LIVE STREAM ADS

Header Ads

SEHEMU YA TATU: TARIME ZIPO MILA ZA KUKUMBATIA, LAKINI SI UKEKETAJI.



Wasichana Wakikeketwa
Suala la wazazi kuwalazimisha mabinti zao kukeketwa linapaswa kukemewa na kupigwa vita kali kwa kuwa limekuwa likikwamisha juhudi hizi za kupambana na ukeketaji, mbaya zaidi wazazi hao wamekuwa wakiwatishia mabinti zao kuwafukuza nyumbani wasipokubali kufanyiwa ukeketaji.

Mfano ni Ghati Chacha na Bhoke Chacha (Si majina yao halisi) ambao ni ndugu wote wakiwa ni wahimu wa kidato cha nne mwaka jana katika shule ya Sekondari Rebu iliyoko Wilayani Tarime, wanaeleza kwamba katika msimu wa ukeketaji wa mwaka 2012 walikumbana na changamoto ya kulazimishwa kwenda kukeketwa lakini waliweza kukataa haswa kutokana na elimu ya madhara ya ukeketaji waliyokuwa wameipata shuleni sanjari na kushuhudia namna dada yao alivyotokwa na damu nyingi pindi alipokeketwa.
“Kwa mfano mimi nililazimishwa kwenda kukeketwa lakini nilikataa, nilipoona wanazidi kunilazimisha ilibidi nikimbie nyumbani hadi msimu wa ukeketaji ulipoisha ndipo nikarudi nyumbani; hivyo nawashauri mabinti wenzangu ni bora mtu ukimbie nyumbani kuliko kukubali kwenda kukeketwa” alisema mmoja wa mabinti hao.

Wazee wa kimila nao bado wanahitaji elimu ya kutosha ili kuweza kutokomeza suala hili la ukeketaji, kwa kuwa wao wanadai kila kabila lina mila yao na hiyo ni mila iliyokuwepo tangu enzi na enzi na haina madhara yoyote katika jamii, kama alivyoeleza mojawapo wa wazee wa kimila kutoka katika koo ya Watimbaru katika kabila la wakurya Wilayani Tarime aliejitambulisha kwa jina la Mwikwabe Mwita Masero.

“Hii mila ilikuwepo tangu zamani; hivyo kama ni kuisha itaisha yenyewe lakini sisi hatuwezi kuizuia kwa kuwa kufanya hivyo tutakuwa tunaingilia mamlaka ya akina mama (Mangariba) na wataona kama tumeipindua serikali yao; japo hatukatai mila hii kutokomezwa lakini ni vyema tukaacha hadi itakapoisha yenyewe” alisema mzee huyo na kuongeza;

“Serikali ndiyo inayozuia ukeketaji lakini sisi hatuoni madhara yake kwani hata mabibi zetu walikeketwa na hawakupata madhara yoyote; hivyo kama ni madhara labda awe nayo mtu mwenyewe lakini sisi hatuwezi kumsababishia mtu madhara kwa kumkeketa” alisema Mzee Masero tena kwa umakini mkubwa. 

Mzee huyo alihitimisha kwa kusema kuwa katika msimu wa ukeketaji ambao hufanyika mara moja kwa mwaka, kila baada ya miaka miwili, idadi ya wasichana wanaofanyiwa ukeketaji inakadiriwa kufikia kati ya elfu tatu hadi elfu nne kwa koo moja, akiitolea mfano koo ya watimbaru.

“Idadi, aaaah mfano katika koo ya watimbaru wanaweza kufika kama elfu tatu au elfu nne hivi kwa msimu,” alisema mzee huyo tena bila mshangao wowote kulingana na idadi hiyo jinsi ilivyokubwa.
MTANZANIA MEDIA: ITAENDELEA...

No comments:

Powered by Blogger.