-Mtandao Jijini Dar es Salaam. Maadhimisho ya Mwaka huu yankwenda na kauli mbiu isemayo "Wekeza kwa Wanawake, Kuharakisha Maendeleo ya Taifa na Ustawi wa Jamii’.
Picha mbalimbali za wadau ambao wameshiriki maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambapo TGNP wameadhimisha leo Machi 6, 2024 kwenye viwanja vya TGNP-Mtandao Jijini Dar es Salaam. Maadhimisho ya Mwaka huu yankwenda na kauli mbiu isemayo "Wekeza kwa Wanawake, Kuharakisha Maendeleo ya Taifa na Ustawi wa Jamii’.

No comments:

Powered by Blogger.