Chuo cha Kolandoto chashiriki maadhimisho ya elimu, ujuzi na ubunifu
Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Chuo cha Sayansi za Afya Kolandoto Shinyanga kimeshiriki maadhimisho kitaifa ya elimu, ujuzi na ubunifu yanayofanyika jijini Tanga kwenye viwanja vya Shule ya sekondari ya Popatlal.
Mkuu wa chuo hicho, Paschal Shiluka amesema Serikali imeboresha maonesho ya mwaka huu, yamekuwa na utofauti mkubwa kwa kuchanganya vyuo vikuu na vyuo vya kati nchi nzima,lakini pia kutoa chachu ya kutamani kupandisha hadhi vyuo vya kati na kuwa vyuo vikuu.
Akizungumzia mafanikio wanayoyapata kupitia maadhimisho hayo ambayo hufanyika kila mwaka kwa mikoa tofauti, amesema kubwa zaidi ni kujifunza kutoka kwa wengine walioshiriki,kuonesha ubunifu na ujuzi wanaotumia kufundisha fani za Afya vyuoni pamoja na kujitangaza kwa kuwa wanakutana na watu wapya wengi.
Ameeleza mafanikio mengine waliyopata kama chuo tangu walivyoanza kushiriki maonesho mwaka 2022, ambapo mwaka 2023 Kwa maonesho yaliyofanyika jijini Arusha waliibuka washindi namba tatu katika vyuo vya Afya vya kati nchini.
Kwa upande wake Afisa masoko wa chuo hicho, Josephine Charles amesema mbali na kozi za awali za uuguzi na Uukunga, Mmaabara, utabibu na famasia kwa sasa chuo chao kimepata kibali cha kuongeza kozi mbili za Radiology na Physiotherapy ambazo zitaanza mwaka huu, hivyo ametumia nafasi hiyo kuwataarifu wanafunzi waliohitimu kidato cha nne na wenye ufaulu wa masomo ya sayansi kuanzia alama D4 wanaweza kutuma maombi.
Amedokeza kuwa kwa wanafunzi wenye sifa ya kujiunga na kozi za maabara, radiology na physiotherapy wanaweza omba mkopo serikalini kwa kuwa Serikali ilishatoa fursa hiyo ya mikopo kwenye vyuo vya kati kwa wanafunzi wa kozi hizo.
Aidha maadhimisho ya mwaka huu yalianza tangu 25 May 2024 na yatahitimishwa mei 31, 2024 ambapo yamefunguliwa na Waziri wa Elimu, Prof. Adolf Mkenda yakiongozwa na kauli mbiu isemayo 'elimu, ujuzi na ubunifu kwa uchumi shindani'.
Mkuu wa Chuo cha sayansi za Afya Kolandoto Shinyanga, Paschal Shiluka akizungunza na waandishi wa habari.
Afisa masoko wa chuo cha Sayansi za Afya Kolandoto Shinyanga akizungumza na waandishi wa habari Tanga.
No comments: