LIVE STREAM ADS

Header Ads

Serikali ya Rais Samia yaja na mkakati wa kuboresha barabara Rukwa

Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imekuwa ikifanya jitihada za kuimarisha na kuboresha miundombinu ya barabara ili kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi na kuzilinda ziweze kutumika kwa muda mrefu.

Meneja wa TARURA Mkoa wa Rukwa, Mhandisi Chacha Moseti amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia imefanya kazi kubwa katika kuimarisha mtandao wa barabara ili uweze kupitika kwa misimu yote kwa kutenga fedha mwaka hadi mwaka.

“Tunamshukuru Rais Samia kwa kuongeza bajeti ya TARURA Mkoa wa Rukwa kutoka shilingi Bilioni 5.1 hadi kufikia shilingi Bilioni 12.9, kwa kiasi kikubwa imesaidia kuimarisha mtandao wa barabara katika mkoa wetu” alisema.

“Kupitia ongezeko hilo TARURA mkoa wa Rukwa, inaendelea kutekeleza miradi ya kimkakati kwa kufungua barabara mpya ili kufika kusiko fikika na kuboresha barabara zilizopo ili zipitike wakati wote” aliongeza.

Alisema barabara za lami zimeongezeka kutoka Km 29.33 na kufikia Km 43.14 ambazo ni sawa na ongezeko la Km 13.81%, wamejenga barabara za zege Km 0.631, barabara za changarawe Km 480.76 na ujenzi wa madaraja na maboksi kalavati 147.

Alieleza kuwa waliweza kuongeza idadi ya madaraja na kufungua maeneo yaliyokuwa hayafikiki na sasa yanafikika muda wote kwa kujenga madaraja 17 kwa kutumia teknolojia ya mawe katika Halmashauri za Wilaya ya Sumbawanga, Kalambo na Nkasi.

Aliongeza kuwa, wametekeleza miradi ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa daraja la mto Kalambo lenye urefu wa mita 80 ambalo limenufaisha wananchi wa kata za Sopa na Pombwe wilayani Kalambo kusafirisha mazao yao sokoni kwa urahisi.

Mkazi wa Nkasi, Sarafina Mbalamwezi aliipongeza serikali kwa kile inachokifanya kuhakikisha miradi ya barabara inatekelezwa na kukamilika kwa wakati na wananchi kuondokana na changamoto ya kutembea umbali mrefu kutafuta huduma mbalimbali ikiwemo ya matibabu.

Mkazi wa Sopa wilayani Kalambo, Amon Kabwe alimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ya kuboresha miundombinu vijijini ili kuhakikisha wananchi wanasafiri na kusafirisha mazao yao sokoni kwa urahisi.

TARURA Mkoa wa Rukwa inahudumia mtandao wa barabara wenye urefu wa Kilomita 2,304.26 ambapo kati ya hizo barabara za lami ni Km 44.3, barabara za changarawe Km 1,145.68 na barabara za udongo Km 1,114.28.
#KaziInaongea

No comments:

Powered by Blogger.