LIVE STREAM ADS

Header Ads

RC Shinyanga atembelea kiwanda cha vipuli

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha ametembelea kiwanda cha EACS kinachozalisha vipuli vya mitambo aina ya 'conveyor' kilichopo Kahama mkoani Shinyanga.

Macha akiwa katika kiwanda hicho amepata wasaa wa kuona mitambo mbalimbali ya kisasa ambayo hutumika kuzalisha vipuli hivyo na vifaa vingine vingi vinavyotumika katika mitambo mbalimbali ya uzalishaji wa uchimbaji madini pamoja na uzalishaji wa saruji ambavyo vinazalishwa kwa teknolojia ya hali ya juu na ubora unaokidhi viwango vya ushindani katika soko la ndani na nje.

Aidha Macha amesema ziara yake katika kiwanda hicho imelenga kujionea namna kiwanda hicho kinavyofanya kazi lakini pia kuona namna ambavyo eneo la Mgodi wa Buzwagi wakati linabadilishiwa matumizi yake na kuwa eneo maalumu la uwekezaji kiuchumi baada ya shughuli za uchimbaji madini zilizokuwa zikifanywa na kampuni ya Barrick kufikia tamati.

"Lengo la Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha mradi huu unaokwenda kuanzishwa wa 'Buzwagi Special Economic Zone' unawanufaisha wananchi wote na kuleta tija ya kuwahudumia jamii yote katika nyanja zote hivyo nampongeza sana mwekezaji wa kiwanda hiki cha EACS" alisema RC Macha.
Kwa upande wake Meneja wa masoko na mauzo wa kiwanda hicho, John Kubini ameishukuru sana Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira Rafiki kwa wawekezaji lakini pia akimshukuru Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Anamringi Macha kwa kutembelea kiwanda hicho.

Aidha amewaomba wawekezaji wa sekta ya madini na viwanda vya uzalishaji wa saruji nchini kutumia vipuli vyao vinavyozalishwa nchini ili kuendelea kukuza uchumi wa nchi.

Kiwanda cha EACS ni miongoni mwa uwekezaji mkubwa katika ukanda wa kanda ya ziwa ambao unafungua fursa za kiuchumi kwa wakazi wa Kahama, Mkoa wa Shinyanga na Tanzania kwa ujumla ambapo mpakasasa inasambaza vifaa vyake kwenye kampuni ya uchimbaji madini Barrick Afrika nzima hivyo hatuna budi kuunga mkono kazi nzurii inayofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan.

No comments:

Powered by Blogger.